Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri na Ofisi yake nzima kwa kutuletea Mpango mzuri ambao kwa kweli unatupa mwelekeo unaotosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile binafsi nataka nimpongeze Mheshimiwa Rais, hivi karibuni alitoka kuzindua barabara muhimu sana Mkoani kwetu na hususan Wilaya ya Ileje, barabara ya kwanza ya kiwango cha lami itakayokuja kutuunganisha mwisho wa yote na Wilaya ya Kyela. Hii ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa Wana-Ileje na kweli naomba nimshukuru sana kwa hilo. Namwomba radhi kwa kumsumbua sana huko nyuma akiwa Waziri kuhusiana na barabara hiyo, lakini mwishowe amekuwa mwaminifu na barabara inajengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, langu kubwa ni suala zima la ukuaji wa uchumi. Ukuaji wa uchumi umeendelea kuwa mzuri sana, kwa muda mrefu zaidi ya miaka kumi sasa nafikiri. Hili ni jambo jema sana, isipokuwa sasa tatizo ni kuwa ukuaji huu wa uchumi unachangiwa zaidi na maendeleo katika miundombinu. Ili ukuaji wa uchumi huu ulete tija ya maendeleo ya uchumi kwa wananchi mmoja mmoja na makundi ni lazima uunganishe uondoaji umasikini katika sekta zote muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu kabisa kuwa ili Taifa hili liendelee kwa haraka zaidi lazima tufungamanishe ukuaji wa uchumi pamoja na ukuaji wa maendeleo ya wananchi kwa maana ya kuondoa umasikini. Najua kwa muda mrefu, nchi yetu imelenga kuondoa umasikini tangu Awamu ya Kwanza. Bahati mbaya sasa hivi umasikini bado upo na maeneo mengine umekithiri. Hii ni kwa sababu bado hatujaweza kuunganisha maendeleo ya huku juu na maendeleo ya huku chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tufanye nini? Kwanza, kuna suala zima la kuongeza tija ya uzalishaji kule ambako wananchi wapo. Hii itasaidia sana kuboresha maisha, ajira na mapato ambayo wataweza kuwekeza katika maendeleo yao lakini vilevile itaongeza Pato la Taifa kwa maana ya kuleta uchumi mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tumekua mpaka asilimia saba na nukta fulani tukilinganisha na lengo letu la kufikia asilimia 10. Tungeweza kukuza kilimo kwa asilimia 10 ambayo tunaitegemea tungejikuta sisi uchumi wetu umeongezeka zaidi ya lengo letu la asilimia 10. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini kifanyike? Ni lazima sasa hivi Serikali ijikite katika kuongeza bajeti ya kilimo, ufugaji, uvuvi, biashara ndogondogo hasa za mipakani lakini vilevile kukuza soko la ndani la mazao ambayo tunazalisha sisi wenyewe. Tuna rasilimali nyingi ambazo zinaweza kutusaidia kuongeza mapato yetu lakini nyingi tunazisafirisha nje zikiwa ghafi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajikuta kuwa hata biashara yetu na nje yaani urari wa biashara umeshuka sana kwa sababu mazao tunapeleka nje yakiwa ghafi na mazao haya bei zake hatuzipangi sisi. Kwa hiyo, tunajikuta sisi ni watu wa kupokea bei badala ya sisi kutoa bei. Tungeweza kuweka viwanda vidogovidogo katika maeneo tunayozalisha, sisi wenyewe tungeongeza thamani na tukaweza kutumia kwanza hayo mazao tunayochakata kwenye soko letu la ndani na hivyo kuongeza ajira, kuongeza mapato na kuondoa umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napenda sana kuona jinsi ambavyo Serikali inakuja na mkakati mahsusi unaolenga kilimo cha kisasa, ufugaji wa kisasa, uvuvi wa kisasa. Hii itawezekana pale ambako wananchi hawa wanaozalisha wataunganishwa na taasisi za kifedha ili wapate mitaji itakayowawezesha wao kuwekeza katika maeneo haya kwa tija zaidi lakini vilevile, itawawezesha kupata mafunzo yatakayowawezesha kuwa wajasiriamali na wazalishaji wazuri na wanaozalisha kwa tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mifano duniani ipo ya nchi ambazo zilikuwa maskini au za chini kama sisi lakini wenzetu sasa hivi wako mbali. Vietnam ni nchi mojawapo ambayo unaweza ukasema wakati sisi tunapata