Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi nami niweze kutoa maoni yangu. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya na kuniwezesha katika kuchangia mapendekezo ya Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kutokukubaliana/kukataa maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani yaliyoko ukurasa wa sita kwamba Serikali imezifilisi Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa kuzinyang’anya vyanzo vya mapato na kuzifanya ombaomba kwa Serikali kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikubaliani kwa sababu mapato ya Halmashauri zaidi ya asilimia 95 yalikuwa yanatumika katika matumizi ya kawaida. Nikiri kwamba pamoja na Serikali kuchukua vyanzo hivyo, Serikali hii imerithi madeni mengi ambayo ni malimbikizo ya mshahara na matumizi mbalimbali ya watumishi kutoka katika Halmashauri hizi. Serikali imerithi madeni ya wazabuni wa Halmashauri ambapo Halmashauri zilikuwa zinakusanya na kutumia fedha kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali kwa kuchukua baadhi ya vyanzo hivi, kwa sababu mambo mengi mazuri yameweza kufanyika. Mwanzo asilimia hizo nyingi zilikuwa zinatumika kwa wachache, lakini sasa hivi fedha hizi zinatumika kwa wananchi wengi ambao pia ni sehemu ya Halmashauri. Watumishi ni sehemu ya Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri kwamba mishahara ilikuwa inalipwa mpaka tarehe 5 ya mwezi unaofuata lakini sasa hivi mishahara inalipwa mapema sana, siyo zaidi ya tarehe 25. Vilevile zaidi ya shilingi bilioni 20 zinapelekwa kwa ajili ya elimu bure, hakuna watoto wanaorudishwa majumbani. Pia mikopo ya elimu inatolewa kwa wakati, inatolewa miezi miwili kabla na ongezeko la wanafunzi wanaolipwa limeongezeka kutoka 100,000 mpaka 128,000. Hatuoni migomo kwa wanafunzi wa vyuoni. Wametulia, wanasoma bila maandamano yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri madeni ya watumishi na ya wazabuni yamelipwa kwa kiasi kikubwa. Fedha za miradi ya maendeleo zimepelekwa kuimarisha miundombinu kwa wananchi wetu. Kwa mara ya kwanza nimeona Mkoa wa Simiyu Vituo vya Afya vinatoa huduma ya upasuaji, mpaka Zahanati na Vituo vya Afya dawa zimejaa. Hayo yote ni sehemu ya Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa mapendekezo katika Mpango, kwamba Serikali iweke mpango mahsusi sasa wa kuhakikisha madeni ya watumishi yaliyohakikiwa yote yanalipwa; na maboma ya maabara na majengo mengine yakamilishwe ili kuwepo kwa thamani ya fedha ili maabara hizo pia zitumike kwa kadri ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri pia maboma ya madarasa ya sekondari, Serikali inakamilisha, lakini sasa Serikali iweke mpango mahsusi wa kuajiri wahandisi wa kutosha wa ujenzi. Kwa sababu wahandisi wengi wameenda TARURA na wahandisi wa majengo katika Halmashauri hawapo. Fedha nyingi za miradi ambazo zimekuwa zikipelekwa zinatumika na mafundi ambao ni local ambapo inasababisha miradi mingine haitekelezwi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nichangie upande wa miradi ya maji. Nakiri kwamba Serikali inapeleka sana fedha nyingi kwa ajili ya miradi ya maji kiasi kwamba mimi nashindwa sasa kusema fedha ziongezwe au zisiongezwe kwa sababu fedha kwanza zinazopelekwa hazijaleta tija. Miradi mingi imekamilika lakini haitoi maji. Fedha nyingi zinapelekwa, miradi haitoi maji, mingine inatoa maji siku tu ya uzinduzi. Kwa hiyo, Serikali pamoja na kuwa tumezipa mamlaka za maji vijijini tuhakikishe upungufu uliokuwepo sasa unafanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto zilizokuwepo ni usanifu mbovu, usimamizi mbovu na utafiti mbovu. Haiwezekani Wilaya ya Muleba yenye vyanzo vya uhakika vya maji, lakini miradi yake inakamilika halafu haitoi maji. Kwa hiyo, hapo nakiri kulikuwa na usanifu mbovu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa pia na upungufu wa wahandisi wa maji. Serikali iweke Mpango madhubuti wa kuhakikisha inaajiri wahandisi wa maji wa kutosha. Vile vile utafiti pia ulikuwa mbovu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya nchi hii yanatofautiana. Kuna maeneo ambayo water table iko juu, mengine water table iko chini. Kwa mfano, Mkoa wa Simiyu kuna maeneo ambayo water table iko chini sana, lakini inapelekewa miradi ya visima virefu. Kuna maeneo mengine hata ukichimba maji hata Lukale maji yale hata kwenye maabara ya maji hayakubaliki kwa sababu ni chumvi. Naiomba Serikali iweke mpango kwa kufanya utafiti mzuri na kupeleka miradi kulingana na maeneo. Kwa mfano, Wilaya ya Meatu kuwepo mpango wa kupeleka mabwawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dhati ya moyo wangu, naiomba Serikali iweze kuusaidia Mji wa Mwanuzi ambao ni Makao Makuu ya Wilaya ya Meatu. Kuna tatizo kubwa la upatikanaji wa maji. Bwawa lile limejaa matope kiasi kwamba hata maji yale hayawezi kutibiwa, hayawezi kupampiwa katika matenki, ni matope matupu. Namwomba Mheshimiwa Waziri wa Maji afike Wilaya ya Meatu akashauriane na wahandisi na wataalam waone namna gani wanavyoweza kuunusuru Mji wa Mwanuzi, kwa sababu hatuna chanzo kingine cha maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipewa mradi wa visima nane, lakini vimefeli kwa sababu water table iko chini sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo, naunga mkono hoja na ninakushukuru sana. Ahsante. (Makofi)