Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa utendaji uliotukuka kwa kipindi cha miaka minne ya Uongozi wake

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa utendaji uliotukuka kwa kipindi cha miaka minne ya Uongozi wake

MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi hii ya kuja kuhitimisha hoja yangu. Nianze kwa kuwashukuru Wabunge wote waliochangia na kuunga mkono na kwa kweli wamezungumza vizuri sana. Lakini nisisitize tu kwamba kwa kweli tukubali tusikubali, Rais, Dkt. Magufuli, ana utendaji uliotukuka, huo ndiyo ukweli, hiyo haina ubishi. Suala la siasa na mambo ya mlengo wa kushoto na kulia tusiyaweke hapa, mambo yanaonekana wazi kwamba utendaji wa Rais, Dkt. Magufuli, ni wa hali ya juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wamesema Wabunge wamechangia hapa, nami nilisema tunafahamu wote kabla ya Rais, Dkt. Magufuli, kuingia madarakani kulikuwa na kiwango cha rushwa kikubwa sana, ukuenda kwenye mahakama, ukienda zahanati uwe na hela ya kumpa nesi ili akupe huduma. Leo hiyo habari imekwisha, utendaji umekuwa mzuri sana.

Mheshimiwa Spika, huduma kwa wananchi, kwangu pale Bukoba Vijijini kuna mzee mmoja alikuwa ananisimulia alikwenda Ofisi ya DC, akapewa nafasi ya kumuona bila appointment, akasema huyu Mheshimiwa Dkt. Magufuli mtu wa ajabu sana, zamani usingeweza kwenda kwa DC bila appointment ukamuona, hili ni jambo ambalo utawala umekuwa mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini wote tunaona huduma za maji zinaboreshwa, tumeanzisha Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA) ambayo inafanya kazi vizuri, REA inazidi kushika kasi wote tunashuhudia. Alipoingia madarakani Rais, Dkt. Magufuli, alikuta vijiji kama 2,000 vyenye umeme, leo vijiji 7,000 vimepata umeme, jambo kubwa sana. Amesimamia ujenzi wa Stiegler’s Gorge licha ya kwamba nchi ni kubwa tajiri zinapinga sana jambo hili, amekuwa imara sana, hatetereki na tunajenga hili Bwawa la Stiegler’s Gorge na mambo mengine mengi ambayo anayafanya na Wabunge wamesema.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Salome Makamba amesema mambo kadhaa hapa na nimeshangaa. Anasema kukasimu hakuelewi, yeye ni mwanasheria wa viwango vya juu nashangaa anasema haelewi kukasimu. Leo Mheshimiwa Mbowe hayupo hapa amekasimu kwa Mheshimiwa Dkt. Sware, sasa ajabu iko wapi; Mheshimiwa Dkt. Sware amekaa pale, tunamuona Mheshimiwa Selasini hapa anakaimu nafasi ya Mheshimiwa Mbowe, jambo ambalo ni la kawaida. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, anasema haijaenda bajeti asilimia 50 kwenye mikoa na wilaya; leo ni Novemba, miezi minne tu ya bajeti ya mwaka wa fedha, tusubiri, na huduma zinafanyika kule vijijini tunaziona. Kwa hiyo, tuwe na subira, kazi zinakwenda na huduma zinazidi kusonga kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, leo tumesikia kwenye taarifa kwenye azimio humu, amejenga vituo vya afya 352 kwa mwaka mmoja; 352, katika historia ya nchi hii haijawahi kutokea, na amejenga kwa fedha ya chini sana ndogo. Kabla ya yeye Rais, Dkt. Magufuli, ilikuwa kituo kimoja cha afya shilingi bilioni 2.7, leo kituo hichohicho shilingi milioni 400, 500, ndiyo maana vimekuwa vingi kwa sababu ya usimamizi mzuri tunazidi kusonga mbele.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli nahitimisha hoja yangu kwa kusema kwamba Rais, Dkt. Magufuli, anafanya kazi kwa utendaji uliotukuka na tuzidi kumuunga mkono. Ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, naafiki.