Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati Hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020

Hon. Shally Josepha Raymond

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati Hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020

MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, kipekee namshukuru Mungu kwa zawadi ya uhai kutuweka wote hapa tuweze kuisemea nchi yetu mambo ya maendeleo na pia tuweze kuishauri Serikali. Awali ya yote naomba niwapongeze sana wenyeviti wote wawili kwa wasilisho lao na pia naomba nichukue nafasi hii rasmi kabisa nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango, Waziri wa Fedha na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji ambao ni wachumi waliobobea na mnaona mabadiliko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze pia Katibu Mkuu Dotto James kwa kubana matumizi, mengine yamesemwa kwenye ripoti na sasa niende tu moja kwa moja kuzungumzia ile sekta ya benki. Kwenye kamati tumekesha na hawa watu, kamati ya bajeti tunatoka saa nne hawali, hawanywi hawachoki, Mheshimiwa Waziri anakuwa Dar es Salaam asubuhi jioni yuko na sisi na tumezungumza mambo mengi. Kuna mambo ambayo tumemshauri na naomba nichukue tena nafasi hii kuweka msisitizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya benki imekaa kibiashara na kweli ni biashara huria lakini Mheshimiwa Rais wetu mpendwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kila leo anataka kumtetea mtu wa chini. Watu wa chini hawa wanaokota fedha zao kidogo kidogo, wanakuwa kwenye vikoba, wanataka kwenda kuweka fedha salama wanapeleka benki na benki wanaweka kwenye savings account wanapata asilimia moja tu (1 percent). 1 percent ikikatwa service fee inakata mpaka ile fedha yao waliyowekeza matokeo yake vikoba wameamua kufanya nini! Wameamua kuvunja vikoba ndani na kugawanya ule mtaji halafu wanaanza upya. Hapa nasimama nazungumzia wale wanawake walionituma hapa Bungeni, wanawake wa Kilimanjaro. Nawashukuru sana kunileta hapa na sitawaangusha nitalizungumzia jambo hili kila siku mpaka benki ziweze kulihuisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiingii akilini, haiingii akili fedha zinavyokusanywa na benki zinakwenda kuwekwa kwenye treasury bonds lakini kwa miaka miwili ni asilimia 8.17, miaka mitano asilimia 10.22, miaka kumi wanalipwa wao asilimia 13, miaka 15 asilimia 15.19 na miaka 20 asilimia 16.71. Shida inatoka wapi! Kweli kuweka ni gharama na pia wanapokuja kulipa hujui yule aliyeweka fedha yake benki ataichukua saa ngapi atetemeshe, lakini kuna wale wazee ambao wanaweka fedha benki na wanaweka tu mpaka itakaposomwa siku ya mauti, fedha ile unakuta imekwisha. Hivi inakuwaje, tunakubalianaje na jambo hilo, nazidi kumuomba Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa vile alivyo msikivu hili jambo alizungumzie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili naomba niwazungumzie watumishi wanaokopa benki. Mtumishi anakwenda kukopa benki, yeye amekaa ofisini mshahara ukija unakatwa deni linalipwa lakini asilimia yake ya kulipia lile deni (interest rate) inalingana na asilimia ya mtu ambaye anafanya biashara. Kuna risk gani hapo? Kuna rate ya ku-default ni ndogo sana mshahara tu ukiingia tu tayari imelipwa hata hapa Bungeni kwa wale tuliochukua mkopo mshahara ukiingia hujauona umeshalipa deni. Kwa nini sasa hayo mabenki yasione kwamba wale wanaokuja kukopa ambao ni wafanyakazi hao ndio wale wanaolipa pay as you earn kubwa na yenyewe pia inakatwa bila kusumbua, wakashushiwa interest rate kutoka kwenye two digits kwenda kwenye single digit. