Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na mpaka siku ya leo tupo hapa. Kwa namna ya pekee napenda pia nitoe shukrani za dhati kwa Mheshimiwa wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Viongozi wote Wakuu wanaomsaidia kwa kuwa na imani nasi na hivyo kuendelea kutuamini katika kuongoza Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote ambao wameweza kuchangia katika hii bajeti yetu kwa azma ya kuifanya Wizara yetu iweze kutekeleza majukumu yake vizuri na pia kuzisaidia sekta ambazo zinapewa huduma na Wizara yetu ya Viwanda na Biashara; na hivyo chini ya uongozi madhubuti wa Waziri wetu Mheshimiwa Joseph Kakunda tunawaahidi kwamba michango yote ambayo imetolewa, yenye tija na nia ya kuisaidia nchi yetu, tunaichukulia kwa umakini mkubwa kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi michango imetolewa katika sura mbalimbali; na unapopewa ushauri lazima utafakari, ushauri huu unapewa na nani? Napewa kwa sababu gani na una malengo yapi? Una manufaa gani? Kwa hiyo, tumeweza kuchambua ushauri karibu wote ambao umetolewa na tumeona asilimia kubwa ya ushauri huu ni mzuri na unalenga kujenga na kuimarisha nchi yetu. Kwa hiyo, tuko pamoja na tutafanyia kazi kadiri inavyowezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi Wizara ya viwanda na Biashara kwa kushirikiana na Wizara nyingine imejizatiti katika kuhakikisha Tanzania inakuwa na viwanda na biashara endelevu zinazoakisi rasilimali nyingi ambazo zipo Tanzania; na Tanzania kwa kweli wote tunafahamu imejaliwa rasilimali nyingi sana. Ni dhahiri kuwa sekta binafsi iliyo imara ndiyo itakayowezesha kuchakata na kuongeza dhamani ya rasilimali hizi, halikadhalika kuzitumia bidhaa hizo na ziada yake kwenda kuziuza ndani na nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa misingi hiyo, tunategemea kwamba kwa kuwa na sekta binafsi ambayo inaweza kuhimili ushindani, ndipo tutakapoweza kupata manufaa makubwa ya rasilimali zetu. Niseme tu kwamba ni ukweli usiopingika, pamoja na jitihada kubwa ambayo Serikali imefanya katika kuimarisha shughuli za sekta binafsi nchini ambayo ndiyo chimbuko na chanzo cha mapato ya nchi, kwa sababu hata tukisema kwamba mfanyakazi analipa kodi, lakini chimbuko la fedha ni pale inapokuwa imetengenezwa kupitia viwanda au hao hao wafanyabiashara ndio hao sasa kodi zao zinawalipa watumishi fedha na hizo fedha nazo zinarudi tena kuchangia katika mfumo wa kikodi. Kwa hiyo, sekta hii ni muhimu sana. Kimsingi ndiyo moyo wa nchi katika kulifanya Taifa letu liweze kuwa imara na liweze kuchakata hizi mali nyingi tulizojaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, tunakubali kabisa zipo changamoto ambazo bado zinawakabili wanaviwanda wetu na wajasiriamali au wafanyabiashara kwa ujumla. Kwa kutambua hilo, ndiyo maana Serikali baada ya kukaa na wadau mbalimbali, iliona iko haja ya kusema kwamba sasa tufikie mwisho tutambue, tuainishe changamoto hizi na tuzifanyie kazi. Kwa sababu hizo changamoto zimekuwa karibu katika kila sekta, kwa sababu wafanyabiashara au wachakataji wako katika kila sekta, ilibidi lazima tuangalie kila Wizara, kila mdau ni namna gani anapata tatizo au changamoto kupitia mazingira na mfumo uliopo sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa misingi hiyo, tulikaa tukatengeneza hii Blue Print, yawezekana wengine kati yetu bado hawajaiona, lakini wengine wameshaona. Kwa hiyo, niseme tu kwamba Wizara itajitahidi kusambaza kwa wadau wengi zaidi ili tuweze kuona nini lilichopo kwenye Blue Print. Hilo andiko ni hili hapa, lina kurasa nyingi ambalo linataja kila sekta. Kimsingi mambo mengi yaliyokuwa yanachangiwa humu ndani kama changamoto, tayari yalishaainishwa humu, lakini kutokana na teknolojia na namna ambavyo tunaendelea kupata ushindani na hali ya kimfumo wa kibiashara, tunaamini kwamba bado Blue Print haitakuwa ni mwarobaini, bali itakuwa ni kazi endelevu ya kuendelea kuiboresha kwa kadri ambavyo changamoto zinavyojitokeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hiyo iko katika maeneo ya ngozi, tumesikia hapo, pia iko katika maeneo ya taasisi za udhibiti kama OSHA, Workers Compensation Fund na taasisi nyingine kama TFDA, wote kila mmoja amechambuliwa humu. Hali tuliyofikia sasa ni kuhakikisha kwamba tunatengeneza mpango mkakati wa utekelezaji, nini kifanyike wakati gani na watu gani washiriki?

