Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara ya Kilimo. Awali nimpongeze Mheshimiwa Waziri aliyepewa dhamana ya Wizara hii ameanza na mwanzo mzuri…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Naomba utulivu Bungeni.

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ameanza na mwanzo mzuri, naamini akisaidiana na wasaidizi wake watafanya kazi vizuri ya kuisimamia Serikali na Wizara kwa ujumla. Nianze kwa ushauri, Mkoa wa Katavi, Rukwa, Songwe, Mbeya, Iringa, Njombe na Ruvuma hii ni mikoa ambayo inazalisha chakula kwa wingi sana. Kazi ya Serikali ni kuwawezesha hawa wakulima wasikate tamaa. Mwaka jana wakulima wa mazao ya mahindi na mpunga wamekula hasara sana kutokana na Serikali kufunga mipaka na kuwazuia wakulima wasiuze mazao yao kwenye masoko ya nje. Nashauri hili kosa tulilolifanya tusije tukalirudia tena, wakulima wanazalisha mazao yao kwa nguvu zao binafsi na hawasaidiwi kitu chochote, muda unapofika mazao yao kuyauza Serikali inaleta vikwazo, tunawaletea umaskini sana. Tunalo soko la kongo, Rwanda na Burundi, sasa hivi maeneo yote hayo yana uhitaji wa kuhitaji mahindi na nafaka nyinginezo. Kwa hiyo nashauri kosa la kuzuia mazao haya lisifanyike tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba waweke mazingira wezeshi ili kusaidia mazao ambayo yanazalishwa kwa wingi hasa Nyanda za Juu Kusini yapate dirisha la kutokea eneo la Sumbawanga kwenye Bandari ya Kasanga ili yaweze kwenda nchi ya Congo. Nchi ya Congo mazao haya yanahitajika muda wote, wenzetu kule hawalimi kwa sababu ya vita vinavyotokea mara kwa mara. Kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri alifanyie kazi eneo hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ninaloshauri kwa Serikali ni kupeleka pembejeo kwa wakati. Mwaka huu uzalishaji wa mazao ya mahindi si mkubwa sana kwa sababu Serikali ilishindwa kupeleka pembejeo kwa wakati. Nimwombe Mheshimiwa Waziri aendelee kufanya utafiti na wawaachie Vyama vya Ushirika viweze kupeleka na kusambaza pembejeo kwa wakulima wake ili waweze kuzalisha kwa wakati. Kuingilia hizi pembejeo kwa Serikali tunaona tunafanya makosa makubwa, tunapeleka kipindi ambacho si cha uzalishaji. Niombe eneo hili wakalifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie mazao ya biashara. Jimboni kwangu tunazalisha, tumbaku, kahawa na pamba. Haya mazao ya biashara Serikali inatakiwa kwanza ikae na makampuni ili waweze kuangalia mazingira rafiki yatakayowezesha kusaidia ununuzi wa mazao haya. Zao la pamba ambalo limezalishwa Mpanda hasa katika Wilaya ya Tanganyika ni zao ambalo limepokelewa vizuri kwa wananchi na niipongeze Wizara ya Kilimo kupitia Bodi ya Pamba, wamewasaidia sana wakulima na takribani tuna matarajio ya kuzalisha karibu kilo milioni 16.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati mbaya sana bado hatujakuwa na uhakika wa soko la zao hili. Makampuni yanayonunua zao hili ni makampuni manne tu kiasi kwamba yanatia wasiwasi kwamba pamba iliyozalishwa Mkoa wa Katavi upo uwezekano ikakosa soko la uhakika. Tunaomba Waziri alifanyie kazi, asukume makampuni mengine yaweze kwenda kununua pamba katika eneo hilo na pamba inayozalishwa kule ni nzuri na walionunua kwa awamu ya kwanza wamesema ni pamba ya grade one ambayo imepatikana kwenye mnada wa kwanza uliofanyika kwenye eneo la Tanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie zao la tumbaku, zao hili ndilo lilikuwa linaongoza hapa nchini kwa kuleta fedha nyingi za kigeni na tulikuwa tuna uzalishaji mkubwa wa zaidi ya kilo milioni mia moja. Ni zao ambalo lilikuwa linaongoza kwa nchi yetu kuleta fedha nyingi za kigeni, lakini kwa sasa linaporomoka siku hadi siku, kutoka uzalishaji wa kilo milioni mia moja kwa sasa uzalishaji ni wa kilo milioni hamsini. Naomba Serikali iangalie uwezekano wa kunusuru hili zao. Kwanza wakae na makampuni ambayo yananunua zao la tumbaku, sasa hivi kuna tetesi kwamba kampuni la TLTC ambalo linanunua kwa kiwango kikubwa linaondoka hapa nchini kwa sababu ya mazingira kutokuwa rafiki kwao. Niishauri Serikali yangu wakae na haya makampuni zao la tumbaku ni zao ambalo linalimwa kwenye mikoa mingi katika nchi yetu, watafanya mdololo wa kiuchumi wasipofanya shughuli ya kufuatilia hili zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie miradi ya umwagiliaji, miradi mingi ya umwagiliaji Serikali imeitelekeza na karibu ambao waliopewa dhamana ya kuisimamia wameshindwa kabisa na wengi waliipiga hii miradi, niombe Serikali wafuatilie hii miradi. Ninao Mradi wa Skimu ya Karema, kunaMmradi wa Skim ya Mpailo na Mradi wa Skimu ya Kabage, bado hiyo miradi yote haijakamilika. Niombe Serikali hebu watumeni wataalam waangalie kifo cha fedha zilizotengwa na Serikali ambazo kimsingi mpaka sasa hazionekani kwamba zimefanya shughuli gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa suala la pembejeo, naomba utaratibu wa pembejeo ubadilike na tunaomba sana hasa kwenye suala la tumbaku, utaratibu uliozoeleka huko nyuma hebu waviachie Vyama vya Ushirika viweze kufanya kazi yake ili viweze kupeleka kwa wakati na ni jambo jema kwao wao. Serikali wanapowaachia vyombo vingine vinapofanya kazi hata wakifanya makosa Serikali itakuwa na nafasi ya kuelekeza mkono wake kwamba chombo hiki wakisimamie...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)