Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Miraji Jumanne Mtaturu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika hoja ambayo iko mezani. Kwa sababu leo itakuwa ni siku ya kwanza kuchangia naomba nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi na uhai wa kuweza kuchangia hoja hii ambapo naishauri Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake ya Wizara nzima, Naibu Waziri pamoja na Katibu Mkuu na watendaji wote kwa kuandaa na kutuletea Mpango huu ambao kwa kweli ni Mpango ambao umeendelea kutuonesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kuwaletea Watanzania maendeleo. Naomba nichukue nafasi hii kuwapongeza na naomba niseme tu kwamba tutaendelea kutoa ushauri ambao utakuwa na tija kwa ajili ya kuleta maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba Mpango wenyewe huu unakwenda kumalizia katika Mpango wa Miaka Mitano ninajua mambo mengi yako dhahiri ambayo yameonekana yameshafanyika. Zaidi niseme tu kwamba kuwa na Mpango ni jambo moja lakini kuusimamia na kuutekeleza ni jambo la pili. Kwa hiyo, sisi kwenye hili tunawapongeza kwa sababu tumekuwa na Mpango na sasa tunaona namna ambavyo kwa muda huu unaenda kumalizika mwaka wa tano mafanikio makubwa katika maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kwa kweli kwa dhati kabisa kumpongeza sana Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa namna ambavyo ameonesha dhamira ya dhati katika kuhakikisha kwamba anawaletea wananchi maendeleo. Najua kwamba utashi wake ndiyo ambao unatupa hata jeuri au inaipa jeuri Serikali kuhakikisha inafanya kazi vizuri kwa sababu tumekuwa tukipata fedha ya kuweza kutekeleza miradi hiyo. Tunaweza tukawa na mipango mizuri sana isipowezeshwa itakuwa ni kazi bure na itakuwa inabaki kwenye vitabu kama ambavyo tumekuwa tukiona baadhi ya maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba maeneo mengi ambayo naweza kuyasema ni yale ambayo nasema kwamba tumeanza kuona dhamira ya Serikali katika kukusanya mapato. Unaweza ukawa na mpango mzuri lakini ukawa hauna fedha lakini ukiwa na mpango mzuri ikiwa ni pamoja na kukusanya mapato inakusaidia wewe kuhakikisha kwamba unatimiza malengo ambayo yako mbele yetu. Jambo kubwa ambalo ni vizuri tukalisema ni dhamira ile ya kusimamia na kuzuia mianya yote ya kukwepa kodi katika nchi yetu. Siyo hivyo tu ni pamoja na kusimamia na kutokomeza kabisa rushwa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika baadhi ya maeneo ambayo tulikuwa tunateseka sana ni pale ambapo baadhi ya watumishi ambao hawana dhamira njema wamekuwa hawafanyi vizuri sana katika kusimamia mapato yetu. Kwenye hili, naomba niipongeze Serikali kwa namna ambavyo imesimamia na imeendelea kuongeza mapato katika nchi yetu yanayonifanya tuweze kutekeleza mipango ambao tunajipangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo yote nieleze sasa yale ambayo yanaonekana waziwazi. Tumeona namna ambavyo tunaboresha sana miundombinu ya barabara ambayo kwa kweli imekuwa ndiyo nguzo kuu ya uchumi wa nchi yetu. Niseme hapa katika mpango nimeona namna ambavyo mwaka huu ambapo tunaelekea kwenye bajeti tutaenda kujikita katika kuongeza fedha ambazo zinakwenda kuongeza uwezo wa kujenga barabara zetu ikiwa ni barabara za lami na madaraja makubwa na kadhalika. Niombe tu kwamba haya ambayo yamepangwa basi yawekwe vizuri kwa ajili ya kutoa fedha ili tuweze kuona miradi hiyo inaweza kufanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hivyo tumeona reli ya SGR inajengwa. Ni dhamira ya dhati tuliamua kama Taifa na leo tunavyoona speed ni kubwa sana tuko zaidi ya asilimia 60 ya utekelezaji wa mradi. Kwa hiyo, niseme tu kwamba hii nayo itakuwa ni kichocheo muhimu katika uchumi na usafirishaji wa mizigo ikiwa ni pamoja na kupunguza bei ya bidhaa sokoni. Bei ya bidhaa ikipungua maana yake itamsaidia mwananchi wa kawaida kuweza kupunguza mfumuko wa bei kwa sababu bei itakuwa chini katika usafirishaji wa mizigo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo yote hatutaacha kusema maneno machache kwenye sehemu ya uboreshaji wa ununuzi wa ndege. Hili jambo tusipolisema na dhamira ya dhati ikaonekana maana wengine wamekuwa wakipotosha eti wanathaminisha ndege wanasema vingejengwa vituo vya afya kadhaa. Niseme tu kama Taifa lazima tuamue nini cha kufanya, huwezi kusema unaogopa kununua shati jipya kwa sababu huna utoshelevu wa kubadilisha kula mboga, huwezi kuogopa hilo, lazima uamue kwamba ndege zinazonunuliwa zinaenda kuongeza uwezo wetu wa kuweza kuhudumia sekta ya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tumekuwa tukiona na tukilalamika na mimi nimekuwa nikiwaona Waheshimiwa Wabunge wanasema ndani ya Bunge kwamba haiwezekani watalii washukie Kenya waletwe kwa magari kuja