Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii ya kuchangia katika Mpango huu ambao umewasilishwa na Serikali.Kwanza kabisa niungane na wale wote ambao wametoa pongezi za dhati kabisa kwa Mawaziri hawa kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kutengeneza Mpango mzuri, lakini Mpango huu ni mwendelezo wa mipango ambayo tumekuwa tunaizungumzia miaka yote toka tumeingia hapa Bungeni. Kwa kweli nataka niwapongeze sana, Mipango ambayo wanaileta inatekelezeka na tumeiona katika maeneo yetu mengi.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizungumzia tulivyofika hapa tulisema tutarekebisha reli yetu ya kati kwa kiwango cha standard gauge. Leo hii tunakwenda vizuri na tunakaribia kufika Dodoma. Sisi watu wa Tabora kama siku zote tunavyosema ni waathirika wakubwa sana wa reli hii ya kati kwa usafiri na usafirishaji wa mazao yetu, mfano, tumbaku, pamba na kadhalika. Kwahiyo, mpango unakwenda vizuri kwa kweli sisi tunapongeza sana kwa kazi nzuri inayofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizungumzia maeneo ya kufungua barabara zetu; mimi nina mfano mmoja; tulikuwa tuna mpango wa kuifungua barabara yetu ya Tabora – Itigi, kilikuwa kipande cha Chanya hajikamilika lakini leo zimetolewa zaidi ya bilioni 141, kipande kile kinakwenda kukamilika kwa asilimia zaidi ya 60 na wananchi watapata faida ya mipango mizuri tuliyokuwa tunaipanga huko nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizungumzia katika eneo la maji; katika Ilani yetu tulisema kwamba tutamtua Mama ndoo kichwani lakini kwa mipango mizuri ya Serikali hii na mipango mizuri ambayo inaendelea kutekelezeka, Mkoa wetu wa Tabora sasa unapata maji ya Ziwa Victoria, tuna asilimia zaidi ya 70 mradi ule unakaribia kufika sasa Tabora. Ni mipango mizuri ambayo inatekelezwa na Serikali yetu.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda na mimi nichangie kidogo pale ambapo wenzangu wamegusiagusia sana; ukiangalia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 14 inaeleza upatikanaji wa chakula. Ukichukua mwaka 2018/ 2019 ilikuwa asilimia 129, lakini mwaka 2019/2020 imekuja asilimia takribani 124 lakini sasa imekuwa asilimia 119. Ukiangalia uzalishaji wa chakula umepungua na ukiangalia upatikanaji wa chakula una athari kubwa sana katika uchumi wetu, unaathari kubwa sana kwa wananchi wetu na kadhalika. Kwahiyo ukiangalia kwamba kama chakula kinakuwa kinashuka, hapa tulishauri jambo moja; suala la kutengeneza miundombinu ya umwagiliaji katika kilimo chetu ni jambo la msingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako maeneo mengi ambayo katika maeneo yetu yanaweza yakatengenezewa miundombinu ya umwagiliaji na kuongeza upatikanaji wa chakula. Nashauri; katika kitabu chote nimejaribu kuangalia, hatujazungumzia sana uwekezaji katika umwagiliaji na hakika maeneo yapo, tukiwekeza katika umwagiliaji upatikanaji wa chakula utakuwa mzuri na utakwenda kuleta athari nzuri kwa uchumi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nipongeze eneo hili la TASAF kusaidia kaya maskini; nimeona zimetoka takribani bilioni 118 mwaka uliopita kusaidia kaya zile maskini. Nazungumzia hapa kwamba pamoja na kwamba tunawapa zile fedha kusaidia kusomesha watoto wetu na kupata mahitaji mbalimbali, ni jambo la msingi, lakini kule vijijini ili kumsaidia mtu ambaye ana kaya maskini ni kuwekeza vyema katika kilimo. Hizi fedha pamoja na kusomesha watoto wetu lakini wangetumia sehemu ya fedha hizi katika kufanya kilimo ambacho kimeboreshwa nina uhakika kabisa suala la chakula na hata huu mpango mzuri wa kusaida kaya maskini ungekuwa na maana zaidi na mwisho wa siku ungesaidia katika uchumi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie pia katika eneo la upaitikanaji wa maji; kwa