Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia mpango wa mwaka 2020/2021. Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia kuwepo hapa tukiwa na afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mpango huu wa Miaka Mitano, nianze tu kwa kupongeza katika suala zima la elimu kwa sababu tangu Rais wetu alipoingia madarakani alifanya elimu bure na wanafunzi wanaomaliza kidato cha nne mwaka huu ndiyo wanafunzi ambao kwa kweli katika hiyo miaka minne wamenufaika na elimu bure. Kwa hiyo, napongeza sana jitihada hizi za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango ni mzuri na tunaona ndani ya miaka minne pia iliyopita utekelezaji umekuwa ni mzuri kwa sababu ipo miradi ambayo kwa kweli wanasema mwenye macho haambiwi tazama. Tunapongeza kwa jitihada hizi ambazo ni Mapinduzi makubwa kwa Serikali ya Awamu ya Tano iliyofanya katika kuwaletea Watanzania maendeleo. Imani yangu kubwa ni kwamba miradi hiyo itakapokamilika Tanzania tutaelekea kabisa katika ule uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025 kupitia viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mpango huu wa 2020/2021 ningependa nizungumzie katika suala zima la Uwekezaji, tunafahamu Uwekezaji ni jambo zuri sana na kwa kweli nipongeze Wizara husika Mheshimiwa Angellah Kairuki pamoja na Ofisi ya Waziri ya Mkuu nawapongeza sana kwa sababu tunaona kwa kweli baadhi ya vikwazo ambavyo tayari kwa sasa vimeondolewa na tumerahisha huduma ambazo sasa zinapatikana katika eneo moja badala ya ule usumbufu uliokuwepo hapo awali. Tunapoelekea kwenye uchumi wa kati ni dhahiri kabisa vikwazo hivyo vingeweza kupunguza kasi ya Wawekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia wawekezaji katika upande wa Maliasili, tunawahitaji sana, lakini ningependa kuishauri Serikali kwamba katika Mpango huu na hata tunaelewa kabisa kwamba tangu tumeweka concession fees kwa kweli pato limeongezeka kwa kiasi kikubwa sana makusanyo yamekuwa ni makubwa, kwa mfano tu TANAPA kwa Hifadhi ya Serengeti kwa kipindi cha tangu Julai mosi mpaka mwezi wa 10 walikusanya zaidi ya bilioni 49 na yote hii imewezekana kutokana na concession fees ambayo tuliipitisha hapa Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza sana na niwapongeze sana Wizara ya Maliasili na Utaliii kwa kazi hiyo nzuri, lakini ningependa kushauri kwamba katika uwekezaji huu sasa tuangalie ni kwa jinsi gani tunapunguza hoteli nyingi ambazo zipo ndani ya Hifadhi zetu. Kwa sababu tunaelewa kabisa utajiri huu tulionao hata wenzetu wa jirani wanatamani wangekuwa nao na tunapoweka hoteli nyingi katika maeneo hayo wanyama nao pia wanakimbia kwa sababu ya kuona mazingira ambayo ni tofauti na yale waliyoyazoea. Kwa hiyo ningeishauri Wizara ya Maliasili na Utalii, tunapokwenda huko labda sasa, tuone kwamba ndiyo tunahitaji, lakini waweke mazingira mazuri kwamba kupunguza hoteli ndani ya Hifadhi angalau zikajengwa pembezoni mwa Hifadhi ili basi wanyama wale waendelee kuwepo na hatimaye waendelee kuongeza pato la Serikali kama ilivyo pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza pia sana Serikali hii ya Awamu ya Tano kwa sababu katika suala zima la mikopo tumeona kwamba mikopo ya elimu kwa vyuo vikuu imeongezwa na ukiniuliza kipaumbele changu ni kipi hasa katika Bunge hili, basi sifichi nitasema kwamba ni watu wenye ulemavu, watu wenye ulemavu. Kwa sababu gani nasema hivyo? Watu wenye ulemavu kwa kweli katika Awamu hii ya Tano Serikali imekuwa na jicho la ziada katika kuhakikisha kwamba wanatimiziwa mahitaji yao. Pia katika suala zima la Uongozi Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kweli ni Rais wa mfano na tunampongeza sana kwa hilo na nawapongeza pia hata Mawaziri ambao kwa kweli wamekuwa na ushirikiano mkubwa sana katika suala zima la watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili sasa basi tuweze kupata viongozi wengi ambao wanatokana na kundi hili la watu wenye ulemavu, napendekeza katika Mpango huu kuona ni kwa jinsi gani kwamba tunaongeza bajeti hii ya mikopo ili wanafunzi wenye ulemavu waweze kupata ruzuku badala ya mikopo, kwa sababu Waswahili wanasema ukimwona nyani mzee, ujue amekwepa mishale mingi. Mtu mwenye ulemavu mpaka anafika Chuo Kikuu kuna changamoto nyingi sana amezipitia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu katika nchi zilizoendelea wanatoa ruzuku badala ya mikopo kwa sababu hata anapomaliza Chuo Kikuu kupata ajira inakuwa ni ngumu sana, kwa hiyo kurudisha ile mikopo bado inakuwa ni ngumu na ni mzigo mkubwa kwake.

