Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuwa miongoni mwa wanaochangia Mpango. Awali ya yote naishukuru sana Serikali, namshukuru Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wake kwa kuleta Mpango mzuri ambao unaonyesha dira ya maendeleo yetu. Katika mpango huu yapo ambayo yametekelezwa na Serikali, kimsingi tunaipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunampongeza Mheshimiwa Rais kwa jitihada kubwa sana ambazo amezifanya za kuboresha vitu vingi ambavyo amevileta katika nchi yetu. Kwenye Mpango amezungumzia suala la miundombinu. Tumeshuhudia Serikali ikiboresha eneo la miundombinu kwa ujenzi wa barabara karibu nchi nzima. Haya ni maendeleo makubwa sana na unapotaka maendeleo, kwanza rahisisha shughuli za kuwafikia wananchi, lakini bado Serikali tumeona ikitekeleza miradi mikubwa, wameboresha viwanja vya ndege karibu 11 ambavyo tunategemea vitarahisha sana shughuli ya uchukuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Serikali imenunua ndege ili ziweze kukuza Sekta ya Utalii, lakini kutoa huduma kwa wananchi. Serikali bado imeendelea kuwaona wananchi hasa wale wa chini, imekuja na Mpango wa kununua au kujenga meli mpya kwenye maziwa makuu; Ziwa Victoria, Ziwa Tanganyika na Ziwa Nyasa. Haya ni maendeleo makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Ziwa Victoria kuna ujenzi wa meli mpya itakayokuwa na uwezo wa kuchukua abiria 1,200 na karibu tani 400 za mizigo. Eneo hili watakuwa wamewasaidia sana wananchi wa kanda ya ziwa, ambao kwa kipindi kirefu walikuwa wana shida kubwa ya usafiri wa majini. Vile vile kuna ukarabati wa meli ya MV. Victoria, haya ni maendeleo makubwa sana katika kipindi kifupi. Tunaona mipango ambayo iliwasilishwa na Serikali ikitekelezwa kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, bado kwenye hiyo hiyo Sekta ya Uchukuzi, Serikali imeamua kusaidia au kupanua ujenzi wa bandari pale Dar es Salaam. Bandari yetu ilikuwa na uwezo mdogo, leo hii tunashuhudia maendeleo makubwa sana ya upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam na tumeshuhudia nchi yetu ikipokea sasa meli kubwa ambazo zinatua kwenye bandari yetu na kupakua mizigo ambayo haikutegemewa huko nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tuna Bandari ya kule Mtwara, imepanuliwa. Tunaamini eneo lile la Kusini nalo litakuwa katika huduma kubwa ya maendeleo katika nchi yetu. Bado kuna upanuzi wa Bandari ya Tanga, ambayo nayo ipo katika Mpango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la Kanda ya Ziwa Victoria, kuna ujenzi wa kivuko kikubwa karibu kilomita tatu kutoka Busisi ambacho kitatoa huduma kubwa sana kwa wananchi. Maeneo haya ni Serikali inatekeleza kwa ajili ya kusaidia wananchi kukuza uchumi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza sana Serikali, lakini tumeona mapinduzi makubwa sana katika nchi yetu. Ili uweze kuendelea, tunahitaji miundombinu na nishati ya umeme. Mheshimiwa Rais kwa nia nzuri ameamua kujenga bwawa kubwa la umeme katika Mto Rufiji; bwawa lile maarufu kwa kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere. Hili litakuwa ni eneo ambalo litawasaidia wananchi wote katika nchi yetu. Ninaomba hizi jitihada tuziunge mkono na tuangalie maeneo mengine ambayo yalisahaulika yaweze kupelekewa miradi ya umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kilimo. Tukitaka kuwasaidia wananchi walio wengi, baada ya Serikali kuweka miundombinu, karibu maeneo yote, sasa Mheshimiwa Dkt. Mpango elekeza mawazo yako ukuze Sekta ya Kilimo ambayo inawaguza wananchi wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili natoa ushauri, kwanza Serikali ianze kufikiria kutoa ruzuku kwenye mazao ya korosho, pamba, chai, tumbaku na yale mazao makubwa ambayo yanatuletea fedha za kigeni kwa wingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yeyote ile iliyoendelea inawasaidia sana wananchi hasa wakulima kuweza kushindana kwenye ushindani. Pale mazao yanapokuwa yameanguka, lazima Serikali iweze kuwasaidia hawa wananchi wapate nguvu, lakini wasiposaidiwa watakuwa na maeneo mabaya ambayo yatawafikisha kutokufanya kazi na kuachana na hayo mazao ambayo yalikuwa yakiwaingizia kipato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie zao la pamba ambalo linazalishwa wilayani kwangu. Zao la pamba wananchi walilichukulia kwamba ni zao ambalo ni sasa lingewatoa kwenye umasikini na wamezalisha kwa kiwango kikubwa na pamba nzuri, kuzidi hata ile iliyokuwa inazalishwa ambako imetoka mbegu zake maeneo ya ukanda wa ziwa, lakini mpaka sasa wakulima bado hawajauza pamba, iko majumbani kwao. Naomba eneo hili mkalifanyie kazi, mboreshe ili wananchi waweze kupata huduma inayostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao lingine ni tumbaku. Nchi yetu ilikuwa inapata fedha nyingi kupitia zao la tumbaku. Kwa bahati mbaya sana mwaka huu yapo makampuni ambayo yalikuwa yananunua tumbaku kwenye nchi yetu kampuni kama TLC lakini imeacha kununua zao hili. Tuna mikoa zaidi ya 12 inayozalisha zao la Tumbaku ukiwemo na Mkoa wa Kigoma ambapo Mheshimiwa Waziri ametoka wananchi hawana mahali ambapo watauza tumbaku walizokuwa wanazalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashauri sasa Serikali iangalie eneo la Kitengo cha Masoko, kwenye masoko bado hamjapaangalia. Tunahamasisha kilimo lakini kuwatafutia wakulima masoko bado Serikali haiajawekeza kwa kiasi cha kutosha. Niombe eneo hili nendeni mkalifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na kuboresha eneo la masoko pia ni muhimu kuboresha mazao ya chakula ambapo mkiwasaidia hawa wakulima na mkawawekea mazingira mazuri ya masoko kilimo ni eneo ambalo litaajiri wananchi wengi na Serikali itakuwa inanufaika kupitia huduma mbalimbali na kodi zitakazokuwa zinatokana na upatikanaji wa fedha. Tunaomba sana hapa Serikali mkapafanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo tunapenda kushauri Serikali ni kwenye …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Muda umekwisha, ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)