kwenye mbuga zetu na baadaye warudi wakapandie Kenya kwa shirika lingine la ndege. Leo tunapata ndege maana yake tuna uwezo sasa wa watalii wale wote kushuka kwenye viwanja vyetu ndani ya nchi yetu na wanakwenda moja kwa moja kwenye utalii. Utalii ndiyo sekta ambayo inaongoza katika mapato katika nchi yetu. Kwa hiyo, tunapoboresha Shirika la Ndege maana yake moja kwa moja tunaiboresha hii sekta ya utalii ambayo ndiyo inaleta fedha nyingi ambapo mwisho wa siku itajenga vituo vya afya, shule, itaboresha elimu bure pamoja na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Taifa lazima tujivunie kwa sababu lazima nchi isonge mbele kwa kuwekeza kwenye mambo makubwa. Kwa hiyo, hatuwezi kuwa sisi wenyewe tunafanya mambo makubwa lakini hatujui kama tunafanya mambo makubwa. Hii haitatujenga kama Taifa, Watanzania tuipende nchi yetu kwa yale makubwa mazuri tunayoyafanya. Tofauti ya vyama vya siasa isitufanye tuondoke kwenye reli, lazima tujivunie na sasa hivi tunaona ATCL wanafanya vizuri, Mheshimiwa Waziri anayehusika na sekta hii yupo pale kwa kweli kazi inafanyika vizuri na sisi kama Waheshimiwa Wabunge ni lazima tuunge mkono juhudi kubwa hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kueleza maelezo haya, kabla muda wangu haujaisha, nitoe maneno machache ya ushauri kwenye suala la kilimo. Waheshimiwa Wabunge wengi wamesema, lakini naomba na mimi nieleze kidogo, asilimia 80 ya wananchi wetu wanafanya kilimo. Kama kweli tutaweza kuwekeza kwa dhamira ya dhati katika kilimo itasaidia sana kutuongezea pato la Taifa lakini itasaidia uchumi wa mwananchi mdogo kule chini chini, wakati wa kutegemea msimu wa mvua umepitwa na wakati, tuongeze nguvu katika kilimo cha umwagiliaji na zaidi tuongeze uwezo wetu wa kusimamia miradi hiyo na itoe matokeo, katika baadhi ya maeneo tuweze kuvuna zaidi ya mara mbili ili tukipata mapato ya kutosha kwenye eneo hili itasaidia hata mapato ya ndani katika halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halmashauri zetu nyingi zinategemea mazao katika mapato, tukiwekeza kwenye kilimo naamini kabisa tutaenda kuongeza uwezo wa wananchi wetu na kipato chao katika kaya. Kipato cha kaya kikifanikiwa ndiyo tutasaidia kwenda kwenye huo uchumi wa kati ambao tunausema kwa sababu tunaangalia na tunatathimini namna ambavyo mwananchi anajipatia kipato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiondoka kwenye eneo hilo, niende sasa kwenye eneo la pili la miundombinu. Tunaamini zile barabara kubwa zile trunk roads zinajengwa kwa kiwango cha lami, lakini nieleze kidogo kwenye barabara ambazo ziko chini ya TARURA. TARURA wamekuwa wakitengewa fedha kidogo sana naamini wanataka kujenga madaraja, wanataka kuongeza uwezo wa ujengaji wa barabara zao, lakini fedha wanazopata ni ndogo sana hazina uwezo wa kututoa pale na ile dhamira ya kuanzisha hii agency haitakuwepo kama hatutawapa fedha za kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana kwenye mpango huu naona imeguswa na imewekwa, lakini naona kabisa namna ambavyo mfano kama Wilaya ya Ikungi pale, zipo barabara ndevu lakini nyingi hazijawahi kutengenezwa, ni barabara za asili kama mapalio, naamini kabisa Mheshimiwa Waziri ananielewa ninavyoeeleza hayo, kwa sababu TARURA huwa wanaleta maombi yao na yamekuwa wakipata fedha kidogo sana, wakati ambapo barabara hizi zikijengwa zitasaidia kusogeza mbele suala la kuleta maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikimalizia kwenye eneo la umeme juhudi naziona ni nzuri sana, nipongeze sana Serikali kwa namna ambavyo wizara imeendelea kusimamia upatikanaji wa umeme kwa kupitia miradi ya REA, tatizo kubwa ambalo naliona lipo kwa wakandarasi, wakandarasi wamekuwa hawatekelezi miradi kulingana na mikataba yao, wakandarasi wengine wanalalamikiwa hata na wafanyakazi wao, hivyo inasababisha kufifisha juhudi za kuwapelekea wananchi umeme, kwenye eneo hili ni vizuri Serikali kupitia Wizara husika waweze kusaidia kuhakikisha kwamba wananchi wanapatiwa umeme mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ndogo ambayo ipo pia ni maeneo yale ambayo wanasema kwamba wanapelekewa umeme kwenye vijiji lakini wanapelekewa vijiji ambavyo viko pale pale centre, umeme hauendi mpaka kwenye vitongoji. Inawezekana dhamira ya Serikali ni hiyo, lakini imekuwa tunavuka baadhi ya vitongoji, jambo hili linatuweka kwenye wakati mgumu ambapo tunakosa majibu, wakati hamu ya wananchi ya kupata umeme ni ya hali ya juu. Baada ya maneno haya, naomba tu niendelee kusema CCM hatujakataa kuingia uwanjani, tuko tayari, lakini naomba pia na wao wafuate mwongozo uliowekwa ili waingie uwanjani wakiwa salama. Huwezi kuingia uwanjani huna viatu wakati wenzako wanaingia na viatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)