Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa FAO wa Kuzuia Uvuvi Haramu kupitia Bandari za Nchi Wanachama pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Kuanzishwa kwa Ushirikiano wa Kimataifa wa Nishati ya Jua (The Framework Agreement on the Establishment of International Solar Alliance)

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa FAO wa Kuzuia Uvuvi Haramu kupitia Bandari za Nchi Wanachama pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Kuanzishwa kwa Ushirikiano wa Kimataifa wa Nishati ya Jua (The Framework Agreement on the Establishment of International Solar Alliance)

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa nafasi uliyonipa tena, lakini pia nimshukuru Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge wa Kilimo Mifugo na Maji, lakini na Msemaji wa Kambi ya Upinzani anayesimamia masuala ya Mifugo na Uvuvi wa hotuba zao nzuri sana walizozihutubia hapa Bungeni na vile vile michango ya Waheshimiwa Wabunge wote. Nichukue nafasi hii kuwashukuru sana kwa mchango ambayo mliyoitoa na sisi tumenufaika sana na michango yenu mliyoitoa.

Mheshimiwa Spika, Azimio letu hii la PSMA, bahati nzuri sana Wabunge wote waliopata nafasi wameunga mkono na wametoa ushauri. Kwa ujumla kwa masaa na dakika ulizonipa, ni ngumu sana kupitia maswali ya Waheshimiwa Wabunge, lakini pia na ushauri walioutoa, lakini itoshe kusema kwamba ushauri wote ambao Waheshimiwa Wabunge wametupatia tumeuzingatia na utatusaidia sana katika utekelezaji wa majukumu yetu ya maeneo haya ya uvuvi wa bahari kuu.

Mheshimiwa Spika, la kwanza, labda ambalo Wabunge wameliongelea sana na limezungumzwa miaka mingi suala la Bandari ya Uvuvi, nataka niwaambie Wabunge kwamba hii Serikali ya Awamu ya Tano inaenda kutanzua huu mtego wa miaka mingi ambao umekuwa kilio kikubwa kwa Taifa. Bandari hatua ambayo tumefikia mpaka sasa hivi tuliliambia Bunge lako wakati wa Bajeti kwamba, tunafanya upembuzi yakinifu kwa ajili ya kujenga bandari ya uvuvi hapa nchini. Nataka nilitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa Mshauri Mtaalam Mwelekezi wa kampuni ya Italy amekamilisha report yake ya upembuzi yakinifu.

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa hivi maeneo yaliyopendekezwa kwa ajili ya kuijenga hiyo bandari ni Bagamoyo, Kilwa Masoko na Lindi. Kwa hiyo, kati ya hayo maeneo hayo tutachagua sasa eneo imebaki sasa kwenye maamuzi ya ku-decide kama Serikali kwamba tutajenga bandari ya uvuvi kati ya maeneo haya mawili. Kama hiyo haitoshi Serikali tayari iko kwenye hatua za mwisho kabisa na Serikali ya Jamhuri ya Korea Kusini kwa ajili ya kuanza ujenzi wa bandari ya uvuvi hapa nchini. Kwa hiyo ninachotaka kusema kwa sasa ni kwamba kilichobaki kwa sasa hivi ni maamuzi ya bandari ijengwe wapi na baada ya hapo katika mwezi huu jambo hili litaamuliwa na mwezi unaofuata wa Desemba ni matarajio kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Korea zitasaini makubaliano tayari kwa kuanza bandari ya uvuvi wa bahari kuu.

Mheshimiwa Spika, swali la pili lililoulizwa, ni bandari zinazotambuliwa ni bandari zipi zinazotambuliwa sasa ambazo zitahusika huu Mkataba wa PSMA. Bandari zinazotambuliwa na ambazo zimeingia na ambazo zitahusika na PSMA ni Bandari ya Dar es Salaam kwa sasa, Bandari ya Zanzibar, Bandari ya Mtwara na Bandari ya Tanga, hizi ndizo zitakazohusika katika utekelezaji wa makubaliano yetu na Mkataba wetu huu wa PSMA.

