Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mie nitoe mchango wangu kwenye huu Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2021. Awali ya yote nichukue fursa hii kumshukuru au kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna anavyotembea na Ilani ya Chama cha Mapinduzi na kwa namna anavyoangalia ustawi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie tu wenzangu upande wa pili wananchi wa Tanzania wanahitaji maendeleo, Watanzania wanahitaji ustawi, Watanzania wanahitaji amani, kwa kasi hii ya Dkt John Pombe Joseph Magufuli, kama hawana namna nyingine ya kuendesha vyama watafute kazi nyingine, hii spidi hawatoiweza kwa sababu kama mbinu wanakoendeshea vyama ni kutegemea makosa ya chama tawala au makosa ya Serikali, sasa hivi Serikali ya Awamu ya Tano, hayo makosa ni machache sana kuliko mambo mazuri. Kwa hiyo wananchi wanaiunga mkono Serikali ya Awamu ya Tano kwa sababu inafanya mambo mazuri, kwa hiyo kama wanategemea makosa ya Serikali hii ndiyo waendeshee vyama, basi watafute vyama vingine au watafute njia nyingine au watafute kazi zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapozungumzia CUF Liwale unazungumzia Zuberi Kuchauka, Zuberi Kuchauka hayupo CUF yuko CCM, wana Liwale hawako tena CUF, kwa hiyo msitegemee kwamba ngoma ya CUF bado ipo Liwale, hiyo nawapa taarifa nyinyi mnaolalamika kila wakati. (Makofi)

MHE. RAPHAEL J. MICHAEL: Taarifa.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ilikuwa ni tanbihi.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kuchauka subiri, taarifa Mheshimiwa Jafary.

T A A R I F A

MHE. RAPHAEL J. MICHAEL: Nampa taarifa mzungumzaji anayezungumza sasa hivi tumefika Liwale, bwana Kuchauka usitudanganye Chama ni taasisi siyo mtu kama wewe umehama basi waliobaki wanaendelea na CUF. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kuchauka.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Siipokei taarifa yake, juzi hapa wamelalamika wamesema Liwale hakuna watu waliochukua fomu, hakuna waliorudisha, Liwale hawajachukua fomu kwa sababu hawapo tena CUF wote wako CCM, ndiyo maana nikakuambia ukiiongelea CCM Liwale unamwongelea Kuchauka.

WABUNGE FULANI: Wacha uongo.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nijirejeshe kwenye Mpango. Mchango wangu kwenye Mpango huu nianze na miradi ya maji; tumefanya vizuri sana kwenye sekta ya elimu, tumefanya vizuri sana kwenye sekta ya afya, lakini bado tunasuasua kwenye sekta ya maji, watu wetu vijijini bado hawajapata maji kwa kiwango kinachoridhisha. Naomba Mheshimiwa Waziri sasa ipo sababu ya kujielekeza kwenye miradi ya maji, tuna miradi mingi sana ya maji, kwanza hapa napenda kumpongeza Waziri wa Maji na Naibu wake, kwa juhudi kubwa wanazochukua kurekebisha idara hii au kurekebisha Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiukweli miradi ya maji imehujumiwa sana, kwa hiyo naomba, kwa kuwa tumefanya vizuri kwenye afya na elimu, basi tujielekeze kwenye maji. Miradi mingi ya maji bado inaendelea kuhujumiwa pamoja na juhudi kubwa zinazoendelea kufanywa. Vile vile hata kwenye utoaji wa fedha kwenye zile certificates za miradi ya maji, bado spidi siyo nzuri sana. Kwa hiyo tunapokwenda kupanga mipango ya mwaka 2021, tuliangalie sana eneo hili eneo la idara ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo moja ambalo naona lilifanikiwa kwenye afya na elimu, ni huu utaratibu ambao Mheshimiwa Rais ameupendekeza wa force account. Ushauri wangu kwenye miradi ya maji basi kuwepo na hizi taratibu za force account kwa sababu miradi yetu ya maji mingi sana inapoteza fedha nyingi sana kwa sababu ya wakandarasi. Wakandarasi wetu wana makadirio ya juu sana kiasi kwamba unapeleka maji kijijini badala ya pale kijijini kuwa na virula tano au sita unakuta viwili au vitatu fedha nyingi zimepotea kwa wakandarasi, lakini tutakapoanza kutumia force account kwenye miradi hii ya maji tunao uwezo wa kusambaza maji pale yakafika kijijini na yakawafikia watu wengi zaidi. Jambo hili ikichukuliwa kwa umakini naona linaweza likatusaidia

