Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi jioni hii kuchangia hoja mahususi, naomba kwanza niunge mkono hoja hii. Pili, naomba niishukuru Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kutimiza dhamira ya kuunganisha Mtwara na Mkoa wa Ruvuma kwa maana ya Mtwara Corridor kuhakikisha kipande kile cha Mbinga kwenda Nyasa kimeanza kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, naomba jambo hili haliwezi kukamilika kama hatutaweza kuzungumzia suala la reli ya kusini ambayo inaunganisha kati ya Mtwara na Mbambabay. Ukweli uzalishaji wa makaa ya mawe Ngaka, tunapozungumzia Mchuchuma na Liganga jambo hili haliwezi kwenda sawasawa bila kuzungumzia suala la reli ya kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali, nimeona kwenye maelezo ya Mheshimiwa Waziri lakini hayaleti matumaini kwa sababu wameendelea kutafuta wawekezaji wa reli hii lakini bado tunaona speed ya kuweza kuwekeza katika reli hii bado ni ndogo. Tunaomba, tunapofikiria suala la kujenga kiwanda cha Mchuchuma na Liganga iende sambamba na ujenzi wa reli ya kutoka Mtwara mpaka Mbambabay ili kusukuma maendeleo katika ukanda wa kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara zetu kwa sasa hivi kwa kweli zinaharibika sana, kwa mfano kuna malori makubwa sana yanayobeba makaa ya mawe kutoka Ngaka kwenda Dar es Salaam yanapita Songea – Tunduru –Lindi na kufika Dar es Salaam, lakini bado mengine yanapita Songea – Njombe mpaka Arusha. Jambo hili kidogo kama tungekuwa tuna reli basi barabara hizi zingeweza kudumu kwa muda mrefu, ukiona barabara ya Songea – Njombe ina hali mbaya sana, kama ni mgeni unaendesha barabara ile basi utegemee kupata ajali wakati wowote kwa sababu barabara ile ina hali mbaya, inatokana na kwamba inabeba mizigo mizito ya makaa ya mawe kutoka Ngaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, nilidhani katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri angeweza angalau kuingiza suala la ujenzi wa meli katika mwambao wa bahari. Kwa kweli barabara ya Mtwara – Lindi mpaka Dar es Salaam imeharibika sana; Dangote peke yake ana magari 600 ambayo kila siku yanabeba simenti kupeleka Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, solution ya jambo hili ilikuwa ni Serikali angalau kuweka msisitizo wa kuwa na meli ya mizigo kutoka Mtwara mpaka Dar es Salaam ambayo ingeweza kupunguza adha hii. Naomba Mheshimiwa Waziri aende kutoka Mtwara kuja Dar es Salaam ataona barabara ile jinsi ilivyoharibika kwa hali ya juu, kitu ambacho kingeweza kupunguzwa na usafirishaji wa simenti kwa kutumia meli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo naomba kulizungumzia ni suala la umeme vijijini. Naipongeza Serikali kwa jitihada kubwa inayoifanya. Pamoja na pongezi hizi, umeme vijijini una dosari kidogo; baadhi ya maeneo vijiji kwa kweli vina hali mbaya, umeme haujafika. Kwa mfano, kwenye Jimbo langu mpaka sasa nina vijiji vitano tu kati ya vijiji 65, kwenye awamu hii nilipewa vijiji 23 lakini mkandarasi bado hajaweza kufikisha hata vijiji nne, ukimuulizia ni suala la nguzo ambalo linasumbua. Jambo lingine ambalo linasumbua wanadai mkandarasi hajalipwa kwa muda mrefu anafanya kazi, invoice ime- raise lakini pesa bado hajalipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, suala la umeme kwenye Halmashauri ambayo ina majimbo mawili ina shida kidogo, utakuta Halmashauri hiyo hiyo mwenzako ana vijiji 20 wewe una vijiji viwili. Jambo hili watu wa REA wanavyopanga mipango yao ya kupeleka umeme vijijini basi waangalie maeneo ambayo yana Majimbo mawili, basi waangalie maeneo hayo wawe wanagawa vijiji kadiri inavyowezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, tunapiga kelele sana kwamba vijiji na vitongoji vyote vitakuwa na umeme lakini shida iliyokuwepo wakandarasi wanapewa scope ndogo sana, ukiangalia high tension inaenda kilometa 30 mpaka 40, katikati anavyopita kuna vitongoji ambavyo havijatajwa kwenye hiyo scope. Kwa hiyo, naomba sana kwa awamu ijayo basi waangalie scope wanayopewa wakandarasi kwa ajili ya kusambaza umeme katika vitongoji mbalimbali basi iongezwe angalau vile vitongoji vilivyo katika line ile viweze kupata umeme kama ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kuliongelea ni suala la kilimo, kama wenzangu walivyoongea, kilimo ni uti wa mgongo lakini kilimo kwa upande wa kusini (upande wa korosho) tunategemea sana mfumo wa stakabadhi ghalani. Mfumo wa stakabadhi ghalani hauwezi kufanyika bila maghala, kuna maghala ya Bodi ya Korosho yana muda mrefu sasa hivi ni mwaka wa tatu yalianza kujengwa lakini mpaka leo yale maghala hayajaweza kukamilika. Naomba Mheshimiwa Waziri aliangalie kwa jicho la huruma, tuna shida sana ya maghala katika maeneo yetu hasa upande wa Tunduru hatuna ghala la kudumu ambalo lina uwezo wa kuhifadhi korosho kwa wakati mmoja ili biashara ya mfumo wa stakabadhi ghalani iweze kufanyika kama inavyofanyika kwa sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la maghala hata ukiangalia kwenye vyama vya msingi kwa maana ya vijijini, maghala yao mengi ni mabovu, yanavuja, yanahatarisha usalama na ubora wa mazao hasa korosho pamoja na mazao mengine mpunga, mahindi, ufuta na kadhalika. Kwa hiyo, naomba sana bajeti ijayo iangalie namna ya kusaidia angalau ujenzi wa maghala katika vijiji mbalimbali ili kupunguza adha hii ambayo inawakumba wakulima wetu kukosa mahali pa kuhifadhi mazao yetu ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda nilizungumzie ni suala la maji; maji ni uhai. Kuna siku moja nilicheka kidogo, Mheshimiwa Diwani mmoja alisema hivi tusipooga wote hapa wiki nzima tutakuwaje?

Jambo hili ni zito sana kwa sababu vijijini maeneo mengi ukame umeathiri maji, maji yamekuwa ni tatizo. Naomba angalau tuweze kuhakikisha kwamba tunapata fedha nyingi zinazoweza kuchimba visima angalau kila kijiji kipate visima vitano ama vinne, tujinyime kwa maana ya aina yoyote ile kwa sababu bila maji maisha kwa kweli yanakuwa ni magumu kwa sababu wote tunaishi kwa kutegemea maji na magonjwa mengi yanapungua kama maji yatakuwepo ya uhakika na usalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana pamoja na Waziri anayehusika basi waliangalie suala la maji katika maeneo mbalimbali ya vijiji vyetu kutilia mkazo ili kuhakikisha kwamba angalau asilimia ile ya maji iongezeke ili wananchi waweze kupata maji salama ambayo ni ya uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo napenda nilizungumzie ni suala la TARURA. TARURA kwa kweli wana kazi kubwa lakini kazi yao inakwamishwa kwa sababu pesa wanayopewa ni kidogo ambayo haikidhi barabara ambazo tunazo/TARURA wanazimiliki. Ukichukulia mfano Wilaya ya Tunduru, ina kilometa 1,200 za barabara za vijijini ambazo zinamilikiwa na TARURA, lakini pesa wanayopewa inaweza kutengeneza kilometa 100 mpaka 200 tu, sasa sijui tutachukua miaka mingapi kuzipitia barabara hizi mpaka kumaliza maeneo yote. Kwa hiyo, naomba sana Serikali waangalie namna ambavyo wanaweza kuwaongezea pesa TARURA waweze kufanya kazi yao vizuri na waweze kuwahudumia wananchi kwa ajili ya kutengeneza barabara zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kabisa ni suala la afya. Naishukuru Serikali imefanya jambo jema la kuongeza vituo vya afya ambavyo vimeleta tija na matumaini kwa wananchi wetu. Jambo hili linaenda sambamba na idadi ya watumishi, mimi Jimboni kwangu tuna vituo vya afya viwili lakini kila kituo kina wafanyakazi sita/saba, jambo ambalo linakwamisha juhudi hizi za kujenga vituo vya afya vipya na vizuri na utoaji wa huduma haulingani na hadhi ya vituo vya afya ambavyo vipo kwa sasa. Kwa hiyo, naomba Serikali ifikirie suala la ajira la watumishi wa afya kuongeza ili kuhakikisha kwamba tunapunguza kero ya watumishi wa afya katika zahanati zetu, vituo vya afya pamoja na hospitali zetu za Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kabisa ni suala la watumishi upande wa elimu. Halmashauri yetu ya Wilaya ya Tunduru ina zaidi ya shule 157, ina upungufu wa Walimu zaidi ya asilimia 40 ambayo ni zaidi ya Walimu 600. Naomba Serikali iangalie namna pekee ya kuongeza idadi ya Walimu hasa kwenye shule za msingi na sekondari ili kuhakikisha kwamba watoto wetu wanapata elimu iliyo bora na ambayo inaweza kuwafanya waweze kuendelea vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuongea. Ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)