Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na niweze kuchangia Mpango wa Taifa wa mwaka 2020/2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa lile agizo lake la kwamba Halmashauri ziweze kuhamia kwenye maeneo yao ya utawala. Mimi kidogo kwenye Jimbo langu tumepata changamoto, baada ya kuwa tumehamia Nzela kwa kweli jiografia imekuwa ngumu sana. Wananchi wa Busanda walikuwa wanafuata huduma kwenye ofisi za zamani yaani ni karibu kilomita 40/50 hivi lakini sasa hivi inabidi waende zaidi ya kilomita 100 kwa ajili ya kufuata huduma. Naomba Serikali pengine itupatie Halmashauri nyingine ili wananchi waweze kupata huduma vizuri na kuweza kufanya kazi zao kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nilipo nimekuwa nikipata simu nyingi kutoka kwa Watendaji wa Serikali, Walimu Wakuu wa Shule lakini vilevile Watendaji wa Vijiji na Kata wanapata shida sana. Jambo ambalo siku za nyuma angetumia siku moja sasa hivi inabidi atumie siku mbili aende Nzela kwenda kusainisha cheki arudi, alale mjini ili kesho yake aweze kupata huduma, ni shida sana. Kwa hiyo, naomba sana Serikali iangalie suala hili. Hata ikiwezekana kwa kuwa mwanzo ofisi zilikuwa Mji wa Geita basi turudishwe hata kama ni Mji kama hatutapatiwa Halmashauri sasa hivi ili angalau wananchi waweze kupata huduma kwa ukaribu zaidi kama ambavyo Serikali inakusudia kusogeza huduma kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la wakulima wa pamba. Kumekuwa na changamoto kubwa sana kwamba wananchi wameuza pamba yao lakini mpaka sasa kuna baadhi ya wananchi hawajaweza kulipwa haki zao, ni kilio kikubwa sana. Kwa hiyo, pia hilo naomba Serikali iweze kulifanyia kazi wananchi waweze kulipwa fedha zao kwa sababu wameuza pamba kwa mkopo sasa umeingia msimu mpya wanatakiwa angalau wanunue tena mbegu lakini wanashindwa kwa sababu hawajaweza kupewa fedha zao kutokana na mauzo ya pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo sasa nilikuwa naomba kwenye Mpango huu wa Serikali katika suala la kilimo hasa mazao ya biashara Serikali iangalie uwezekano wa kuwekeza zaidi fedha nyingi kwenye viwanda vya kuongeza thamani ya mazao. Kwa mfano, katika zao la pamba, Serikali iweke fedha nyingi kuhakikisha kwamba viwanda vya kuchakata pamba vinakuwepo ili hatimaye masoko ya pamba yawepo kwa sababu haiwezekani wananchi wanalima pamba ya kutosha lakini masoko hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa na viwanda vingi vya kuchakata mazao, nina uhakika kwamba wananchi wataweza kupata fedha zao kwa wakati na hatimaye watu wengi watahamasika zaidi kuongeza ulimaji wa pamba kwa wingi. Kwa hiyo, katika bajeti ijayo kwenye kilimo, Serikali iwekeze zaidi kwenye viwanda vya kuchakata mazao ya biashara ili hatimaye kuweza kuongeza thamani ya mazao hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kweli inafanya kazi kubwa sana kwa sababu Mpango huu wa Miaka Mitano naufuatilia mwaka hadi mwaka na kweli mipango yake na utekelezaji vinaonekana. Kwa mfano, katika sekta ya afya tumeona jinsia Serikali ambavyo imeweza kutekeleza mambo makubwa sana yanayoonekana katika taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya afya, Serikali imetujengea zahanati na vituo vya afya pamoja na Hospitali za Wilaya lakini vilevile tuna upungufu mkubwa sana wa watumishi katika sekta hii. Nitumie nafasi hii sasa kuomba katika bajeti tuangalie umuhimu wa kuweza kuweka bajeti kubwa kwa ajili ya kuajiri watumishi katika sekta ya afya kwa sababu upo upungufu mkubwa sana pamoja na kwamba tunajenga vituo lakini kama hakuna mtaalam wa kutoa huduma bado tutakuwa hatujatenda haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la umeme wa REA. Naipongeza sana Serikali kuona umuhimu wa kuwa na umeme vijijini. Wananchi wanaoishi vijijini wamehamasika sana