sasa Serikali kutokana na mipango mizuri tuliyoipanga huko nyuma, hali ya upatikanaji wa maji vijijini inaongezeka siku hadi siku na hali inazidi kuwa nzuri kwa sasa. Ilani yetu ilisema inataka kumtua mama ndoo kichwani, tunaelekea kutimia kwa asilimia kubwa sana katika maeneo yetu. Nimezungumzia upatikanajiwa maji ya Ziwa Victoria kutoka Mwanza kuja Mkoani Tabora, lakini kuna uchimbaji mkubwa wa visima katika maeneo yetu mbalimbali. Ninachotaka kushauri hapani nini? Maeneo mengi tumechimba visima havitoi maji ya kutosha baada ya muda mchache. Serikali inatumia fedha nyingi na upatikanaji wa maji baadhi ya maeneo hayo unakuwa siyo mzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kushauri hapa ni nini? Yako maeneo ambayo tunaweza tukatega maji kwa maana ya kujenga mabwawa ambayo yale mabwawa yakija yakijengewa miundombinu kwanza yatakuwa ni chanzo cha uhakika, lakini pili, itazuia upotevu wa fedha mkubwa ambao unapotea katika uchimbaji wa visima hivi katika maeneo mengi ya vijijini na hausaidii wananchi wetu. Tukijenga mabwawa na haya maeneo yapo, kwanza mabwawa haya yatakuwa yana uwezo wa kuhifadhi maji ya kutosha, gharama zake ndogo lakini yatasaidia maeneo mengi hata kwenye eneo la umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie suala la miundombinu; mipango yetu pia ijielekeze kwenye miundombinu. Hapa nazungumzia miundombinu ya simu kwa maana ya mawasiliano lakini bado pia nataka nisemee suala la barabara. Unapozungumzia mawasiliano sasa hivi ni Benki unatembea nayo mkononi, ni kifaa kichokusaidia kufanya biashara zako kwa urahisi. Tukitengeneza mazingira ya kufanya wananchi wetu wakafanya biashara kwa urahisi kwasababu kutumia simu sasa unawezaukanunua bidhaa, unaweza ukatuma fedha, unaweza ukahifadhi fedha kwa usalama zaidi. Wananchi wetu wanaokaa vijijini Benki ziko mbali. Kwenda kutembea zaidi ya kilometa 100 kufuta benki wakati mwingine inakuwa ni gharama kubwa kwa wananchi wetu. Kwa hiyo, wanapokuwa na simu siyo tu kwa mawasiliano, inawasaidia kufanya biasharazao kwa urahisi. Kwahiyo nishauri Mpango wetu uangalie pia katika kuboresha upatikanaji wa mawasiliano katika maeneo yetu mbalimbali hasa vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo pia nataka nizungumzie barabara; unaporekebisha miundombinu ya barabara unasaidia hata kilimo chetu kupata soko kutoa mazao kule kijijini kupeleka kwenye soko, barabara zikiwa nzuri tunatumia gharama ndogo, mwisho wa siku tija inaonekana kwa mkulima na mwisho wa siku Serikali inaweza kupata mapato.TARURA wawezeshwe wapate bajeti ya kutosha.

Mheshimwa Mwenyekiti, nimalizie la mwisho kwenye eneo la afya; Ilani yetu inasema kila kijiji kiwe na zahanati, kila kata iwe na kituo cha afya. Tunakwenda vizuri kwa sasa, lakini nataka niiombe tu Serikali, mipango mizuri ya kujenga hospitali za wilaya sawa, lakini katika maeneo mengi bado vituo vya afya havijakamilika. Niombe mipango sasa ielekezwe katika kukamilisha baadhi ya maeneo ambayo hayana vituo vya afya ili kusaidia mrundikano utakaokuwa unakwenda kwenye hospitali zetu za Wilaya kwasababu rufaa ya zahanati unakwenda kwenye kata kwa maana ya kituo cha afya, ukitoka kwenye kituo cha afya unakwenda kwenye hospitali ya wilaya na ya mkoa. Sasa kwasababu ya kukosekana vituo vya afya katika baadhi ya maeneo, watu wanatoka kwenye zahanati wanakwenda kwenye hospitali za mikoa na kuzifanya zinashindwa kutoa huduma iliyo bora zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi tu nataka nipongeze kwa mipango mizuri inayotekelezeka ambayo tunakwenda nayo sasa kwa miaka minne inaonekana, Mheshimiwa Waziri wa Mipango hongera sana, Mheshimiwa Naibu Waziri hongera kwa kazi nzuri ambayo mnaifanya.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.(Makofi)