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana jambo hili lizidi kuangaliwa na linazungumzika. Mimi hainingii akilini tuna mabenki yetu mazuri kama CRDB, tuna mabenki yetu ya hapa nyumbani kama Posta, tuna benki kama NMB lakini mabenki ya nje yaje hapa yafanye rough ya kutafuta hela halafu na sisi tunajirusha tunataka kulingana nayo mnamsaidiaje huyu mwananchi wa chini anayezungumziwa siku zote na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hili jambo likakae kitaalamu zaidi hata kama hiyo hela wanakopeshana wenyewe kwa wenyewe waangalie basi jinsi gani interest rate itashuka na huyu mfanyakazi anayekesha ofisini anakopa kagari kake mnaziita sijui Vitz aone raha ya kufanya kazi ametulia ajue kwamba analipa kwa ustahi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme wazi kwamba tumelizungumza na narudia tena na ninaamini linafikirika na linazungumzika. Lakini niiombe pia hii Wizara ya Fedha iweze kuangalia jinsi gani wale watu wa SACCOS watalipwa asilimia moja zaidi ya interest isilipwe moja kwa sababu wao wanakusanya kule nje wanaleta hela huku benki. Hiyo nayo wangetosha wapewe elimu na hayo mabenki na pia wapewe asilimia moja zaidi na iliwahi kutokea huko nyuma sijui inashindikana wapi ili waweze ku-run ofisi zao vizuri. Matokeo yake tutakuwa tu tunalaumu SACCOS hawafanyi lakini SACCOS pia hawapati elimu ya kutosha, SACCOS hawana motisha, SACCOS hizo ndio maana wanaanza kula wanakuwa mchwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo haya yalifanyika na yakawezekana naamini kwamba bado yatawezekana, tukiweza kuwapa motisha hawa wanaokwenda kutuokotea hela na nitawakumbusha tu. Mwaka jana Serikali ilichukua hela zake ambayo ilikuwa inawaachia mashirika yakae nazo waweke kwenye benki zao za commercial wamepeleka kwenye akaunti BOT lakini mashirika yale Benki zile zinaenda kutafuta hela na sasa hivi kuna benki ambazo zilikuwa na deposit kidogo zime-trip na benki hizo zinaendelea kumbe bado huku nje kuna hela, watu waliamua kuzishikilia lakini wale wakandarasi wanaolipwa pia na BOT zikisharejeshwa hela kwenye akaunti za wale makandarasi kwenye commercial banks wameenda kwenye zile benki ambazo zinaaminika na mnazijua benki zinazoaminika na sisi pia tuna-save huko kama CRDB. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niwaombe sana watu sasa waende wanunue hisa, hisa zipo chini unaambiwa kwenye hisa buy low, sell high huu ndio wakati wote na mimi nawaambia wanunue hisa na wananchi wetu wapewe elimu ya hisa. Lakini nimwombe Mheshimiwa Dkt. Mpango leo tumezikia lugha ngumu sana huku ndani kwamba uchumi umeendaje wape hawa Wabunge wako semina, kuna mataasisi mengi tunatakiwa kuelimishwa tukuone tujue, Wabunge wanataka elimu ili waweze kufikiri sharp kama wewe. Dkt, please PHD yako ni ya ukweli sio Honarally umesoma vitabu mpaka vikasema enough wape watu semina hapa ndani tuongee lugha zinazofanana. Bahati nzuri nao wamekiri ni makanjanja lakini sio mmoja wengi hapa uchumi hatuujui. Tunaomba utupe semina kila Bunge likianza tupe semina tuonge lugha ambazo zinafanana na wewe baada ya kuzungumzia bajeti nakushukuru kwa yote uliyotufanyia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niipongeze sana Kamati ya PIC Kamati hii imefanya kazi kubwa na ya weledi chini ya Mheshimiwa Dkt Raphael Chegeni na niseme kwa mara ya kwanza tumeona dividend zikilipwa hadharani, kuna ambao walikuwa wana hisa lakini walikuwa hawalipwi hivi imekuaje overnight wakajua ni baada ya nyie Kamati kufanya na kwenda kuwaelimisha walipe. Wanapolipa inakuwaje, hela hizo zinaingia kwenye mfuko mkubwa wa Serikali tunapata vifaa ambavyo tunastahili kupata, tunapata dawa, tunapata hela za kununuliwa vitu ambavyo visingenunulika kama hizo hela zisingeokotwa. Kwa hiyo, nawapongeza sana hii Kamati ya PIC na nasema kwa kweli uzi ni huo huo Spika hakukosea, nampongeza sana Spika kwa sababu ni Kamati mpya ilikuwa haipo na naona tukienda tukirudi mambo yatafanyika makubwa zaidi. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)