Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie katika Mpango huu wa Maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, niishauri Serikali tupange kuwawezesha wavuvi kwa kuwapa mikopo, zana za kisasa ili basi waweze kwenda kuvuna katika bahari yenye kina kirefu. Hii ni moja ya sekta ambayo imesahauika kabisa, tofauti na sekta nyingine wavuvi ni kama bado hawajapata ule upendeleo wa makusudi wa kutenda kazi zao. Tukifanya hivi tutaongeza kipato cha watu wale lakini tutainua uchumi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine tupange sasa kusitisha uhamishaji wa mifugo. Kulikuwa na maamuzi sasa ya kuhamisha mifugo kutoka maeneo ya Ihefu (Mbeya) kuipeleka Mikoa ya Kusini hasa Mkoa wa Lindi. Mifugo ile sasa imekuwa mingi sana, nafikiri tupange kusitisha zoezi hilo na sasa tujikite na kuboresha miundombinu ya mifugo iliyopo pale. Tumepeleka ile mifugo hakuna mabwawa, malambo na utaratibu wa wapi inakaa na wapi isikae sasa kumekuwa na vurugu. Mimi nafikiri kwa tija bora ya mifugo ile tupange kuboresha miundombinu ili basi ile mifugo iwe productive, hilo litawasaidia sana wale wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kwenye kilimo tuongeze sasa uzalishaji wa mbegu za mafuta. Ni dhahiri shahiri kwamba ukiacha uagizaji wa petroli basi kitu kingine kinachoagizwa kwa pesa nyingi za kigeni ni mafuta ya kula. Bado tunayo fursa ya kuzalisha mbegu hizi za mafuta ili basi tuweze kupata mafuta mengi ya kula ambayo yatapunguza kutumia pesa nyingi za kigeni kuagiza mafuta hayo kutoka nje. Hilo litakuwa ni jambo jema sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tupange pia kuwa na viwanda vya mafuta. Kwa mfano, sisi kule kwetu tunazalisha ufuta mwingi lakini hatuna kiwanda cha ku- process mafuta ya ufuta, ni kama tunazalisha kwa ajili ya kusafirisha ufuta ghafi kitu ambacho kwenye uchumi nafikiri hakiko sawasawa. Tukipanga sasa mpango wa kuwa na viwanda vya ku-process ufuta, vitasaidia kupata hayo mafuta, kutengeneza ajira na kuinua uchumi wa watu wale. Lindi leo tumetajwa kama Mkoa wa mwisho, tunazalisha ufuta mwingi tukiwa na viwanda vikubwa vya ku-process mafuta ya ufuta tutawezesha kupandisha uchumi wa watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nafikiri sasa tupange kuwa na mtawanyo unaofanana wa uwekezaji wa viwanda. Tunajenga viwanda ni jambo jema na tunaenda kwenye uchumi wa viwanda lakini hivyo viwanda tumeona kama vinajikita sehemu moja. Serikali iangalie uwezekano sasa wa kutawanya, tuangalie kule zinakopatikana malighafi basi na viwanda vijengwe huko. Vitasaidia kutengeneza ajira lakini vitasaidia kujenga ustawi wa miji na kupandisha uchumi wa watu katika maeneo husika. Hilo litakuwa ni jambo jema sana kwa ustawi wa uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka kusema ni kuhusu suala zima la uwekezaji. Tupunguze urasimu katika uwekezaji kwani bado kuna urasimu mkubwa katika uwekezaji. Sisi pale kwetu alikuja mwekezaji kutoka Marekani akitaka kuwekeza katika Bonde la Mto Matandu kwa ajili ya kilimo cha mpunga, ni uwekezaji wa zaidi ya dola milioni 50, uwekezaji mkubwa sana. Sisi Halmashauri tukashawishi Serikali za Vijiji tukatoa ile ardhi lakini kilichotokea basi alitokea tu dalali mmoja akaanzisha longolongo mwishoni yule mwekezaji akaondoka, nafikiri aliamua kuondoka kwa sababu ya urasimu. Serikali ijaribu kufuatilia tupunguze urasimu kwani uwekezaji kama ule ungefanyika ungewasaidia sana wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ule uwekezaji wa miradi mikubwa kwa mfano LNG lakini kiwanda cha mbolea ni jambo jema kama Serikali ingehuisha utekelezaji wake. Limekuwa likizungumzwa lakini utekelezaji wake mpaka sasa naona ni kama umekwenda kwa kusuasua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusiana na uamuzi wa kupunguza kwanza ushuru wa Halmashauri katika yale mazao yanayolimwa na wakulima katika Halmashauri kutoka asilimia 5 mpaka 3 lakini ule uamuzi wa kutotoa ushuru wa korosho umezi-paralyze Halmashauri zetu, Halmashauri zetu hali ni mbaya sana. Hii inachangia pengine hata kufanya wananchi katika Halmashauri uchumi wao kuwa chini na kutajwa kama maskini. Lindi na Mtwara tunazalisha korosho, mwaka jana ushuru ule haukwenda kabisa. Zipo Halmashauri zaidi ya asilimia 90 ya mapato yake zinategemea ushuru wa korosho. Kwa hiyo hilo nalo Serikali iliangalie vinginevyo hawa watu ukisema ni maskini tu inakuwa kama hukuwatendea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la maji. Tumekuja na mawazo mazuri kabisa ya kuanzisha Mamlaka ya Maji Mijini na Vijijini, ni jambo jema lakini sasa Serikali ipange kupeleka pesa za kutosha. Katika jambo ambalo bado linaguswaguswa ni suala la maji. Tuna Wakala huyu kwa mfano DDCA wa kuchimba visima bado kabisa kazi haijafanyika. Tuwaongezee pesa waweze kuchimba visima vingi na kufufua ile miradi ya siku nyingi ambayo imekufa ili basi wananchi wetu waweze kupata maji safi na salama na hivyo kuinua uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa ni suala la uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Suala hili la hiki kinachoendelea ni jambo geni kwenye mchakato wetu wa demokrasia na uchaguzi. Ni jambo ambalo limeleta sintofahamu, tumestushwa na tumepigwa na bumbuwazi, kwa nini hili limetokea?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niseme tu hili ni jambo geni na Waswahili wa Pwani wanasema: “Mgeni kumpokea pengine kujichongea”. Sasa hili limekuja tulikemee siyo jambo zuri baadaye litakuja litatusumbua sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi bado wanaendelea kuhangaika kufuata zile taratibu za kupata hizo haki. Tumejiandikisha majina baadaye ukaja uchaguzi wa kuteuliwa, hatukuteuliwa, tukaweka yale mapingamizi bado hatukupata hiyo haki, sasa hivi hatua inayofuata ni kwenda kukata rufaa na rufaa inatakiwa ukakate Makao Makuu ya Wilaya. Sasa kwa jiografia ya Majimbo yetu kutoka vijijini kwenda Wilayani ni mbali sana kiasi kwamba zile siku mbili hazitoshi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali ina nia njema ya kuona hii haki inapatikana, niishauri Serikali iongeze siku kwa ajili ya kukata rufaa. Wananchi bado wanaona kwamba wanataka kutafuta hii haki, kama ambavyo mmeongeza siku za kujiandikisha basi ongezeni siku za watu kwenda kukata rufaa ili kuona wanapata haki zao ili tuweze kwenda kwenye kuchagua viongozi ambao wananchi wanawataka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, ahsante. (Makofi)