Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasoi ili niweze kuchangia mapendekezo pamoja na muongozo wa Mpango wetu wa Mwaka wa 2020/2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo ambayo tuanajadili kwenye kikao chako hiki ni mapendekezo ambayo yamepitia pia kwa wadau wengine na kupitia hatua mbalimbali hatimaye kuja kwenye Kamati ya bajeti lakini pia mwishoni yamekuja kwenye Bunge lako hili Tukufu ili pia Waheshimiwa Wabunge waweze kutoa mapendekezo yao ili kuboresha mapendekezo ya mpango wa maendeleo wa mwaka 2020/2021. Kwa hiyo, hapa tunajielekeza kwenye kuboresha mapendekezo haya na kupendekeza mambo mengine ambayo Waheshimiwa Wabunge wanadhani kwamba ni muhimu yakawemo ndani ya mpango wa maendeleo wa Mwaka unaokuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini cha pili ni mwongozo; tunaoujadili ni mwongozo huo wa mapendekezo na mwongozo unatoa tu muelekeo kwa namna gani Wizara, Taasisi na Mashirika ya umma, halmashauri zetu na watu wengine wa Serikali wanaongozwa katika kupanga, katika kubajeti, katika kutekeleza na kufuatilia na hatimaye kutoa taarifa kwa mipango watakayoitekeleza mwakani. Nilitaka nianze na huo ufafanuzi ili kwamba tuweze kuelewana tunapokwenda pamoja na Waheshimiwa Wabunge. Kwa hiyo, hapa hatujadili mpango wenyewe haujafika ni mapendekezo.

Mheshgimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumze mambo machache ambayo naamini na ni mawazo yangu. Mengine tumeyazungumza kwenye Kamati ya bajeti lakini mengine ni mawazo ambayo ninadhani pia ni muhimu kuyazungumza mbele ya Bunge lako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni changamoto ya mzao yetu ya kilimo; nakumbuka mwaka jana tulikuwa na changamoto ya masoko ya zao la korosho mpaka Mheshimiwa Rais aliingilia kati, Korosho zikaanza kununuliwa, zikanunuliwa lakini zikakaa muda mrefu bila kuuzwa nje ya nchi mahali ambapo tunauza kwa wingi ikiwa ghafi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna changamoto ya zao la pamba mwaka huu; mwaka huu pia tumepata changamoto hiyo kwasababu soko la pamba kwenye soko la Kimataifa lilianguka kwa hiyo bei ikawa ya chini lakini bado tunaishukuru Serikali kwasababu iliweka bei ambayo ingekuwa na faida kwa wakulima sasa kukatokea kutoelewana hapo kati ya wakulima pamoja na wanunuzi wa zao hilo la pamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna changamoto hapa kubwa ya masoko ya mzao yetu. Nilikuwa naomba kwamba katika mapendekezo ya mpango huu, hebu Serikali ijielekeze katika kutatua changamoto hii. Tunapozungumza bado kuna wakulima wa pamba hawajalipwa pamba yao kwenye maeneo mengi ya maeneo wanayolima pamba. Sasa tatizo ni soko la zao hilo sasa ni muhimu sasa Serikali ikachukua hatua tangu mapema kuhakikisha kwamba masoko ya mzao yetu ya kilimo yanatengenezwa mapema ili wakati wakulima wetu wanapovuna basi waweze kuuza mazao yao bila matatizo, bila shida, bila kurupushani na bila wao kuhangaika. Kwa hiyo, nilikuwa naomba sana tufanye hivyo na tutaboresha masoko ya mazao yetu hata hapa ndani ikiwa tutakubaliana na usemi wa Serikali ya Awamu ya Tano kwamba tuwe na viwanda vinavyochakata mazao yetu badala ya kuyauza yakiwa ghafi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna soko la bidhaa; soko hili lipo, limesajiliwa na lina watumishi lakini hatujaona likitumika sawa sawa. Kwa hiyo, nilikuwa naomba sana kwenye mapendekezo haya basi soko la bidhaa lionekane sasa linafanyakazi yake iliyopangwa kufanyika ya kuuza mazao yetu ya kilimo. Sasa inavyoonekana sasa hivi ni kama halijawa na uwezo mkubwa wa kufanya kazi hiyo sasa ni vizuri kwenye mapendekezo