Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nami nafasi ya kuweza kuchangia katika mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka wa 2020/2021. Awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, Naibu Waziri pamoja na timu yote na niipongeze Serikali kwa ujumla wake ikiongozwa na Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa namna ambavyo imekuwa ikitekeleza Mpango wa Maendeleo katika bajeti iliyopitia na bajeti hii ambayo inaendelea sasa ya mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona yako mafanikio mengi katika miradi mingi ya kielelezo ukiwepo Mradi wa umeme wa Stiegler’s Gorge au bwawa la Mwalimu Nyerere, tumeona kwenye standard gauge, ununuzi wa ndege, uboreshaji wa miundombinu, lakini zaidi sana katika sekta ya afya tumeona juhudi kubwa sana za ujenzi wa hospitali za wilaya, lakini na vituo vingi vya afya ambavyo kwa kweli vitakwenda kuboresha maisha ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa zaidi pia tumeona mchango wa Serikali hii katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali ambayo yameongezeka kwa kiasi kikubwa na inatusaidia sana sisi katika kutekeleza mipango, ukizingatia kwamba mipango mingi sasa ya Serikali tunaipanga kwa kutumia fedha zetu za ndani. Mfano, katika mapendekezo haya ambayo yapo, katika fedha za mpango wa maendeleo zaidi ya bilioni 12.6 za bajeti ya maendeleo zaidi ya trilion 10.1 zitakuwa sasa zinatokana na fedha zetu za ndani. Kwa hiyo tunaipongeza sana Serikali kwa juhudi kubwa ambayo imefanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichangie katika sekta mbalimbali katika kuboresha Mpango wetu wa Maendeleo wa mwaka 2020/2021, nikianzia na sekta ya afya, kama nilivyosema juhudi kubwa imefanyika katika Serikali hii ya Awamu ya Tano, lakini niombe sana katika Mpango huu kazi tulioifanya kwa mfano kwenye vituo vya afya, pamoja na wingi wa vituo vya afya tulivyofanya ukilinganisha na idadi ya Watanzania zaidi ya milioni 55 waliopo sasa, juhudi kubwa bado inatakiwa katika eneo hili. Pia tujue kwamba bila kuwa na afya njema hata kazi zetu na mipango yetu ya maendeleo haiwezi kutufikisha vizuri. Kwa hiyo niiombe sana Serikali na Mheshimiwa Waziri waangalie namna ambavyo wataongeza vituo vya afya. Ushauri wangu katika hili ni kwanza kukamilisha maboma ambayo yamekwishaanzishwa na wananchi wenyewe. Awamu zilizopita ikiwemo Awamu ya Nne ya Mheshimiwa Kikwete tulianza, wananchi wamejitolea sana katika ujenzi wa maboma ya vituo vya afya na maboma mengine kwenye sekta ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya afya, kwa mfano katika jimbo langu, yapo boma katika Kata yetu ya Ngimu lakini nyingine Makuro ambayo yamekaa kwa muda ya miaka 10, wananchi hawa wametoa nguvu zao, lakini mpaka leo maboma hayo hayajaweza kukamilika na kwa kweli wananchi wamekuwa wamezidiwa na ukamilishaji wa maeneo hayo kutokana na mipango mingi ambayo tunawapelekea, ukizingatia kwamba kwa kila fedha za Serikali zinazokwenda asilimia 20 ya nguvu za wananchi inahitajika huko. Kwa hiyo niombe sana Serikali ifanye mpango wa makusudi kama ilivyofanya kwenye sekta ya elimu tuweze kukamilisha maboma haya ambayo yapo katika nchi nzima na wananchi walishajitolea katika kuyajenga ili kusudi tuweze kuboresha huduma za . Tunahitaji afya bora na hasa tunahitaji kuzuia vifo vya wa kina mama na watoto wakati wa kujifungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye sekta ya maji; sekta hii ni muhimu sana, kwa kweli tunao uwezo wa kufanya kila kitu, lakini tunaweza tukashindwa kuishi bila maji. Tumewekeza sana katika maeneo mengi, tumewekeza vizuri katika miundombinu, sasa hivi tunaendelea kuwekeza katika miundombinu ya umeme, tunaendelea kuwekeza katika maeneo mengine, lakini maji ambalo ni hitaji la msingi la maisha ya binadamu kwa kweli bado tumekuwa na nguvu kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia katika bajeti ya maji, imekuwa ni kidogo sana na haina uwezo wa kututoa hapa tulipo. Tunajua Ilani ya Chama cha Mapinduzi inataka angalau kwa upande wa vijijini tufikie asilimia 85 mpaka kufikia mwaka unaokuja. Sasa hivi tunaongelea chini ya asilimia 65, utaona kazi hiyo ni ngumu, kazi hiyo ni kubwa, kwa hiyo niombe sana, zitafutwe fedha za maji. Mwaka jana tulikuja na ombi hapa la kuongeza shilingi 50, lakini