Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami nitoe mchango wangu kuhusu hoja iliyo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niungane na wenzangu kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Dkt. Mpango na Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wengine wa Wizara ya Fedha na Mipango kwa kazi nzuri ambayo wameifanya, na hata wakaja na documents hizi mbili ambazo sasa hivi tunazijadili; ile ya mwongozo wa uandaaji wa bajeti ya Serikali, lakini vilevile na mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo 2020/2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli ukisoma document hii unaona kabisa kuna uwiano na kile ambacho tumekitekeleza mwaka 2018 na ume-take into consideration ile miradi ambayo so far haijakamilika. Kwa hiyo, ni mpango ambao unaendeleza kile ambacho tumeshakianza. Ukiangalia vipaumbele vyetu bado ni vilevile. Kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa kazi nzuri ambayo wameifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu tunawajibika kikanuni na kisheria kuchangia, basi nina mchango katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza ni la kilimo, ule ukurasa wa 65. Ukurasa ule unazungumzia ujenzi wa maghala ili kuhifadhi nafaka. Mheshimiwa Ninashauri kwamba, ni wazo zuri kuwa na maghala ya kutosha kwa ajili ya hifadhi ya mazao yetu, hususan mazao ya biashara; korosho, pamba na kadhalika, lakini hili eneo tungetumia vizuri litakuwa eneo ambalo litaongeza uwezo katika Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ambazo zinalima zao la korosho tungeweza kuwapa kazi hii na ikawa chanzo kikubwa cha mapato. Sasa hivi maghala ya watu binafsi tunalipa zaidi ya shilingi 38/= kwa kilo. Sasa kama kwa kazi hii tutawapa fedha na Halmashauri nyingi za Mikoa ya Mtwara na Lindi wameshaandika maandiko yao, wamepeleka TAMISEMI na Wizara ya Fedha na Mipango ili wajenge maghala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, council ambayo inavuna kwa mfano tani 30,000 za korosho wanaweza kupata mpaka shilingi milioni 900 au shilingi bilioni moja kwa mwaka. Kwa hiyo, tukitoa fedha hizi kwa Halmashauri wakajenga maghala ya Halmashauri itakuwa chanzo kizuri cha mapato na hivyo tutaongeza uwezo wa Halmashauri zetu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Dkt. Mpango nakuomba sana kwamba hili ni wazo zuri lakini kazi hii tutoe kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa ili tuongeze mapato kwenye Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maghala haya yatatumika muda wote. Kwa maeneo ambayo tunalima korosho utahifadhi korosho, lakini vilevile muda wa msimu wa kusambaza pembejeo yatatumika kuhifadhi pembejeo. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, ile mipango ambayo imeandaliwa na Halmashauri ambazo zinalima korosho, ni muda mwafaka wa kufikiria tuwape fedha ili fedha hizi zizunguke katika Mamlaka za Serikali za Mitaa na hivyo kuongeza mapato katika Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili kwenye kilimo ni kuhusu muuzaji wa mazao yetu. Napenda sana sehemu hii ya mapendekezo ya mpango yaeleze wazi kwamba mazao ya biashara sasa ni muda mwafaka tutumie TMX. Sheria tulishapitisha mwaka 2015, lakini kuna kusuasua. Kwa mfano, msimu huu wa korosho tuliambiwa kwamba TMX ingeanza kutumika lakini ghafla tukaambiwa kwamba kuna elimu kwa wakulima haikutolewa na ukiangalia sana kuna uwoga tu ambao siyo wa lazima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuchukue nafasi hii sasa tutoe elimu kwa wadau wote wa mazao ya biashara ili Sheria yetu ya Commodity Exchange ambayo tuliipitisha mwaka 2015 ianze kufanya kazi. Nina uhakika kwamba kuna uwezekano mazao mengi ya biashara tukapata bei ya juu tukianza kutumia TMX. Ni taasisi ya Umma, nashangaa kwa nini tunakuwa na wasiwasi kutumia taasisi hii. Ukiangalia sana ni mfumo ule ule wa stakabadhi ghalani, isipokuwa ni advanced stage tu, kwamba unakuwa na maghala na unakuwa na huo mnada kama tunavyofanya sasa hivi kwenye mazao mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nashauri sana kwamba siyo kitu cha kutia uwoga, wadau wote wahusika wapewe elimu ya kutosha ili mazao yale ya kimkakati; korosho, kahawa, tumbaku, tuanze kutumia taasisi yetu ambayo tulishapitisha sheria yake mwaka 2015 na kuna watumishi wapo pale bado wapo idle.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu mwingine kwenye kilimo, Mapendekezo ya Mpango yameelezea vizuri kabisa kwamba kuna kujenga mazingira rafiki katika uwekezaji katika kilimo na bima ya mazao. Hiki ni kitu muhimu sana, lakini bado mazingira ya uwezeshaji kwa wakulima wetu siyo rafiki, mikopo kwa wakulima siyo rafiki, haipatikani kwa wakati, wakulima wanapewa masharti mengine ambayo wanashindwa kutekeleza. Unapomwambia mkulima wa mbaazi au wa korosho kwamba alete andiko la mradi, unamfukuza moja kwa moja, kesho hatakuja tena. Kwa hiyo, tutafute taasisi ambazo zitatoa mikopo rahisi kwa wakulima wetu ili waweze kuongeza uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mikopo hii ina riba kubwa ambapo mkulima mdogo hawezi kuilipa na haipatikani kwa wakati. Ukiniuliza mimi mkulima wa korosho kwamba unatakiwa upate mkopo mwezi wa ngapi ili ukusaidie katika kuzalisha korosho, nitakwamba mwezi Aprili, lakini mikopo ya aina hii inapatikana mwezi Oktoba wakati msimu au korosho zimeshaanza kuuzwa sokoni. Kwa hiyo, haimsaidii mkulima. Kwa hiyo, naomba tuangalie taasisi zilizopo jinsi ya kusaidia mikopo kwa wakulima wetu na kiwango cha riba kiwe kidogo na iwe rafiki na ipatikane kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kufunganisha uchumi na maendeleo ya watu. Ukisoma ukurasa wa 68 umezungumzia suala la elimu, nami niunge mkono kwa sababu kuna mapendekezo mazuri yametolewa pale kwenye elimu ya msingi, sekondari na vyuo vikuu, lakini tunasahau watumishi wetu; in-service training haipo na hakuna kitu muhimu kwa watumishi wetu kama in-service training. Kwa hiyo in-service training isisitizwe kwenye Mapendekezo ya Mpango wetu kwamba ni kitu muhimu ili watumishi wetu wapate maarifa na ujuzi mpya ili waweze kufanya kazi vizuri. Vilevile nilisahau, kuwe motisha kwa wafanyakazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la miundombinu, nalo napenda kushauri. Imeelezewa vizuri kabisa; ujenzi wa madaraja mipakani, ujenzi wa barabara kuunganisha mikoa, lakini changamoto iliyopo sasa hivi ni barabara za vijijini. Mpango unaelezea vizuri kwamba kujenga na kukarabati barabara zenye kufungua fursa; fursa nyingi sasa hivi zipo vijijini, lakini changamoto kubwa sasa hivi ni barabara za vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeanzisha TARURA lakini TARURA haina fedha, haina uwezo wa kufanya kazi, hakuna Wahandisi. Kwa hiyo, inaomba sasa ile formula ya kugawa fedha za Mfuko wa Barabara iangaliwe upya ili fedha za kutosha zipeleke TARURA ili iweze kutimiza majukumu yake. TARURA ndiyo wanajenga barabara za vijijini, tunatoa mazao vijijini na kupeleka sokoni. Kwa hiyo, mgao wa road fund uangaliwe vyema ili TARURA wapate fedha za kutosha ambazo zitasaidia katika ujenzi wa barabara za vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ujenzi wa barabara za mipakani, Mheshimiwa Waziri alifika Kilambo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji na aliahidi kutoa gari, nimpongeze na kumshukuru kwamba kwa taarifa tulizonazo gari imeshafika Mtwara lakini bado dereva hajapatikana. Kama Waziri ameshakula ng’ombe mzima sidhani atashindwa kumalizia mkia. Naomba Katibu Mkuu wako afanye mpango dereva apatikane ili Kituo cha Kilambo kipate usafiri ili waweze kukusanya vizuri mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya pili pale Kilambo lazima tujenge daraja la kudumu kati ya Tanzania na Msumbuji. Tulijenga Mtambaswala lakini Mheshimiwa Waziri kama alivyoona pale watu wengi kutoka Msumbiji wanatumia kivuko cha Kilambo. Ukitoka Kilambo mpaka Mji wa Palma - Msumbiji ni kama saa mbili wakati ukitoka kule Mtambaswala ni zaidi ya saa tano. Kwa hiyo, watu wengi wanapenda kutumia kivuko cha Kilambo na kwa sababu kwenye biashara hatuwezi kulazimisha watu na mizigo mingi inapita pale, tujenge daraja, tujenge kituo kingine cha forodha ili tukusanye fedha za kutosha kwa ajili ya kuongeza mapato ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na huo ndiyo mchango wangu, naunga mkono hoja. (Makofi)