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye miradi ya kimkakati tulikuwa na miradi ya kimkakati kwenye halmashauri zetu, lakini mwezi uliopita mwishowe Waziri alifuta baadhi ya miradi lakini au amesitisha baadhi ya miradi, lakini kwa nini ilipelekea hili? Jambo hili lazima tulifanyie utafiti tuliangalie kuna hii Sheria ya Manunuzi, napendekeza Mheshimiwa Waziri Sheria ya Manunuzi tuifanyie mapitio kwa sababu miradi mingi sana inakwama au haiendi kwa wakati kwa sababu ya Sheria hizi za Manunuzi ambapo kutafuta mkandarasi mmoja wa mradi inatuchukua zaidi ya miezi mitatu. Unapompa mkandarasi mradi ule anaposhindwa kuutekeleza kwa wakati, tunabadilisha tunatafuta mkandarasi mwingine, naye kumpata mkandarasi mwingine itachukua zaidi ya miezi mitatu mingine, utakuta hapo miezi sita mradi hauja-take off. Kwa hiyo katika jambo hili ushauri wangu ni kwamba Mheshimiwa Waziri tufikie mahali tuone ni namna gani tunakwenda kulitekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine naomba nijielekeze kwenye miradi ya kilimo, asilimia 65 ya wananchi wetu wanategemea kilimo, kwenye hii miradi ya kilimo naomba tuweke msisitizo kwenye idara ya masoko. Kwa sababu mkulima kama ana uhakika wa soko, suala la pembejeo atazitafuta kwa udi na uvumba atazipata kokote atakapozipata, lakini tatizo linakuja kwenye masoko. Kama hatutaweza kuimarisha masoko, juhudi kubwa tunazoingiza kwenye kutafuta pembejeo na kuimarisha kufanya tafiti mbalimbali, kuangalia magonjwa ya mazao na namna ya kuendeleza kilimo, kama hatujaweza kupata masoko ya uhakika juhudi hizi ambazo tunazielekeza kwenye kilimo bado hazitatuletea matunda tunayokusudia. Kwa hiyo, ushauri wangu kwa upande wa kilimo ni uimarishaji wa masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia huu uimarishaji wa masoko uende sambamba na uimarishaji wa miundombinu ya barabara, yapo maeneo yanapatikana mazao ya kutosha, lakini mazao yale kuyafikia kwenye masoko inakuwa ni shida kubwa na yanapofika kwenye masoko bei inakuwa ni ya juu sana ambayo watu wanashindwa kumudu. Kwa hiyo uimarishaji wa kilimo uendane sambamba na masoko vilevile na uimarishaji wa miundombinu kuhakikisha mazao haya yanafika kwenye soko kwa muda unaotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hii miradi mikubwa ambayo Mheshimiwa Rais anaitekeleza ni jambo zuri sana, nami niseme tu kwamba Watanzania wanamwelewa vizuri sasa Mheshimiwa Rais wetu na nia yake kubwa ya kuipeleka nchi yetu kwenye uchumi wa kati. Hapa napo naweza kutoa ushauri kwamba sasa Serikali tuanze kufikiria katika baadhi ya miradi kuimarisha utaratibu wa PPP ili Serikali iweze kutoa huduma za kijamii kwa mfano kama maji, afya, elimu, ni lazima tuhakikishe kuwa baadhi ya miradi ambayo inatumia fedha nyingi sana fedha zetu za ndani, kuanza sasa kuanza kufikiria kushirikisha hii PPP.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa napo kuna tatizo kubwa la urasimu, naiomba sana Serikali, Serikali ya Chama cha Mapinduzi, Serikali sikivu, Serikali ambayo inapanga mipango inayopangika, mipango ambayo inayotekelezeka, basi na hapo tuendelee kuimarisha uwekezaji, tuendelee kuimarisha ushirika wa watu binafsi na miradi mikubwa Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo Watanzania ambao wanapenda kushiriki kwenye hii miradi mikubwa na midogo, lakini shida kubwa inakuja kwenye mitaji. Hapa napo naomba niishauri Serikali kuangalia namna gani ya kuwashirikisha au kuwapa mitaji au kuwawezesha watu wa sekta binafsi kushiriki kwenye uchumi huu ili tuweze kutoka wote kwa pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitaweza kukaa chini bila kutaja sekta ya vijana pamoja na ajira. Suala hili la ajira ni muhimu sana, naishauri Serikali ili kuondokana na dhana kwamba mtu yoyote au mhitimu yeyote ategemee kuajiriwa na Serikali, tuanze kufikiria sasa kwamba wahitimu wetu waweze kujitegemea. Watawezaje kujitegemea, ni pale ambapo Serikali itajikita kuimarisha miundombinu ya watu kuweza kujitegemea kama vile kuendelea kuimarisha shule zetu za VETA, shule ambazo zitaandaa wahitimu wetu kujitegemea. Jambo hili ni muhimu sana kwa vijana wetu kwa sababu leo hii kila mhitimu anafikiria kutembea na vyeti akitafuta ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachoshangaza zaidi hata wale ambao wahitimu wametoka kwenye vyuo labda mtu ametoka kwenye chuo cha mifugo, chuo cha kilimo, chuo cha ufundi bado na yeye anatembea na vyeti akitafuta ajira. Hii ni kwa sababu watu wetu bado hatujawajengea uwezo wa kujiajiri.

Kwa hiyo, pendekezo langu pamoja na kuimarisha vyuo vyetu vya VETA na vyuo vya ufundi, bado Serikali ione umuhimu wa kuwawezesha vijana hawa, kuwahamasisha vijana hawa wajiunge kwenye vikundi mbalimbali ili waweze kupatiwa mitaji ili waweze na wao kushiriki kwenye uchumi wa nchi yetu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja hii ya mapendekezo ya Mpango, tuko vizuri. (Makofi)