Kwa hiyo ningeomba kwamba hawa watu wenye ulemavu tuangalie Serikali ni kwa jinsi gani tunawapa ruzuku badala ya kutoa mikopo kwa kweli ambayo hapo baadaye kwao inakuwa shida sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiamini Serikali yangu kwa umakini ilionao na ombi langu hili basi katika Mpango huu tunapoelekea tuone kwamba bajeti hiyo inazingatia mahitaji ya watu wenye ulemavu na hata wale watoto ambao wamezaliwa na familia za watu wenye ulemavu kipato chao kinakuwa ni duni. Naiomba Serikali tuone kwamba ni kwa jinsi gani tunawa-accommodate hawa watu wenye ulemavu na familia zao ili basi angalau ruzuku hiyo itasaidia, lakini kuona ni kwa jinsi gani sasa tunaboresha shule, naipongeza kwa kweli Serikali kwa sababu tayari imekwishaanza na matunda tunayaona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, bado mimi kama Mwakilishi wao ninawasilisha ombi la kuona kwamba ni kwa jinsi gani tunaboresha shule zetu ambazo zita wa- accommodate na watoto wenye ulemavu. Kwanza kwa kuangalia katika ajira ambazo tayari wamekwishaanza kufanya, lakini tuongeze pia Walimu ambao wana ujuzi na utaalam wa kufundisha watu wenye mahitaji maalum ambao ni wanafunzi wenye ulemavu. Shule nyingi za vijijini bado miundombinu yake siyo rafiki kabisa, kabisa, kwa hiyo naiomba Wizara iangalie ni kwa jinsi gani miundombinu hii inawawezesha watoto wenye ulemavu hasa vyoo, imekuwa ni shida, wakati mwingine unakwenda vijijini ukienda kwenye hizo shule kwa kweli inahitaji moyo ambao kwa kweli ni mgumu kwa sababu watoto wale wanalazimika kwenda kwenye vyoo ambavyo wanatambaa, wakati mwingine akitoka kwa kweli anatia huruma na ni rahisi sana kupata magonjwa, kwa hiyo tuone ni kwa jinsi gani tutaboresha hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala zima la ajira kwenye Ofisi ya Waziri ya Mkuu, nimeona kwa kweli jitihada kubwa na natambua na nampongeza sana Mheshimiwa Jenista yeye ni mwanamke shujaa, jasiri kwa jicho lake la ziada ambalo amekuwa karibu sana na watu wenye ulemavu. Sasa naomba basi katika Mpango huu tuone ni kwa jinsi gani zile Taasisi au Wizara ambazo bado hazijatimiza asilimia tatu, asilimia tatu kwa ajili ya watu wenye ulemavu tuzingatie.

Ningeomba hata Bunge letu pia kwa kweli limekuwa la mfano na Mheshimiwa Spika popote alipo nampongeza sana kwa kazi kubwa kwa sababu miundombinu amekuwa ni mfano na wengi waje kuiga hapa, lakini sasa naomba pia katika suala la asilimia tatu, matarajio yangu ni kuona napishana na watu wenye ulemavu katika Taasisi yake ambayo kwa kweli watakuwa ni mfano bora na watatoa elimu ambayo itasaidia wengine pia ambao bado kwa namna moja au nyingine wako nyuma sana katika ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika suala la uwekezaji, wawekezaji wanaokuja tumeona kwamba wanaajiri watu wengi na ajira zipo nyingi, lakini na wao pia asilimia tatu nayo izingatiwe pia ili watu wenye ulemavu wale ambao wamepata elimu, wamesoma waweze hizo ajira na hatimaye kuweza kujikomboa wao wenyewe na kusaidia familia zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumza kwa sababu mimi ni mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria na nimeshuhudia mengi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, kazi wanayofanya hasa kwa kuzingatia kwamba kitalu nyumba kinawasaidia sana, vijana wengi wamewezeshwa. Nawaomba sasa katika Mpango huu tuone ni kwa jinsi gani tunafika maeneo mengi zaidi katika nchi hii ili vijana tuweze kuwawezesha katika kilimo hasa kupitia Mfuko wa Uwezeshaji wa Vijana, vijana wengi waweze kupata mikopo ambayo itawawezesha kujiajiri badala ya kutegemea ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayaona mengi kupitia Kamati hii, vijana ambao wamewezeshwa na sasa hivi wengine mitaji yao imefika zaidi ya bilioni. Kwa hiyo kwa kweli tukiwawezesha vijana wengi na maeneo mengi tukawafikia na pia tukawatumia hata baadhi ya Wabunge huku katika Majimbo yao, naamini kabisa vijana wengi sasa hawatokuwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mollel kwa mchango wako na ushauri wako.

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)