Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa utendaji uliotukuka kwa kipindi cha miaka minne ya Uongozi wake

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa utendaji uliotukuka kwa kipindi cha miaka minne ya Uongozi wake

MHE. DKT. MWIGULU L. NCHEMBA: Mheshimiwa Spika, naomba kwanza na mimi nikushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuwa sehemu ya wachangiaji wanaoweka kumbukumbu sawa ndani ya Bunge lako Tukufu, ubora wa kazi na kazi zinazoishi ambazo anazifanya Mheshimiwa Rais kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kazi anazofanya Rais Magufuli hata kama tungejifanya vipofu tukaamua kupofusha akili zetu ili tusiziseme lakini kazi zenyewe anazozifanya zingesema kwetu kwa watoto wetu, kwa wajukuu zetu na vitukuu vya taifa hili, Kwasababu kazi anazozifanya zitaishi muda mrefu kuliko umri wetu na watoto wetu na wajukuu zetu.

Mheshimiwa Spika, tukiangalia katika sura ya kiuchumi kazi moja kubwa inayojumuisha kazi zote zinazofanyika, ni kwamba Mheshimiwa Rais anatuondoa kwenye mnyonyoro wa umaskini ametutoa kwenye mzunguko wa umaskini; anakata ule mrija anakata ule mnyororo ambao kiuchumi tunaita vicious cycle of poverty ambayo ni lazima uwe na uwamuzi dhabiti na ujasiri dhabiti na udhubutu dhabiti ndipo unaweza kufanya kwa sababu cake ile ile ambayo unatakiwa uigawe ili uweze kuondoka kwenye mnyororo huu.

Mheshimiwa Spika, ni kitu gani kinatokea; Mheshimiwa Rais angekuwa na uamuzi wa kuamua kufanya jambo lolote lile ambalo lingehusisha matumizi na fedha hizi hizi ambazo zinajenga vituo vya afya, bwawa la umeme, barabara na zinasomesha watoto zikapita katika mianya ambayo haingeweka alama; lakini yeye ameamua kufanya udhubutu, uamuzi wa busara wa kutengeneza uridhi wa watanzania wa leo na Watanzania wajao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatua ambazo tulikuwa tunaenda nazo kama taifa tungeweza kujipiga kifua, tungeweza kujivuna lakini tungeweza kujivuna kwa fedha za kukopa kwa fedha za kuazima na kwa fedha zenye masimango. Hiki anachokifanya leo anatengeneza miundombinu ya uchumi ambayo itatuondoa kwenye utegemezi na tukaenda kwenye kujitegemea na tukaweza kufanya maendeleo mengine makubwa na tukawa kuweka ustawi wa jamii yetu ya kitanzania inayojitegemea na ambayo ina maendeleo.

Mheshimiwa Spika, kimojawapo ambacho tunaweza tukakisemea; anzia kama Mbunge aliyepita alivyotokea kusema ukitaka kuondoa umaskini kwa kaya moja moja unatakiwa uelimishe watoto wao kwa sababu vingine ambavyo unaweza ukavifanya, hata ungewagawia fedha wazazi wao bado zile fedha wangetumia zisingeweza kutengeneza uridhi kama wa elimu ambao unatengeneza, ambayo mtoto akishapata elimu hata kama mzazi usipomwandikia miradhi elimu yake aliyopata ni miradhi ambayo haina ugomvi na haina ndugu anayeweza kwenda kuilalamikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa wengine wanashindwa ku- connect hivi vitu ambavyo Mheshimiwa Rais anafanya, kila Mbunge akisimama atasemea kwamba angehitaji apate umeme kila kijiji, lakini baadhi yetu hapo hasa upande mwingine utakuta wanasema hakukuwa na ulazima wa kutengeneza bwawa kubwa la umeme litakalotengeneza megawatt nyingi kuliko zile ambazo ziliwahi kutengenezwa katika historia. Umeme siyo nguzo za umeme, unaanzia na chanzo cha kufua umeme ambao utasafirishwa ili wananchi waweze kupata umeme. Hilo ni moja kubwa ambalo linaingia kwenye historia ambalo hata tusingesema watoto wetu wangekuja kusema kwamba kuna bwawa kubwa la umeme ambalo ilikuwa maono ya Mwalimu Nyerere, akaja Rais moja anaitwa Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli akaja akalitimiza ndoto hiyo na watoto wa Tanzania wakapata urithi huu.

Mheshimiwa Spika, hili linabadilisha maisha ya kila mtu mmoja mmoja katika vijiji vyetu tulipo, vijiji ambavyo tulikuwa navyo kabla ya kuwa na maendeleo haya na tulivyokuwa navyo sasa ni vijiji tofauti. Si hilo tu, miundombinu hii mingine ambayo inatengenezwa ambayo italenga kuboresha kuanzia uzalishaji mpaka uchakataji, vyote vinahitaji miundombinu mikubwa hii ambayo inatengenezwa ambayo mwisho wa siku itaunganisha uchumi kuanzia uzalishaji mpaka uchakataji na baadaye kupeleka kwenye soko bidhaa ambazo zitakuwa zimezalishwa zikiwa za kisasa ambazo ni za kukidhi masoko ya kisasa, ambayo si lazima yawe ya ndani hata ya nje, zikaweza kukidhi viwango vinavyotakiwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kitendo cha Bunge lako kuridhia kutengeneza historia hii iingie kwenye hansard ni jambo ambalo na wewe umefanya kitu cha kiungwana ambacho kinastahili tukupongeze kwa sababu hii sasa Kumbukumbu Rasmi za Bunge liliweza kupongeza kazi kubwa anazozifanya Mheshimiwa Rais. Kwa maana hiyo hata wale ambao hawatasema kwa sababu wanatoka katika maeneo yaliyopo humu humu nchini kwetu, kazi anazozifanya Rais zitaendelea kusema na zitaendelea kuwakumbusha wawe na moyo wa kiungwana na moyo wa kizalendo wa kupenda nchi yao ili waweze kusema haya mambo makubwa yanayofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, nikiongea kama Naibu Katibu Mkuu mstaafu, Mheshimiwa Rais ambaye ni Mwenyekiti wa chama chetu amekiheshimisha sana chama chetu. Kuna kipindi wanachama wetu walikuwa wanaogopa kutembea hata na uniform za chama kwa sababu ya mashambulizi waliokuwa wanapata yanayotoka kwa wapinzani wao wa kisiasa, lakini kwa sasa hivi hata wale wasio na CCM angalau wanababaisha kwa kuvaa jezi za Yanga, lakini kimsingi wanataka wavae za CCM na wenyewe wajifananishe na mafanikio makubwa yanayofanyika ambayo Mheshimiwa Rais ameyafanya. Kwa hiyo sisi kama wanachama wa CCM tunajivunia sana kwamba jemedari wetu tuliyemkabidhi Ilani ya Uchaguzi ameitendea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais amezidi sana, maana amezidi maeneo hata yale tuliyokuwa tumeandika kwenye ilani. Tukienda kwenye umeme amevuka, zaidi ya asilimia 10 zimevuka zile tulizozikadiria kwenye ilani, ukienda kwenye maji, ukienda kwenye barabara na mambo mengine ya maendeleo. Viva Magufuli na itakapofika 2020 itakuwa chagua Magufuli kazi iendelee.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Tumwombee Mheshimiwa Rais afya njema aendelee kudunda na sisi tuendelee kutembea kifua mbele. (Makofi)