ya mpango huu, mapendekezo yangu ni kwamba lipewe uwezo wa kufanyakazi iliyopangiwa lifanye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nililotaka kuzungumzia ni mapato yetu hasa yale yanayokusanywa na TRA; tunaipongeza TRA kwa kuongeza mapato kutoka bilioni 800 Mwaka 2016 hadi trilioni 1.3 sasa trilioni 1.3 imeendelea hivyo kwa muda sasa wa miaka miwili tunakwenda mitatu haiongezeki zaidi ya hapo sasa ninachohisi ni kwamba inawezekana TRA wamefika mahali ambapo pengine hawawezi tena kwenda zaidi ya hapo lakini nakumbuka dhana ya uchumi wa viwanda. Kiwanda kikiwa kikubwa kikawa na malighafi nyingi, wafanyakazi wengi, mashine nyingi namna ya kukitawala inakuwa ngumu maana kunatokea kitu kinachoitwa diseconomies of scale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa inawezekana kwa TRA kitu kama hiki pia kimetokea sasa TRA ni kubwa. Sasa mapendekezo yangu ni kwamba, mapendekezo haya tunayojadili yatambue kwamba TRA ni kubwa na pengine inatakiwa sasa muundo wake utengenezwe upya kwa namna ya kuwa na Kanda badala ya kuwa na mikoa na wilaya kama ilivyo sasa hivi ili management ya TRA ya juu iweze kuwasiliana na watu wachache badala ya kuwasiliana na watu mikoa 26 na wilaya sijui 100 na ngapi, huyo mkuu wa TRA inamuwia vigumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, muundo wake ubadilishwe na utakapobadilishwa utawezesha hawa watu wa kwenye Kanda kuwafikia kwa urahisi watu wa Mkoani, watu wa Wilayani na hivyo kuongeza mapato ya Serikali au mapato yanayotokana na kodi vinginevyo itakuwa bado ni ngumu kwasababu TRA imekuwa ni kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uzoefu tulioupata mwezi wa tisa, mwezi wa juzi, TRA wamekusanya trilioni 1.740 sasa hiyo inawezekana ikawa ya kipindi tu, ikawa ni event, tusiporekebisha mambo kadhaa wa kadhaa lakini inawezekana kabisa makusanyo yetu kwa vyanzo tulivyonavyo hatujakusanya kiwango cha kutosha lakini ikiwa tutarekebisha muundo wake kwa viwango au kwa kodi zilizopo sasa hivi inawezekana tutakusanya kiwango kikubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ninalotaka kuzungumzia ni deni la Serikali; deni la Serikali limekuwa likiongezeka na nakublaiana na maelezo ya Mheshimiwa Waziri pia kwamba deni hili bado ni himilivu lakini Mwezi Agosti tumeambiwa denoi hili kuwa Trilioni 49, Mwezi Agosti mwaka huu lilikuwa trilioni 52 limeongezeka sasa ni himilivu kwasababu ya vigezo mbalimbali ambavyo Waheshimiwa Wabunge pia wanavifahamu humu ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nilichokuwa naomba kwenye mpango huu tunaoujadili, ni kwamba thamani ya shilingi yetu iendelee kuwa imara pia. Mpango uhakikishe thamani ya shilingi yetu inaendelea kuwa imara vinginevyo ikitikisika kidogo tu deni hili linaweza likaongezeka bila hata kuongeza kukopa ikiwa shilingi yetu itakuwa dhaifu dhidi ya sarafu ya nchi zingine hasa zile tunazofanyanazo biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa naomba sana kwenye mpango huu ambao tunaupendekeza, Serikali ihakikishe thamani ya shilingi yetu inakuwa imara, inaimarika dhidi ya Dola ili ya kwamba tusipate shida. Kuna usemi unaosema “wenzetu nchi zilizoendelea wakipata kikohozi sisi huku tunalazwa” maana yake ndiyo hiyo kwamba shilingi yao ikiimarika na ya kwetu ikawa dhaifu tunapata shida. Kwa hiyo, nilikuwa naomba kwmaba kwenye mpango huu tunaoujadili, Serikali ihakikishe shilingi yetu ni imara, imeimarika na kwmaba inakwenda vizuri dhidi ya sarafu zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa na hayo machache ya kusema jioni ya leo, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)