Mheshimiwa Spika, suala lingine lililozungumzwa hapa na Waheshimiwa Wabunge ni suala la udhibiti wa uvuvi haramu kwenye eneo la high seas kwamba hivi sasa hakuna udhibiti na hata hii PSMA tunayoazimia haifiki katika eneo hilo la high seas. Nataka nitoe taarifa kwamba tayari UN wameanza kuandaa legal instruments za usimamizi za resource katika high seas, yaani biodiversity beyond national jurisdiction, tayari inaandaliwa na mara hii instrument itakapokuwa imekamilika, sasa mfumo huu wa PSMA utaenda mpaka high seas. Kwa hiyo, huu ulinzi wa rasilimali wale waliokuwa wanafanya uvuvi haramu kwenye maeneo hayo hawatapata excuse tena.

Mheshimiwa Spika, suala la marekebisho ya Sheria ya Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu ya mwaka 1968 pamoja na kanuni zake za mwaka 2007 ambazo zilifanyiwa marekebisho mwaka 2016, hivi sasa tuko kwenye marekebisho ya Sheria yenyewe pamoja na kanuni zenyewe. Katika marekebisho hayo eneo hili la PSMA ambalo tunalozungumza litaingizwa, lakini pia tutazingatia maombi mbalimbali ambayo yatawezesha ruhusa ya uvuvi yaani authorization to fish kwa meli zenye bendera ya Tanzania kuweza kuvua katika maeneo ya high seas na EEZ za nchi nyingine. Kwa hiyo katika hizi kanuni ambazo kanuni na sheria ambazo tunazifanyia mapitio kwa sasa na zingine zitaingia Januari kwenye Bunge lako Tukufu, tunawaahidi Waheshimiwa Wabunge kwamba maboresho mengi yatakayohusika na Kanuni ya uvuvi wa bahari kuu yatazingatiwa katika haya marekebisho ambayo tunafanya kwa sasa hivi.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambao Waheshimiwa Wabunge wamelizungumza ni suala la eneo la kitutia Mafia kwamba ni muhimu sana kwa mazalia ya samaki, lakini halilindwi ipasavyo, nataka nitoe taarifa kwamba hili eneo linalindwa ipasavyo na liko chini la MPRU, linalindwa uvuvi hauruhusiwi eneo hilo kwa sababu ni eneo ambalo lina mazalia ya samaki, kwa hiyo eneo letu hili tunalilinda na tunatambua umuhimu wake kwamba ni eneo mahususi sana kwa ajili ya mazalia ya samaki.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge hapa walizungumza sana na wakaomba sana kwamba hii kuondolewa kwa tozo ya dola za Kimarekani 0.4 kwa kilo ya samaki inayovuliwa na kusafirishwa nje ya nchi hasa na meli hizi za foreign vehicles kutoka nje ya nchi zinazofanya uvuvi katika ukanda wetu wa uchumi wa uvuvi wa bahari kuu. Waheshimiwa Wabunge walisema na waliomba sana Serikali kwa muda iondoe tozo hii ili kuwezesha uvuvi uweze kufanyika kwa sababu meli zilizokuwa zinakuja kuvua zilishindwa kabisa kuvua baada ya kuweka hii tozo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema kwamba na kama wewenyewe walivyosema ni kweli kabisa sisi Serikali tumeridhia kwa kipindi hiki cha mwaka mmoja wakati tunatafakari njia bora ya kunufaika na rasilimali zetu zilizoko katika ukanda wa bahari kuu ili tuweze kunufaika kwa hiyo, hii tozo tumeiondoa na Waheshimiwa Wabunge tayari tumeshasaini nadhani GN itatoka muda wowote, lakini wavuvi wetu wako ni rurksa sasa hivi kuvua na kwamba 0.4 haitatozwa ila watatozwa zile gharama zingine ikiwemo kulipia leseni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ilikuwa ni suala la kuwekeza kikamilifu katika utafiti; ni kweli kabisa kwamba hakuna mtu anayeweza kukubali ku-risk investment yake katika eneo ambalo halina utafiti. Hakuna Taifa ambalo linaweza kuwa na mipango mizuri kama hakuna taarifa za kiutafiti za kutosha kwenye eneo husika na sisi kama Serikali tunakubaliana na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge na wamekuwa wakitushauri mara kwa mara na kwa sasa tumeanza. Kwa mfano sasa hivi hii Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu (DSFA), tumeshaipatia fedha kupitia Mradi wa SWIOFISH. Jumla ya shilingi milioni 457.7 ambazo hizi tunaanza sasa kufanya utafiti wa kujua rasilimali zetu zilizoko katika eneo la uvuvi wa bahari kuu.

