Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Angelina Adam Malembeka

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kwenye Wizara hii. Kwanza namshukuru Mwenyenzi Mungu kwa kuniamsha salama. Nitoe pongezi kwa Amiri Jeshi Mkuu, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Joseph Pombe Magufuli kwa kuiongoza nchi yetu vizuri na kazi nzuri anazo zifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nichukue fursa hii kumpongeza Waziri mwenye dhamana kwa kazi nzuri, zenye tija zinazoendelea kufanywa kwenye Wizara yake, pongezi hizi pia ziende pia sambamba kwa makamanda na Maafande wote nchi bila kuwasahau watendaji wao katika nafasi zao. Kipekee napenda kuwapongeza vijana wote wanaojitolea katika Jeshi la Kujenga Taifa tunawatambua, tunathamini mchango wao na tunawajali sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania nasema ni salama na usalama huu unatokana baina ushirikiano baina ya Wizara hii, Wizara nyingine pamoja na wananchi na pia niwakumbushe wananchi kwamba usalama wa nchi ni jukumu letu sote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tunao vijana wengi ambao bado hawajapa ajira japo wamekuwa wakijitolea katika vituo vya JKT hapa nchini. Ninaomba Serikali iangalie upya jinsi gani wataweze kuwa ajiri vijana hao. Lakini pia nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais ambaye
aliweza kuruhusu ajira zitolewe kwa vijana waliojenga ukuta wa Marerani na waliojenga Mji wa Seriakali hapa Dodoma. Lakini Waziri atakapokuja atuambie Wizara yake imejipangaje kwa ajili ya kutoa ajira kwa vijana hao badala ya kusubiri matamko ya Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze pia SUMA JKT kwa kazi nzuri wanazifanya. Wamekuwa wakifanya kazi nzuri na zenye uhakika na gharama naafuu naomba tuenelee kuwaamini na kuwapa kazi ambazo zinaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi letu limekuwa na ushirikiano mzuri na majeshi mengine katika nchi nyingine katika masuala ya ulinzi na amani na usalama kwa ujumla wake, katika kuboresha maslahi ya watendaji katika vyombo vya ulinzi na usalama ningependa kujua kwa jumla Mheshimiwa Waziri wiki nzima hii tumekuwa na clip au taarifa ambazo zinatembea kwenye mitandao zikionesha baadhi ya Watanzania na wananchi wa nchi jirani ambao wanasema kwamba wamepigwa Afrika Kusini au wamechomwa moto. Sasa Waziri angetuambia taarifa hizi ni za kweli au ni mitandao tu na kama ni kweli Waziri anatueleza nini kuhusiana na hilo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa suala la ulinzi na usalama limo katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2025 na pia limo katika Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa miaka mitano, 2016/2017 mpaka 2020/2021 na utekelezaji wa majukumu mengine katika Wizara hii, mimi naomba niwashawishi Wabunge wenzangu tukubali na kuipitisha bajeti ya Wizara hii ili waweze kuweka mazingira mazuri ya JKT na kuimarisha mafunzo ya vijana, pia kushirikiana na Umoja wa Mataifa (UN) na Umoja wa Afrika katika shughuli za ulinzi na amani. Pia waweze kushirikiana na mataifa mengine katika kupambana na uhalifu unaovuka mipaka ikiwepo ugaidi, uharamia na biashara haramu ya madawa ya kulevya. Lakini pia kuviwezesha vyombo vya ulinzi na usalama kuviongezea rasilimaliwatu na fedha ili waweze kufanya kazi zao vizuri. Sambamba na hilo kufanya tafiti mbalimbali zenye maslahi kwa wanajeshi na raia kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuunga mkono maombi ya bajeti kwa ajili ya Wizara hii, ninaomba Waziri atakapokuja kuhitimisha hoja yake atueleze ni lini Serikali italipa fidia au kurejesha maeneo ambayo wanajeshi walichukua kutoka kwa raia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi pia limeweza kuwekeza katika maeneo mbalimbali, lakini katika uwekezaji wake ni vizuri aje atueleze ni utaratibu gani unaotumika unaotumika katika uwekezaji unaofanywa na Jeshi bila kuzingatia mipango miji na haiba ya mji. Nikitolea mfano Jimbo la Welezo eneo la Jeshi kuna biashara pale za gereji, za kuuza miti, kuuza vyakula, kuosha magari wote katika eneo moja. Naomba Mheshimiwa Waziri akija atueleze vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo jeshi limekuwa na kumbi mbalimbali za burudani, nilitegemea kumbi zile zitatumika zaidi na wanajeshi. Sasa hivi kumbi zile zimekuwa zinaingiliwa na raia wa kawaida pamoja na wanajeshi na katika burudani zile mara nyingi ugomvi unatokea na ugomvi huo mara nyingi unahusishwa na pombe pamoja na wanawake na katika vita hivyo siku zote wanaopigwa ni raia wanajeshi wanakuwa ndio washindi. Sasa tunataka watuambie ni lini au ana tamko gani kuhusiana na maeneo hayo ya burudani ili wananchi wetu wasiendelee kupigwa, aidha kutokana na masuala ya pombe au masuala ya mapenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze pia vituo vya afya vinavyioendeshwa na Jeshi nikitolea mfano Kituo cha Bububu - Zanzibar, Kituo cha Welezo - Zanzibar, Lugalo - Dar es Salaam pamoja na vituo vingine. Vituo hivi vimekuwa vinafanya kazi nzuri sana na wananchi wanapenda sana kwenda kutibiwa pale kwa sababu kwenye vituo vile wanajali sana wagonjwa, wanatoa huduma nzuri na wana upendo wa dhati, lakini tatizo kubwa pale ni bajeti finyu, wanakuwa na bajeti ndogo ambayo wanashindwa kuwa na dawa za kutosha japo wanatoa huduma nzuri. Ni vizuri basi Serikali waviangalie vituo hivi kwa jicho la huruma ili wananchji waendelee kupata huduma na nikiamini kwamba Jeshi liotaendelea kuisaidia Serikali katika kutoa huduma kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze tena wanajeshi wetu wote kwa kazi nzuri za ulinzi na usalama zinazofanyika hapa nchini. Maneno madogo madogo yapo, lakini hayo Jeshi wakiamua kunyamaza humu ndani hakukaliki tusidanganyane. Jeshi linafanya kazi nzuri sana na katika 100 mtu akikosea 10 akapata 90 maana yake ndio kashinda kafanya vizuri. Lakini kipekee niwapongeze...

MWENYEKITI: Ahsante.