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunayo furaha kuliarifu Bunge letu Tukufu kwamba tayari kuna wadau wameshajitokeza wenye nia ya kusaidia utekelezaji wa mpango huu wa Blue Print. Kwa hiyo, naamini kwa dhamira na nia njema ya Serikali, huo upungufu au changamoto zilizojitokeza zitafanyiwa kazi na tunaahidi kufikia mwezi wa Saba tayari huo mpango mkakati wa utekelezaji utakuwa tayari na hivyo Blue Print kuanza kufanyiwa kazi na zile sheria ambazo zinazoonekana kuwa ni za kikwazo, zitaletwa humu Bungeni ili ziweze kufanyiwa kazi. Tunaamini kwamba, baada ya kuanza kufanyia kazi hii Blue Print hatutegemei tena kwamba sisi wenyewe tutaendelea kutunga zile sheria au kanuni kinzani zitakazokwenda tena kinyume na hii Blue Print. Kwa misingi hiyo, labda kutakuwa na kamati maalum ambayo itaweza kuangalia ni nini kinaletwa Bungeni ili kisitengeneze tena tatizo juu ya tatizo kwa nia njema na dhamira ambayo tayari nchi imeshaiweka.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kuhusu hoja pia iliyotolewa na Waheshimiwa Kambi ya Upinzani kuhusu korosho. Niseme tu kwamba kwanza hoja hiyo sisi tumeipokea na tumeiona ni nzuri kwa sababu inatusaidia kufafanua zaidi kwa wananchi nini kilichotokea katika suala la korosho. Korosho kama wote tunavyofahamu, ni zao muhimu na linawasaidia wananchi wengi hususan katika Mkoa wa Mtwara, Lindi, Ruvuma, Tanga na mikoa mingine ambayo sasa hivi inajizatiti katika kilimo cha korosho.

Mheshimiwa Naibu Spika, bei ambayo ilikuwa inatolewa na wanunuzi wa korosho kwa kipindi cha nyuma ilikuwa ni mbaya sana. Kwa mtu yeyote mwenye nia njema na nchi yake, mwenye nia njema na wakulima, kwa vyovyote vile hawezi kukubali kuona hali kama hiyo iendelee.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa misingi hiyo, tunao wajibu na heshima kumpa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ambaye hakuiangalia tu faida ya kupata hiyo hela ndogo wanayoileta wafanyabiashara kwa gharama ya kuwatesa wakulima kwa ile bei ndogo, ndipo aliposema kama nchi ibebe huo mzigo. Tukaona kwamba korosho zinunuliwe kwa shilingi 3,300/=.

