Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. ORAN M. NJEZA: Nashukuru sana Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kunipa nafasi na mimi ya kuchangia hii Wizara muhimu ya Kilimo. Ningependa kuanza kwa kutoa pole kwa wananchi waliopoteza maisha na majeruhi kutokana na ajali ya gari iliyotokea jana pale Mji Mdogo wa Mbalizi Wilaya ya Mbeya. Kwa kweli eneo lile limekuwa ni hatarishi sana, nafikiri Wizara ya Miundombinu pamoja na Mambo ya Ndani pamoja na juhudi wanazozifanya wangejaribu kuangalia namna ya kupunguza ajali katika eneo lile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuisema hiyo nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Hasunga, Naibu wake Mheshimiwa Mgumba, na Naibu wa pili Mheshimiwa Bashungwa; kwa kweli wanafanya kazi nzuri sana, ni timu nzuri timu ya wataalamu. Ukiangalia na hii hotuba yao ya bajeti kwa kweli imesheheni utaalamu mwingi unaoonesha matarajio mengi, na imekaa kimkakati mno. Kwahiyo inaonesha kabisa ya kwamba wataalamu watatu walikaa vizuri na wakaitengeneza hii hotuba yao vizuri. Mimi ningependa kuongezea kidogo tu katika hicho ambacho nao wametuletea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi nimezungumzia zao la pareto hapa na watu inawezekana wanashangaa hii pareto ni nini. Pareto Tanzania inaongoza Afrika, na sisi ni wa pili duniani. Kwa miaka mingi tulikuwa tunazalisha takriban tani zaidi ya elfu nane lakini leo hii tunazalisha chini ya tani 2000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilo moja ya pareto huko sokoni duniani ni dola kati ya 150 mpaka dola 300, kwa kilo moja; sasa angalia umuhimu wa hili zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tuna fursa za kuweza kuzalisha zaidi pareto. Sasa ningemuomba Mheshimiwa Waziri aliangalie kwa jicho la kipekee, ni namna gani atusaidie; kwa kuanzia usimamizi wa hili zao sio mzuri tuna Bodi ya pareto na siwezi kuwalaumu sana wataalamu inawezekana katika ule muundo sio mzuri sana. Kwasababu Mheshimiwa Waziri hapa amesema anajaribu kuangalia namna ya kuboresha ile sheria ya kilimo. Ile Bodi ya pareto kwa kweli haijatusaidia.

Mimi kama Mbunge wa Bunge la Mbeya Vijijini tunalima zaidi ya asilimia 85 ya pareto yote inayozalishwa Tanzania, lakini inavyoelekea katika wadau wa pareto Mbeya Vijijini haimo. Sasa ukianzia hapo tu utaona ya kwamba hili ni tatizo, ya kwamba hata wadau wenyewe hawajulikani. Bei ya pareto iliyooneshwa kwenye kitabu cha Waziri kwa kilo ni 3,700, wakulima wanalipwa shilingi 2,300. Sasa unajaribu kuangalia, hizi takwimu zinatoka wapi? Utakwenda kuwaambia nini wakulima? ya kwamba pareto yenu mnayolima mnalipwa shilingi 3,700 wastani ilhali zaidi zaidi wanalipa 2,300.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimesema kuwa kilo moja ya extract ambayo inatokana na kuichuja ile pareto, kilo moja inakwenda mpaka dola 300; na hata Kenya wenzetu wananunua kwetu kwa dola 70, India kwa dola 90 mpaka 100 na Korea vivyo hivyo. Sasa huyu mkulima unayemlipa 2300 inatoka wapi? Sasa je, kama nchi tunapoteza kiasi gani? Nilikuwa najaribu kuangalia hata ile Kampuni inayonunua pareto, nimegundua katika hisa mle kuna asilimia 15 ambazo ni za wakulima. Hizo asilimia 15 mpaka leo hatujui ni nani anayezifaidi. Asilimia 15 ya hisa ni nyingi. Kwa makusudi kabisa Serikali baada ya kubinafsisha hiki kiwanda ikasema wakulima nao wawe sehemu ya maamuzi ya hiki kiwanda, lakini mpaka leo hizo asilimia 15 hazieleweki nafikiri Waziri labda akiwa pamoja na TR waje watuambie hizo asilimia 15 ziko wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa vile vile niongelee na kwenye kahawa. Fursa tulizonazo kwenye kahawa bado ni kubwa, bei ya kahawa hapa kwetu ni ndogo. Leo hii sisi tunauza dola mbili kwa kilo, Kenya ni zaidi ya dola tatu, lakini ukiangalia kwenye soko la ICO kule paundi moja ni kama senti 144 ambazo ni dola 1.44 sasa hii tofauti yote inatoka wapi? Hii kahawa yetu ya arabika tunayolima Tanzania ni nzuri sana kwasababu ndiyo inayotumika kwenye blending kwenye kahawa nyingine kwa vile sisi tunachuma kwa mkono hizi kahawa, kwa hiyo ina heshima ya kipekee. Sasa hiyo hela tofauti hiyo inayopotea inaenda wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukienda zaidi kwenye masoko, hata ya mahindi. Nimemsikia msemaji hapa mama Anna Lupembe amezungumzia hoja ya muhimu sana kuhusu soko la mahindi la Kongo. Ni kweli tuna soko zuri Kongo, kuna rafiki zangu na ndugu zangu ambao wame-access hilo soko, lakini wamekuwa wakipitishia hiyo mizigo Zambia. Zambia sasa hivi wameweka masharti, lakini sisi tunapakana na Kongo. Sasa kwanini tusitumie njia ya Kongo na barabara za lami hizo zipo?

Sasa haya ndiyo mambo ambayo Wizara ikikaa mkakati kama walivyokuwa Mawaziri, tutumie brain zenu kuweza kuwaokoa wakulima tuachane na kufanyakazi kwa mazoea. Kama kuna timu zinawakwamisha huko angalia hizo timu zinazowakwamisha namna gani mzifumue sio wakati wake huu wa kuanza kulea watu ambao hawatusaidia katika kazi zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo napenda tu niunge mkono hoja nashukuru sana.