Mheshimiwa Spika, tutafanya hivyo kuhakikisha kwamba zipatikane taarifa zote za uhakika ambazo wananchi wetu wanazitaka, wawekezaji wetu wanazitaka ili sasa tuweze kuhakikisha tunaweka mipango madhubuti yenye taarifa za uhakika za kiutafiti juu yake na sisi tunaamini kwamba tunazo resources katika eneo letu la EEZ ambazo haziko maeneo mengine yote na kwamba pia sisi katika usimamizi wa rasilimali na katika mapambano juu ya uchafuzi wa bahari, pamoja na usimamizi wa uvuvi haramu tunafanya vizuri Waheshimiwa Wabunge, sisi kimataifa eneo letu linatambulika kuwa eneo ambalo bado ni clean, maeneo mengi katika sehemu nyingi duniani watu wameshachafua sana mazingira, lakini maendeleo haya …

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, naongeza nusu saa ili tuweze kumaliza mambo yetu. Haya Mheshimiwa Waziri malizia.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nataka kusema kwamba nchi yetu inazidi kupata sifa kubwa kimataifa katika usimamizi wa rasilimali hizi na tulivunja rekodi kubwa sana tulipokamata ile meli maarufu inaitwa meli ya Magufuli, lakini baadaye majuzi, tukaja kukakamata meli ya Buhanaga One, sisemi ya Mpina, lakini hiyo ni ya Buhanaga One. Ile meli tulipoikamata tumepata sifa kubwa sana duniani katika kuhakikisha kutuma message kubwa sana ya ulinzi wa rasilimali hizi za Taifa.

Mheshimiwa Spika, nataka niwaambie Waheshimiwa tuko vizuri sana tunapongezwa kila kona kwa jinsi ambavyo tumesimama kidedea katika kuhakikisha kwamba hizi rasilimali zinalindwa sana. Hivi majuzi kuna baadhi ya viongozi tuliwaambia wanaotaka kutumia rasilimali hizi za Taifa kujipa sifa za ziada katika kuchaguliwa, kiongozi anashindwa kutaja sifa zake za kuchaguliwa anaanza kuwaambia wananchi wakafanye uvuvi haramu au anaanza kusitisha zoezi la doria linalolinda rasilimali kwamba kwa sababu hiki ni kipindi cha uchaguzi. Tunazidi kusisitiza Watanzania wasimamie sheria rasilimali hizi za uvuvi zitalindwa muda wote, bila kuzingatia majira ya mvua au ya jua, uchaguzi hauwezi kuwa na mahusiano na ulinzi wa rasilimali hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka kusema kwamba viongozi wote wanaohusika wahakikishe kwamba na leo tunaunga mkono hili Azimio hii kubwa la dunia ambalo litaleta mchango mkubwa katika kusimamia kwa dhati hizi rasilimali tulizonazo ili tuendelee kuzivua kwa uendelevu kwa leo na siku zijazo.

Mheshimiwa Spika, sitaki niende nje sana ya muda huu ulionipa, lakini nizungumzie suala la by-catch, suala hili tunaangalia changamoto zake katika haya marekebisho ya kanuni ambayo tunayazungumza ili kuweka utulivu na kuondoa malalamiko yaliyoko hivi sasa ya by-catch.

Mheshimiwa Spika, mwisho suala la ku-extend ile continental shelf ambayo imezungumzwa hapa, nimshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje ametoa ufafanuzi mzuri, lakini na Mheshimiwa aliyezungumzia hoja hii naye alizungumza vizuri. Sisi kama Serikali tunaendelea kufuatilia kwa karibu kuhakikisha kwamba tunafikia haya malengo yetu.

Mheshimiwa Spika, nalishukuru sana tena Bunge lako katika kuunga mkono hii hoja iliyoko mbele yetu kwa sasa baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja. (Makofi)