Mheshimiwa Naibu Spika, hayo ni maamuzi makubwa sana ambayo katika nchi yetu nasema kwamba kwa upande wa wakulima pengine haijawahi kutokea. Kwa hiyo, kwa maamuzi hayo, yamefanya kwamba ule mzigo ambao wangeubeba wakulima urudi sasa kwa Serikali ambayo ina vyanzo vingi vya mapato ukilinganisha na huyu mkulima. Kwa hiyo, sisi tunaendelea na niwapongeza sana Wizara ya Kilimo ambao tayari wameshalipa sehemu kubwa ya fedha na hiyo nyingine tunaamini itaendelea kulipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kampuni ya INDO Power ambayo ilikuwa inunue korosho, jamani kampuni ile nashangaa tunaizungumza sana. Yule ni mdau ambaye alitaka kununua korosho sawa na wadau wengine wowote. Mnapokuwa na makubaliano kwamba nataka labda nichukuwe mali yako hii, tuchukulie kama ingekuwa ni nguo dukani kwako, tunapeana muda; kufikiana muda fulani utakuwa umetekeleza, umelipa. Kama hajalipa, sisi tunamchukulia ni sawa na mfanyabiashara mwingine yeyote ambaye alikuwa hana uwezo, hatuwezi kuendelea kuitunza korosho eti tunamwekea mtu ambaye hana uwezo wa kulipa kwa wakati huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ingekuwa imepata hasara kama tungekuwa tumechukua hizo korosho tukampa yeye, halafu tukamwambia baada ya muda utatulipa. Tulikuwa hatujampa, tulichukuwa precautions zote na hayo ndiyo mambo makubwa aliyofanya Mheshimwia Prof. Kabudi, kuhakikisha kwamba mambo yote ya msingi kwa kushirikiana na Wizara yetu na wadau wote muhimu tunayalinda. Kwa hiyo, hata kama akiwa amepata fedha sasa, anataka kuja kununua, kama hatujamaliza kuuza, sisi tutampa tu, lakini kama hajafika, tunaendelea na wanunuzi wengine. Kwa hiyo, Serikali au nchi haijapata hasara. Sisi tumefanya biashara zetu kwa umakini tukizingatia kwamba hakuna hata senti tano au mali ya Tanzania inayoweza kuliwa na mtu mjanja mjanja, hilo hatukubali.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nichukue nafasi hii kuwashawishi lakini pia kuwaonya, sisi wenyewe Watanzania tunapokuwa na jambo zito kama hili, siyo suala la kufanya la mzaha mzaha, tunapochukua maamuzi mazito, siyo masuala ya kimzaha mzaha, ni masuala ambayo yanagusa mustakabali wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wengine unaweza kukuta wanazunguka zunguka tena wanamfuata mnunuzi, anamwambia unajua hapa bwana, ungefanya hivi, ufanye hivi. Wewe ni Mtanzania? Kwa nini ufanye hivyo? Kwa faida ya nani? Nilitegemea wote tutashirikiana, tutaungana na tena hasa kwa Wabunge wanatoka Mkoa wa Mtwara na Lindi na Ruvuma kwa sababu waadhirika wakubwa walikuwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme tu kwamba Serikali inaendelea na mikakati, korosho ambayo ilitakiwa kubanguliwa kwa muda mrefu ilikuwa viwanda vingine vimefungwa, havibagui korosho, sasa hivi tunabangua, tumefungasha tunazo katoni zaidi ya 17,427 tayari kwa kuuza na zimekuwa-tested, zipo katika hali nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hiyo korosho ambayo bado haijabanguliwa, tumei-test katika maabara yetu ya Tanzania, lakini na maabara nyingine za nje zimedhibitishwa kuwa na ubora wa kiwango cha juu. Kwa hiyo, bado tuko katika hali nzuri. Anayetaka kuja kununua kwa tija, karibu; anayetaka kuja kununua kwa kutuibia au kutufanya sisi manamba, kwaheri. Tanzania siyo jalala, Tanzania ni nchi