Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa na mimi kuweza kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa mimi naunga mkono hoja na nataka nitamke mapema kabisa kwamba kama kuna taasisi hapa nchini yenye rekodi ndefu iliyotukuka ya nidhamu, maadili, weledi na utendaji wa hali ya juu basi taasisi hiyo ni Jeshi letu la Wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dalili za Jeshi kuwa mfano bora wa kuigwa nchini ilijitokeza mapema tu baada ya uhuru, wakati wa uhuru ambapo Baba wa Taifa alimkabidhi Luteni Alexander Ngwebe Nyirenda, bendera na mwenge wa uhuru akauweke juu ya Mlima Kilimanjaro, kitendo ambacho Baba wa Taifa alikielezea kishairi shairi kwamba mwenge huo utamulika ndani nan je ya mipaka yetu ili ulete matumaini pale ambapo hakuna matumaini, ulete upendo mahali penye chuki na heshima mahali palipo na dharau na kwa hakika mwenge ulitusaidia kuona mapema kabisa baada ya uhuru kwamba kuna dhuluma ndani ya Bara la Afrika na ndiyo maana Tanzania tukawa ngome kuu ya mapambano ya harakati za kupigania uhuru katika Bara la Afrika na ndiyo maana mwaka 1963 nchi yetu ikapewa heshima kuwa ndiyo Makao Makuu ya Kamati ya ukombozi wa Bara la Afrika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile mwaka 2011 nchi yetu ikapewa heshima kubwa kuwa ndiyo Kituo Kikuu cha Kumbukumbu ya Historia ya Harakati za Ukombozi wa Bara la Afrika na ukiongelea harakati za ukombozi kwa kweli tunapata hiyo heshima kutokana na Jeshi letu la Wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nduli Iddi Amin alipojaribu kuleta jeuri hiyo jeuri ilizimwa na majeshi yetu, tunawapongeza sana. Na kwenye vurugu popote pale duniani vijana wetu wakienda wanaacha alama ya heshima na ndiyo maana leo hii ukienda Kinshasa, Lubumbashi unatembea kifua mbele kama Mtanzania kutokana na kazi kubwa ambayo akina Jenerali Mwakibolwa waliifanya hao wote ndiyo JWTZ. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu kwa kusema nalipongeza sana Jeshi letu hasa kwa upande wa michezo. Hawajaanza jana hawa. Akina Filbert Bayi wakiwa jeshini ndiyo Mtanzania wa kwanza kutuletea sifa hapa mwaka 1974 baada ya kuvunja rekodi ya dunia ya mita 1,300 Christchurch – New Zealand, hiyo JWTZ. Sio huyo tu, tunae mweznake Juma Ikangaa mwanajeshi mwenzake ambaye alikuw abingwa wa mbio za New York za marathon mwaka 1988, JWTZ hiyo, sio huyo tu, tuna Samson Ramadhan, mshindi wa marathon Melbourne – Australia mwaka 2006 ni JWTZ.

Mheshimiwa Mwenyekiti, orodha ni ndefu sana, nisimsahau kijana wetu Simbu, mshindi wa medali ya dhahabu Mumbai Marathon na vilevile medali ya shaba London Marathon…

MWENYEKITI: Ikangaa.

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO:Mheshimiwa Mwenyekiti, Ikangaa nimemtaja ndiye mshindi wa marathon ya New York, kuna wengi. Tuna akina Cecilia Panga bingwa wa Beijing International Marathon, Emmanuel Gisamoda, Shanghai International Marathon. Kwa kweli jeshi letu limetupa heshima kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naona muda wangu umekwisha, naomba tu niseme naunga mkono hoja na kwakweli Jeshi letu linastahili heshima kutoka kwa kila Mtanzania. Ahsante sana. (Makofi)