Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie mapendekezo ya Mpango wa Serikali ambao umewasilishwa na Mheshimiwa Waziri. Na mimi niungane kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango, Naibu Waziri na wafanyakazi wote wa Wizara ya Fedha kwa jinsi ambavyo mmeuandaa Mpango huu, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba tunapokuwa na Mpango ni lazima tuwe fedha za kuutekeleza Mpango. Kwa hiyo, nianze tu kupendekeza katika mipango ya Serikali kuhakikisha vyanzo vya mapato vinaimarishwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya chanzo cha mapato ambacho hatufanyi vizuri sana ni cha kodi ya majengo (property tax). Kwa kweli eneo hili tukiliimarisha, Serikali inao uwezo mkubwa sana wa kupata fedha. Naomba Wizara ihakikishe katika Mpango ujao na bajeti iliyokuja basi eneo hili la ukusanyaji wa kodi za majengo uweze kuimarishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ni muhimu sana ni suala zima la nyumba za Serikali ambazo zilikuwa za Wizara na taasisi zilizopo Dar es Salaam hivi sasa hazitumiki. Naomba Serikali katika mpango na bajeti ijayo itoe mipango ya kuhakikisha majengo yale sasa yanageuka kuwa ni vitega uchumi vya kuisadia Serikali kupata fedha. Majengo yale ni mengi na baadhi ya maeneo tunalo tatizo kubwa sana la hosteli za wanafunzi kwa Dar es Salaam, kwa hiyo, Serikali iangalie uwezekano wa baadhi ya majengo aidha kuyakarabati na kuwa hosteli kwa sababu wanafunzi wale watachangia na kuiingizia Serikali mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakupongeza sasa Mheshimiwa Job Ndugai umekuwa ni mfano wa kuigwa katika Maspika na Bunge hili mzee unalimudu, unaliendesha vizuri na kwa kiwango. Moja ya ishara hiyo ni jinsi ambavyo umeamua sasa kutuweka kwenye Bunge Mtandao, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa jitihada hizi ukisaidiwa na Mheshimiwa Naibu Spika na Katibu wa Bunge, juzi tulikuwa tunapata takwimu ya jinsi ambavyo tutaokoa fedha nyingi sana za Serikali ambapo tulikuwa tunatumia karatasi nyingi sana, niIombe Serikali kwa kuwa tumeanzisha Mamlaka ya Serikali Mtandao basi mawazo haya mema ya Spika na Bunge letu yahamie kwenye maeneo ya taasisi zote za Serikali pamoja na Halmashauri ziachane na mambo ya kutumia karatasi. Hii itakuwa imeokoa fedha nyingi sana za Serikali na kufanya fedha hizo zitumike katika shughuli zingine za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nielekee kuchangia kwenye suala zima la ununuzi wa ndege. Naipongeza Serikali kwa jinsi ambavyo tumeionyesha dunia kwa kauli ambazo anatoa Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwamba Tanzania ni matajiri, hii imedhihirishwa kwa jinsi ambavyo tunanunua ndege zetu kwamba sisi tunao uwezo kuliko hata nchi zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu, najua dhamira ni kutaka tuongeze mapato kwa maana ya watalii lakini pia kusaidia usafiri wa ndani. Baadhi ya maeneo mengine yanahitaji uboreshaji wa viwanja vya ndege. Kwa mfano, Uwanja wa Ndege wa Masasi tunatumia Uwanja wa Ndege wa Mtwara kwa abiria kutoka Tunduru, Liwale, Nachingwea na Newala. Hata hivyo, kwa kuuboresha Uwanja wa Ndege wa Masasi itakuwa ni kituo kimoja muhimu sana kwa wasafiri wa kutoka maeneo haya na kuweza kuhakikisha tunaboresha usafiri katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke kwamba uwanja huu ndio unaotumiwa na Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Mheshimiwa Rais Benjamin William Mkapa. Uwanja huu uko katika hali mbaya sana na niiombe Serikali katika mipango ya uboreshaji wa viwanja vya ndege basi tuboreshe uwanja ule ili pia hata anapotua Rais wetu Mstaafu basi uwe ni uwanja wenye usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye reli, nishukuru sana mpango huu umeainisha kwamba tutakuwa na ubia kati ya Tanzania na wabia wengine katika ujenzi wa reli ya kutoka Mtwara hadi Mbambay lakini pia matawi ya Mchuchuma na Liganga. Niombe Serikali jambo hili ni la muda mrefu basi sasa ifikie kwenye utekelezaji wa kuingia makubaliano na hao wabia ili reli hii iweze kuleta matunda na tija katika mapato ya Serikali yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la kilimo, Waheshimiwa wengi wamezungumza kuhusiana na kilimo cha umwagiliaji. Wewe ni shahidi umezunguka nchi hii sana, nchi hii ina utajiri mkubwa sana wa kuwa na mito ambayo maji yake yake hayakauki. Tunao Mto Simiyu, Mto Mara na Mto Ruvuma lakini maji yake yote yanakwenda baharini bila sisi kuyatumia. Kwa hiyo, mii niiombe Serikali tuimarishe sana kwenye suala zima la kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo kwenye kilimo nilitaka kuishauri Serikali kwamba tunayo mazao ambayo yanatuingizia fedha za kigeni ikiwemo korosho, chai, pamba, pareto, tumbaku lakini unapokuwa na ng’ombe wa maziwa ni lazima uhakikishe kwamba baadhi ya fedha zinazopatikana kwenye maziwa ziende zikanunue nyasi na maboresho mengine ili tupate maziwa zaidi.

Kwa hiyo, niiombe Serikali kwamba lazima itenge fedha tunazozipata kurudisha kwenye mazao haya ili kuyaendeleza vinginevyo itafika wakati tutakuwa tunapata kiwango kidogo sana cha mazao kwa sababu hayapati fedha kutoka Serikalini kama ruzuku ya kusaidia kwenye uimarishaji wa mazao haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mimi ni mchangiaji wa mwisho nataka niokoe muda wako, naunga mkono hoja, ahsanteni sana. (Makofi)