ombi hilo halikukubaliwa na sisi hatupingani na hilo, lakini madhali vinaweza vikapatikana vyanzo vingine, suala la maji ni la muhimu sana wewe mwenyewe ni shahidi, Mheshimiwa Rais alipotembea kila mahali alipokwenda ni maji, maji, maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la maji linawagusa sana akinamama ambao ndio wazalishaji wakubwa na wanatumia muda mwingi sana kwenye kutafuta maji na tunaona kwamba takwimu tunazokuwa nazo zinaweza zisiwe za kweli kwa sababu tunadhani kwamba kisima kimoja kinakwenda pale kama kinasema kinahudumia wananchi 250 au wananchi 500 au 600, hizo ndizo takwimu tunazokuwa nazo, lakini utakuta wengine wapo zaidi ya mita 400 ambayo ndiyo sera yetu au Awamu hii ilikuwa imejiwekea, kusogeza huduma karibu na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niiombe sana Serikali, ukienda katika miradi ya vieleleze Sekta ya Maji sio sekta ya muhimu, sio sekta ya kipaumbele. Sasa hili halitupi sisi nafasi ya kuweza kutenga fedha nyingi kwenye kuboresha miundombinu ya maji. Niombe Mheshimiwa Waziri tulipe kipaumbele cha kwanza kabisa sasa hivi kwenye bajeti inayokuja hii ya mwaka 2020/2021 ili tuweze kuwatua akina mama ndoo kichwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata walioko mijini bado hawajapata maji ya kutosha, bado kumekuwa na urasimu mkubwa. Ukiangalia hata katika Mkoa wa Dar es Salaam shida ya maji bado ni kubwa, katika majiji yote shida ya maji bado ni kubwa. Kwa hiyo niombe sana Wizara hii iangalie na niombe sana Sekta ya Maji iwe ni moja ya sekta za kipaumbele katika Taifa letu. Tunaweza hata tukapunguza kwenye maeneo mengine; tunaweza tukaishi bila lami, tunaweza tukaishi bila miundombinu bora huko lakini hatuna uwezo wa kuishi bila maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine lipo katika kilimo; Sekta ya Kilimo inaajiri zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania, wengi wao – asilimia 90 – wanatoka vijijini ambako mimi ni mwakilishi wao, lakini pia wako wakulima ambao wanaishi mijini. Bado mpango wa Serikali haujatenga fedha za kutosha katika kuboresha Sekta ya Kilimo, bado tunahitaji kuongeza fedha, tunahitaji kuongeza uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika mpango ambao umewasilishwa sasa, fedha nyingi zinazotegemewa ni hizi za mpango wa kuendeleza Sekta ya Kilimo ya Awamu ya Pili (ASDP II). Fedha hizi hazitoshi. Fedha hizi zina maeneo maalum, yako mazao mengine ambayo hayawi-covered kabisa kwenye mpango huu. Mpango huu wa ASDP II wenyewe umelenga zaidi kwenye mazao yale ya kimkakati ambayo utakuta ni korosho, pamba, kahawa, chai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa yapo mazao mengine ambayo kwa kweli yanahitaji yapewe kipaumbele; tuna mazao ya mafuta kama ufuta, alizeti mchikichi, karanga na maeneo mengine. Haya yanahitaji kupewa kipaumbele kwa sababu tunajua kwamba nchi yetu inatumia fedha nyingi, zaidi ya bilioni 410 katika kuagiza mafuta ya kula kila mwaka. Fedha hizi ni nyingi sana, tusipowekeza katika kilimo hatuwezi kuwasaidia wananchi wetu. Huku ndiko wananchi wetu walio wengi tunakotoka sisi wote waliko. Kwa hiyo, niombe sana Sekta ya Kilimo ipewe umuhimu na kipaumbele cha kwanza pia ili kuweza kuboresha maisha ya wananchi wetu kule vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukumbuke kwamba nchi yetu sasa tunakwenda na tunakwenda kwenye uchumi wa kati ambao utaongozwa na uchumi wa viwanda. Viwanda hivi vitahitaji malighafi za kutoka mashambani, viwanda hivi vitahitaji malighafi za mifugo, viwanda hivi vinahitaji malighafi kutoka kwenye uvuvi. Sasa tusipowekeza katika maeneo haya tutajikuta kwamba hatuwezi kufikia malengo yetu vizuri na ndoto ya Mheshimiwa Rais wetu ya kutufikisha uchumi wa kati 2025 haitaweza kutimia kwa sababu ya uwekezaji mdogo katika Sekta ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapozungumzia Sekta ya Kilimo ni pamoja na mifugo vilevile. Tumeona zipo changamoto nyingi, na niipongeze sana Wizara ya Mifugo, sasa hivi wamekuja na utaratibu wa uhimilishaji wa mifugo ambao unawasaidia wafugaji wetu kuwa na mazao bora zaidi.

Kwa hiyo, niombe sana uwekezaji uongezwe katika sekta hizi ikiwa ni pamoja na Sekta ya Uvuvi. (Makofi)

MWENYEKITI: Kengele ya pili imegonga Mheshimiwa.

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja.