Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, awali ya yote naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa siku ya leo kuweza kupata fursa ya kuchangia. Pia nichukue fursa hii kuishukuru Serikali kwa kazi nzuri na kubwa na kwa nia ya dhati ya kuonesha kwamba, kutakuwa na mabadiliko katika sekta nzima ya kilimo. Nimshukuru Waziri, Manaibu Waziri, Katibu Mkuu na timu nzima ambayo iko Wizarani kwa kazi kubwa na nzuri na taasisi zote zilizoko chini yao kwa kazi kubwa wanayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku zote tunaendelea kushauri na ningeomba Wabunge wengi badala ya sehemu kubwa kutumia muda wetu kuelezea changamoto, changamoto kila mtu anazijua. Tuendelee kutoa ushauri mbalimbali ili kwenye dakika 10 kama dakika nane kila mtu atatoa ushauri, kwa Wabunge 300 angalau moja au mbili ikichukuliwa hapo tayari tutakuwa na mageuzi makubwa kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kwanza ningeendelea kuomba kwamba bajeti ya Serikali tuendelee kuiongeza. Najua wataalam wanaweza kusema kwamba bajeti hii kwa kilimo peke yake inajitosheleza kwa sababu bado kuna mengi huko kwa sababu ni mtambuka, bajeti inaenda kubwa yaani inaenda kwa Wizara nyingine nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kwa utafiti wangu binafsi, naweza kuwa nimekosea, nikiangalia bajeti ya mwaka jana na mwaka huu ya kilimo utaona imepanda kidogo lakini ukiirudisha (convert) kwenye bei ya USD bado imeteremka haijapanda. Lakini ukiichukulia kwa ujumla wake, kwamba trilioni 33, ukichukulia 10 percent yake ambayo ilikuwa ndiyo makubaliano kwamba iende kwenye kilimo, inatakiwa angalau kwenye trilioni tatu au zaidi. Hivi nikichukulia Wizara zote ambazo zinaenda vijijini ambako kilimo kwa sehemu kubwa kinapofanyika hiyo trilioni tatu sikuiona; yaani mimi nilivyojumlisha jumlisha tu sioni hiyo trilioni tatu. Kwa hiyo, bado bajeti ya kilimo inazidi kushuka na mchango wake katika Pato la Taifa bado nao unaendelea kushuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru kwamba sekta nyingine zinaendelea kukua, lakini asilimia kubwa ya Watanzania walipo ndipo huko kwenye Sekta ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, kwa ujumla tunasema kilimo; kwa hiyo ni vizuri tukaangalia namna ya kuboresha bajeti yake. Serikali isiangalie tu namna ya kuongeza bajeti kwa kupitia Serikali yenyewe, iweke mazingira wezeshi ili na sekta binafsi pia iweze kuchangia kwa sehemu kubwa na kama ilivyokuwa kwenye ASDP II, asilimia 65 inatakiwa fedha zitoke kwa sekta binafsi; lakini pasipokuwa na mazingira wezeshi, Serikali isipoweza kufanya kama timu moja, pakawa na uratibu, bado haya mambo yote hayatawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tusitegemee Wizara ya Kilimo, wanafanya kazi nzuri na wana mpango mzuri ila Wizara nyingine zote zisiposhirikiana bado tutaendelea kupata changamoto hiyo. Kwa hiyo, naomba mfanye kazi kama timu na wote mkae mezani mnapojadili kilimo basi kama ni kodi, tozo na ada mbalimbali mshirikiane namna ya kuzipunguza au kuziondoa. Huku kukiwa na tija huko kwingine utaendelea kupata kodi kwa njia nyingine ambayo ni indirect tax. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuomba; tunaendelea kutegemea umwagiliaji, bila umwagiliaji hatutaweza kusogeza kilimo mbele. Sasa kwenye umwagiliaji tulikuja hapa na wazo kubwa tukaanzisha sheria na ikaanzishwa Tume ya Umwagiliaji; lakini tangu imeanzishwa bado haijawahi kupewa fedha yoyote, yaani ni sifuri, kwenda kushughulika na umwagiliaji. Sasa nilikuwa naomba tuiwezeshe Tume ya Umwagiliaji ili kwenda kushughulika kwenye umwagiliaji. Sasa nilikuwa naomba tuiwezeshe Tume ya Umwagiliaji ili iweze kufanya kazi yake. Pamoja na hiyo ningeomba kwamba Benki ya Kilimo na Mfuko wa Pembejeo nao wawezeshwe vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ila kwenye hiyo pesa ambayo wamepata pawe na mkakati maalum, kwamba asilimia 20 ya fedha wanayopewa kukopeshwa kwenye sekta ya kilimo basi 20 iweze kutumika kwenye umwagiliaji tu, hapo pia utaiona sekta binafsi kwa sababu ni pesa ambayo watakopa watarudisha. Kwa hiyo, Benki ya Kilimo na Mfuko wa Pembejeo watenge asilimia 20 ambazo zitaenda kwenye umwagiliaji tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye umwagiliaji bado kuna changamoto nyingi. Kwa mfano ukitaka leo kuchimba visima, ukitaka kuleta mitambo ya kuchimba visima, kutengeneza mabwawa, solar pump za irrigation zote zina kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukishirikiana, kama Serikali mkikaa pamoja, ondoeni hizo kodi, wekeni mazingira wezeshi ili watu waweze kuchimba visima, kutengeneza mabwawa, na private sector itafanya. Kwa hiyo Serikali iweke tu mazingira mtaona kwenye kilimo jambo hilo la umwagiliaji litaendelea kukua. Pia mboreshe na kuandaa wataalam wa kutosha kwa upande wa umwagiliaji ili wao wakiweza kufanya kazi vizuri kwenye umwagiliaji ndiyo tutakuwa tunaweza kuokoa Watanzania badala ya kutegemea mvua, tuweze kufanya kilimo cha uhakika zaidi, na badala ya kufanya msimu mmoja, tufanye misimu miwili au mitatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nishukuru kwamba kuna wazo la kuwa na Sera na Sheria mpya ya Kilimo ambayo tunaamini itakuja kulinda ardhi za kilimo. Leo hii maeneo mengi ya kilimo yanachukuliwa kuwa makazi na kubadilishwa matumizi; na hayo sisi si kama wenzetu, uwezo wetu ni mdogo. Leo Mji wa Dodoma tu kila mahali itakuwa makazi, hii zabibu na mvinyo wa Dodoma utapotea. Vivyo hivyo, maeneo ya makazi yamechukua hayo maeneo ya kilimo. Kwa hiyo, sheria ije ya dhati, tunaweza kwenda kujenga milimani, tukajenga maeneo ambayo hakuna rutuba na ardhi ambayo siyo nzuri kwa uzalishaji, tukapeleka tu maji, barabara na nishati makazi yatakuwa mazuri, lakini maeneo ya kilimo yalindwe kwa dhati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukija pia kwenye sekta ya mbogamboga (horticultural) inafanya vizuri. Huko pia tulikuwa tunaomba cold storage ili wakulima waweze kuhifadhi mazao yao kabla ya kwenda kusafirisha, hasa kwenye maeneo ambayo Serikali itawekeza. Vilevile sekta binafsi iweze kuwekeza kwenye cold storage na kwenye mambo ya chillers pia muangalie namna ya kusaidia kupunguza na kuondoa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Upande wa Ushirika. Tulishakubaliana kwamba leo tunaweka nguvu kubwa kwenye shirika, na ndiyo njia pekee ya kwenda mbele kwenye kilimo. Kwenye ushirika bado ile Sheria ya 2013 tulipobadilisha kuliwa na dhana kwamba pale lazima tuhakikishe kwamba fedha ambayo ushirika itakuwa inachukua hakutakuwa na makato ya wakulima, tulisema ushirika kazi yao ni kuhudumia wanachama wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wanapotafuta masoko, wanapoleta pembejeo tofauti ya kwenye bei na nini wanaponunua kwa wingi ile tofauti ya bei ndiyo iwe inaendesha ushirika. Ushirika usimkate mkulima hata shilingi moja, ndiyo maana wakulima hawapendi kupeleka mazao yao kwenye ushirika. watu wapendelee kwenda kwenye ushirika badala ya kukwepa kwenda kwenye ushirika. Kwa hiyo, ni jambo ambalo naamini tukikaa tukaelezea vizuri, tutafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, luna jambo linguine. Leo hii tunaagiza vitu vitano; mbegu, asilimia kubwa ya mbegu zetu hasa mahindi, asilimia 65 ya mbegu inatoka nje ya nchi, usalama wa chakula na mbegu haupo. Kwenye mbegu kuna alizeti na mbegu hizi ambazo zinazalisha mafuta, tunaangiza sisi, baada ya mafuta ya magari mafuta haya ya kula ndiyo sehemu kubwa ya fedha yetu inakotumika. Kwa hiyo mbegu, sukari, mafuta, mchele, mbogamboga, matunda na hivi vyote ambavyo tunaagiza kutoka nje tuwekeza. Muwe na timeframe, kwamba ndani ya miaka mitatu hakuna kitu kitakachoagizwa nje, tutazalisha ndani ya nchi na sisi ndio tutapeleka nchi nyingine. Hayo yanashindikana kutokana na mazingira wezeshi kwenye sekta hii ya kilimo na Wizara zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie mfano, juice zote tunazokunywa hapa Tanzania asilimia 99.5 ni concentrates kutoka nje, ni asilimia 0.5 ndiyo inazalishwa hapa nchini, kwa nini? Tukizalisha hapa nchini kwanza tutapata lishe bora, fedha kwenye uchumi wetu na tutapata mazingira bora kwa ajili ya miti hiyo mingi. Kwa hiyo itakuwa na trickling effect kwenye Wizara nyingine zote. Kwa hiyo, naomba tuifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ni muhimu ni kwamba bajeti ya TARI ni ndogo sana, na tunapanga wakati mwingine tunaweza kupitisha hapa lakini fedha zinazokwenda ni ndogo. Bila utafiti kwenye kilimo hakuna uwezekano kwa kwenda popote kwa sababu kilimo ni sayansi, kilimo ni biashara kama biashara yoyote nyingine. Wekezeni kwenye TARI ili vituo vya utafiti vizalishe mbegu, viangalie namna ya kudhibiti magonjwa lakini pia tuangalia namna ya kuboresha ASA. ASA ina mashamba mazuri sana, wanahitaji uwekezaji wa kwenye umwagiliaji na uwekezaji kwenye zana za kilimo (matrekta na zana zake). Mkiwawezesha wale wala siyo kwa kuwapa bajeti, wakopesheni wataweza kulipa kwa sababu wanafanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia TPRI na…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JITU V. SONI: Ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)