uhuru na wao walikuwa katika ngazi ya kiuchumi sawa na sisi lakini sasa hivi wamepiga hatua sana. Siyo kwamba wao walikuwa na elimu kuliko sisi na wao viwango vyao vya elimu vilikuwa kama vya kwetu tu lakini walichofanya wao ni kuihusisha sekta binafsi kwenye ubia na wananchi katika uzalishaji wa kilimo, mifugo na viwanda vya kuchakata bidhaa zinazotokana na kilimo, mifugo na uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunaweza kufanya hivyo kwa kutumia ushirikiano wa Kusini kwa Kusini au nchi za kiafrika ndani kwa ndani. Haya ni mambo yanayowezekana, tujipange tuhakikishe kuwa tunaweka bajeti zinazotosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna vitengo katika Serikali vinavyohusiana na uwezeshaji wa vijana kwa kutoa mafunzo mbalimbali ambayo yatawawezesha vijana wetu wanawake kwa wanaume kuzalisha kwa tija lakini fedha inayowekwa pale ni ndogo. Kila siku Mheshimiwa Mavunde anajibu maswali hapa, anatutajia namba ya watu wachache sana wanaopata manufaa ya mafunzo haya. Hii Tanzania ni nchi kubwa, ina watu wengi na vijana ni wengi. Ukija na mifano ya vijana 7,000 waliofundishwa hiki au kampuni moja ya SUA iliyofanya hivi, hiyo haitoshi kabisa. Tuwekeze kwa kiasi kikubwa tutaona tija itakavyokuwa kubwa. Mwaka huu wakati wa bajeti nilisema tukiwekeza hata trilioni moja tu kwenye kilimo tutaona impact yake itakavyokuwa katika maendeleo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nachotaka kuhimiza hapa ni kwamba tunaendelea vizuri kiuchumi lakini tufike sasa mahali ambako tunakwenda pamoja katika masuala ya uzalishaji wenye tija. Tutumie sekta binafsi, ubia na teknolojia ili tuwawezeshe wananchi wengi zaidi na wao kuingizwa katika mfumo wa kifedha utakaowawezesha kupata mikopo na mitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile Benki Kuu itumie fursa ya kuwa wananchi wengi wa Kitanzania tayari wanatumia simu za mkononi na wanafanya miamala kwa kutumia simu na wao waje na bidhaa ambazo zinakidhi level hiyo ya wateja kuwatengenezea bidhaa ambazo wataweza kuzitumia kukopa, kuweka akiba lakini vilevile kwa kupunguza riba. Riba inawashinda wananchi wetu kukopa kwa sababu bado ni kubwa. Tunafahamu kuwa riba hata ikiwa asilimia 10 itawawezesha wananchi wengi zaidi kukopa vilevile wakakopeshwe katika njia ya makundi, maana mkulima mmoja mmoja inawezekana asiweze kukopeshwa na mabenki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka kabisa kuna wakati CRDB walianzisha mfumo wa kukopesha SACCOS halafu SACCOS wanakwenda kukopeshana wenyewe kwa wenyewe na CRDB wanakaa wanasimamia kuhakikisha kuwa ule mkopo unawezekana. Kwa kufanya hivyo, tutajikuta tunapunguza zile gharama za benki kujiingiza katika kumkopesha mtu mmoja mmoja lakini bado tukafikia uwezekano wa kukopesha wazalishaji wetu, wakulima, wafugaji, wavuvi, wakiwa katika makundi hayo au vyama hivyo vya ushirika na wakaweza kukopeshwa na wao wakaingizwa sasa katika mfumo mzima wa uchumi wa nchi na wakachangia pato kubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la biashara ya ndani. Kwa bahati mbaya Tanzania tunaagiza vitu vingi sana kutoka nje ambavyo tungeweza kuvizalisha wenyewe. Hili ni eneo ambalo lazima tulitilie mkazo na kwa vyovyote vile mimi sioni kama tuna haja ya kuona aibu kulinda viwanda vyetu au wazalishaji wetu, dunia nzima ndivyo wanavyofanya. Huwezi kwenda kumlisha mtoto wa jirani wakati wa kwako analia njaa jamani! Lazima tuhakikishe sisi wenyewe soko letu limejaa bidhaa tunazozalisha wenyewe na hii ndiyo itakayotuwezesha kuongeza mapato ya ndani. Tunategemea mapato kidogo sana kutoka kwa wafanyabiashara wakubwa wachache sana wakati kuna fursa kubwa sana ya soko la ndani kwa wazalishaji wadogo wadogo ambao wangeweza kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante sana. Kengele ya pili.

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, nashukuru sana. (Makofi)