kuhusiana na suala la umeme. Niombe Serikali iendelee kuwekeza fedha nyingi hasa kwenye upande wa kupeleka umeme vijini kwa sababu vijijini ndipo ambako wanaishi wananchi wengi, asilimia kubwa ya Watanzania wapo vijijini. Tukiwekeza kwenye suala la umeme wa REA vijijini kwa wingi kabisa, vijiji vikapata umeme, mimi najua kwamba tutaweza kufikia ile azma ya Serikali ya Tanzania ya viwanda lakini pia tutaweza kufikia ule uchumi wa kati mpaka mwaka 2020 - 2025. Kwa hiyo, niombe sekta ya umeme ipewe kipaumbele kikubwa zaidi ili wananchi waishio vijijini waweze kupata umeme huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu kila napokwenda Jimboni wananachi wanaulizia kuhusu umeme, kila mtu anataka umeme, kila kijiji kinahitaji kupewa umeme. Sina uhakika sehemu zingine lakini ni karibu kila sehemu katika nchi ya Tanzania sisi ambao tunatoka Majimbo ya vijijini tunahitaji umeme. Tunaomba sana wanapopanga bajeti tuhakikishe suala la umeme lipewe kipaumbele cha kutosha ili wananchi walio wengi waishio vijijini wapatiwe umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la msingi kabisa ni suala la barabara za vijijini. Mimi nazungumzia vijijini kwa sababu Jimbo langu ni vijijini. Bajeti ya TARURA haitoshi, tuongeze bajeti zaidi kwenye TARURA kwa sababu tukiwa na barabara nzuri vijijini tutawawezesha wananchi wetu kuweza kufanya shughuli zao na kuuza mazao yao vizuri na kwa wakati. Kwa hiyo, niombe tuongeze bajeti zaidi TARURA ambako ni barabara za mjini na vijijini lakini zaidi kwenye vijiji ambako ndipo kuna changamoto kubwa sana ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye suala la UKIMWI, tunafahamu kabisa kuna takwimu zinaonesha kwamba vijana kati ya miaka 15 mpaka 24 wanapata maambukizi makubwa sana ya UKIMWI lakini zaidi ya hapo asilimia 60 ya hao vijana ni watoto wa kike, jambo hili kwa kweli ni la kusikitisha. Kwa hiyo, naomba kwenye Mpango wa Taifa na bajeti tuone umuhimu wa kuwekeza mpango zaidi kuweza kunusuru suala hili hasa kupunguza maambukizi ya UKIMWI kwa vijana wetu ambao ndiyo Taifa tunalitegemea kesho na nguvu kazi ya Taifa. Kwa hiyo, niombe Serikali iangalie umuhimu, ikiwezekana tuendelee kuhamasisha zaidi masuala haya ya UKIMWI ili wananchi waendelee kujiepusha na na masuala haya ya UKIMWI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu UKIMWI huu tunapoteza Taifa hasa vijana wetu, kwa hiyo, tuwekeze bajeti zaidi kuendelea na kampeni kuhusiana na suala hili la UKIMWI. Nasema hivyo kwa sababu miaka ya nyuma mara kwa mara kulikuwa na uhamasishaji sana kuhusu kuepuka suala la UKIMWI lakini leo hii tumepunguza kidogo hiyo kasi na ndiyo maana pengine maambukizi yameanza upya, yameongezeka zaidi kwa kipindi hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, naipongeza Serikali hasa Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa makusanyo ya fedha hasahasa kwa kielektroniki. Naomba tuendelee kuwa na msisitizo zaidi kwamba kila mtu ukinunua kitu uchukue risiti kwa sababu kuna wafanyabiashara wengine hawatoi risiti kwa hiyari hivyo tuendelee kuweka msukumo. Sasa hivi tumepunguza kidogo msukumo lakini tuendelee kama ambavyo Rais ameendelea kusisitiza, tuendelee zaidi kuhamasisha, kusisitiza kwa sababu wananchi wakilipa na kupata risiti, mapato haya yanaenda moja kwa moja kwenye Pato la Taifa yanaingia TRA kwa ajili ya mapato ya Taifa letu. Kwa hiyo, naomba sana Serikali kupitia Wizara hii iangalie namna ya kuendelea kusisitiza suala la kudai risiti na kulitolea msukumo mkubwa ili tuendelee kupata mapato zaidi katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, napenda kuendelea kusema kwamba Serikali aingalie…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Lolesia Bukwimba kwa mchango wako mzuri.

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)