Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati Hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati Hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kuwapongeza sana Wenyeviti wa Kamati zote mbili kwa ripoti nzuri. Nawapongeza sana Wajumbe ambao ni washiriki wa Kamati hizo kwa ripoti ambazo wametuletea. Nami naomba nikiri kwamba ndani ya Serikali tunawashukuru kwa sababu wanaendelea kutushauri mambo mema na ninaomba kuwahakikishia kwamba tupo pamoja na tutaendelea kuyazingatia ili kujenga ustawi wa Taifa na wa Tanzania kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda kabla sijaendelea nichukue nafasi hii pia kumpongeza sana Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Ni ukweli usiopingika, Rais wetu toka ameingia kwenye Serikali hii ya Awamu ya Tano amefanya kazi kubwa za utekelezaji wa Ilani lakini utekelezaji huo unaowagusa Watanzania wengi. Kwa sasa maendeleo ya Taifa letu yamekuwa ni mtambuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia miradi ya maendeleo ambayo imetekelezwa ndani ya Serikali ya Awamu ya Tano unaiona kabisa mgawanyo wake unawagusa Watanzania kwenye mikoa yote kwa kuzingatia mahitaji na vipaumbele walivyonavyo. Ukisema masuala ya elimu bure, miundombinu ya maji, miundombinu ya barabara, ujenzi wa hospitali mpya, ujenzi wa vituo vya afya, ukarabati wa shule, kabisa Waheshimiwa Wabunge mtakubaliana name kwamba Rais wetu na Serikali wamefanya kazi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo basi, kama tunatekeleza Ilani ya Uchaguzi, Rais wetu na Serikali wanatekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. Hata kuhamia hapa Dodoma haikuwa kukurupuka, ilikuwa ni utekelezaji wa Ilani. Kuhamia hapa Dodoma wote tumekuwa ni mashahidi, hakuna mji wowote ama nchi yoyote ambayo inaweza kukua kiuchumi kama haipanui shughuli za kiuchumi katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wala isingetusaidia, ukiachia mbali kurithi mawazo mazuri ya Baba wa Taifa hili, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambaye ni mwasisi wa Serikali kuhamia Dodoma, lakini Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi na maamuzi dhahiri ya Rais wetu ya kuhamishia Serikali Dodoma yamekuwa na effect ambayo ni positive kwenye kukua kwa uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa nini? Baada ya Serikali kuhamia hapa Dodoma, tumeona kabisa miji inayozunguka hapa Dodoma imeanza kukua. Ukienda Singida inakua, Manyara - Babati kunakua, Iringa inakua na Morogoro inaendelea kukua. Kwa hiyo, kwa kuhamia tu hapa Dodoma unaona ile multiplier effect ya kuhamia Dodoma imeambukiza na Miji mingine ambayo ipo karibu na hapa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini maana yake? Mwisho wa siku tutakuwa tumekuza uchumi katika maeneo mengi ya nchi ya Tanzania, tutaongeza mapato, tutaboresha huduma za jamii, vile vile ukuaji wa uchumi huo utatatua na matatizo mengine ambatanishi kama matatizo ya ajira na mambo mengine kama miundombinu na huduma za jamii. Hapa Dodoma sasa hivi tuna hospitali kubwa ya Benjamin Mkapa, ukiacha mbali ile ya Muhimbili ambayo ilikuwa Dar es Salaam kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposema tumehamia Dodoma, hatujaiacha Dar es Salaam. Dar es Salaam nayo imeendelea kufanyiwa mambo makubwa. Waheshimiwa Wabunge nyie ni mashahidi, katika historia ya nchi hii, miundombinu ya barabara inayojengwa kwa sasa kwenye Jiji la Dar es Salaam ni miundombinu ya hali ya juu. Huo ni ushahidi kabisa. Miundombinu inayowekezwa pale Dar es Salaam itafanya Jiji la Dar es Salaam kuwa ni Jiji la kibiashara na likiwa Jiji la kibiashara litasaidia sana kukuza uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba niseme Waheshimiwa Wabunge, ninadhani sisi kama Wabunge tukihesabu yale yanayofanyika Dar es Salaam na katika Mikoa mingine yote Tanzania, hakika tunayo kila sababu ya kumpongeza sana Rais wetu kwa maamuzi aliyoyafanya katika kipindi chake pamoja na Serikali yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nimtoe hofu dada yangu Mheshimiwa Halima, Mwenyekiti mpya wa Wanawake wa CHADEMA na kumwomba tu aunge mkono juhudi za Rais wetu na hasa pale Dar es Salaam katika kuleta maendeleo. Namwomba afikishe salamu hizi za upendo wa kazi znuri ya Rais wetu kwa wanawake wa CHADEMA nchi nzima na hasa pale Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa hapa suala la Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF). Ninaomba niwaambie Waheshimiwa Wabunge, nakubali NSSF huko nyuma baada ya Serikali yetu kuingia, tumegundua kulikuwa na matatizo makubwa. Sasa tulichokifanya ni kuendelea kuhangaika kuona kwamba ule uwekezaji ambao ulifanyika huko nyuma usiokuwa na tija unarekebishwa haraka ili kuwe na manufaa na tija kwa wanachama na Watanzania kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni hivi juzi tu, tunayo majengo ya muda mrefu Mtoni Kijichi, nimeyakabidhi wa Waziri wa Elimu yatumike kama hosteli za wanafunzi wa elimu ya juu, wanaosoma katika Vyuo Vikuu pale Dar es Salaam. Tumekabidhi hosteli zile mpaka kufika mwezi wa Tatu wanafunzi wasiopungua 4,000 na kitu watapata makazi kwenye zile hosteli mpya. Tutakwenda mpaka nafasi zisizopungua 8,000 na kitu. Kwa hiyo, hiyo ni kazi kubwa, ni lazima muone Serikali inafanya kazi na inajaribu kurekebisha kila ambapo hapakuwa na tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa imetolewa hoja kwamba hili shirika linakufa. Ninachokwenda kufanya sasa hivi ni utathmini wa mfuko (actuarial), hii ndio itatuambia. Hatuwezi kusema kitu kingine chochote, mfuko unakufa bila actuarial.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukichukua facts za kawaida kwa sasa, makusanyo ya shirika mwaka 2018 kwa mwezi yalikuwa shilingi bilioni 60 tu. Kufika mwaka 2019 yameongezeka mpaka shilingi bilioni 96 kwa mwezi. Hilo ni ongezeko na tunaona kumbe shirika linakua. Uwekezaji kwenye dhamana za Serikali ilikuwa ni negative mwaka 2018, lakini baadaye ikaja kuongezeka mpaka 8%. Leo ninaposimama hapa, imefika asilimia 20 kwenye dhamana za Serikali. Kwa hiyo, hilo ni ongezeko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na malimbikizo ya wastaafu yenye thamani ya fedha za Kitanzania shilingi bilioni 109, mpaka kufika 2019 toka hiyo 2018 fedha hizo za malimbikizo na malipo mengine tumeshalipa shilingi bilioni 409. Kwa hiyo, unaona kwamba shirika linaendelea kufanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, daraja la Kigamboni ambalo ndiyo mradi umesemwa hapa, ni kweli una matatizo na tunaufanyia kazi kuyaondoa. Tumeweza kuongeza makusanyo kwenye Daraja la Kigamboni kutoka shilingi bilioni 697 mwaka 2018 mpaka shilingi bilioni 950 mwaka 2019. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge, Serikali imejipanga, tunajua miradi hii ya uwekezaji kwenye Mashirika yetu ya Hifadhi ya Jamii ni fedha za wanachama. Tunachokifanya sasa hivi ni kutembelea mradi mmoja baada ya mwingine, kutafuta namna ya kuhakikisha uwekezaji huo unakuwa na tija kwa wanachama na Watanzania kwa ujumla.

Kwa hiyo, nakubaliana na ushauri walioutoa Waheshimiwa Wabunge, pale ambapo hapajafanyika vizuri, tutafanya vizuri, lakini kama shirika linafanya vizuri, tutaendelea kuwapongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, ahsante sana kwa hoja zilizotolewa. (Makofi)