inayojitambua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala lingine ambalo limejitokeza kuhusiana na bajeti ya Wizara yetu kuwa ni ndogo. Kwanza niseme kwamba tunapokea kwa kiasi fulani concern za Waheshimiwa Wabunge. Kama ambavyo inaeleweka kwamba kupanga ni kuchagua, nasi Wizara yetu kimsingi ni Wizara ambayo ni coordinator, yaani inashawishi Wizara nyingine ziweze kuweka miundombinu rafiki kwa ajili ya hawa wazalishaji wetu na wafanyabiashara kwa ujumla. Ndiyo maana bajeti nyingine unaona haziji moja kwa moja kwenye Wizara yetu, zinajitokeza katika Wizara nyingine. Mfano mzuri ni kama ambavyo ilielezwa hapo awali na Mheshimiwa Mollel kuhusiana na ujenzi wa umeme, Stiegler’s Gorge kuhusiana na mradi mkakati wa SGR. Nyie mnakumbuka, reli hii ya kati ni ya toka mwaka 1905, mpaka leo ilikuwa haijakarabatiwa kadri ya kiwango kinachohitajika kuweza kubeba mzigo unaostahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, tunazo meli kama Liemba ya mwaka huo huo 1905, lakini mpaka leo haijaweza kupata huo ufadhili. Huyo mjomba tunayemsubiri kila siku atufanyie kazi, yuko wapi? Hayupo. Lazima tujifunge mikanda. Katika kujifunga mikanda, kuna maeneo yatakuwa yanaathirika kwa muda, kwa sababu nguvu zote zinakuwa zimeelekezwa huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, Serikali kimsingi inasikiliza ushauri wa Waheshimiwa Wabunge. Naamini michango iliyotolewa haiwezi ikaishia hewani tu, lazima Serikali itafanya kitu katika kuangalia maeneo yale yenye umuhimu na ambayo yanakusudiwa kwa ajili ya kuleta tija kwa haraka ikiwemo na maeneo ya miradi mikubwa ya kimkakati yatazidi kuangaliwa na kutengewa fedha inayotakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi niseme tu kwamba dhamira iliyopo ya Serikali ni kubwa sana katika kuhakikisha kwamba tunajitoa katika wimbi hili la kuitwa sisi ni masikini Tanzania wakati tuna rasilimali nyingi nyingi, nyingi. Hapana, muda umefika wa sisi kufanya maamuzi ya liyo sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu baadhi ya viwanda ambavyo havifanyi vizuri kutokana na bidhaa mbalimbali ambazo zinaingizwa kutoka nchi za nje. Kweli suala hilo tunalitafakari, lakini unakuta katika baadhi ya viwanda vyenyewe vinatumia rasilimali (raw materials) kutoka nje. Pia tunataka tujiridhishe hivi viwanda vyetu ambavyo tunasema havina uwezo wa kushindana katika hali iliyopo, kule wanapochukuwa malighafi, wanapata kwa bei halali au pengine kuna mazingira ya urafiki yanayofanya pengine huko wanapochukulia mali ghafi yaongezwe bei kiasi kwamba inapofika hapa hizo mali ghafi zisiweze kuzalisasha kwa tija? Kwa hiyo, tutaangalia pande zote mbili, kwa sababu sisi tusingependa kuishi kama nchi ambayo inajiangalia tu yenyewe bila kuwa na washindani wengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba viwanda vya ndani vinalindwa. Kwa misingi hiyo niseme tu kwamba Wizara tumejizatiti, tumejipanga, kuhakikisha kwamba viwanda vyetu vya ndani vinapewa msaada unaohitajika ikiwemo kupunguziwa kodi katika bidhaa maalum au pengine kupewa msamaha au ruzuku katika baadhi ya malighafi na vile vile kuweza kuweka tozo zaidi kwa bidhaa ambazo zinatoka nje ya nchi wakati kuna utoshelezi ndani ya nchi. Tumefanya hiyo katika maeneo mengine. Kwa mfano, cement sasa hivi hatuagizi kutoka nje, tunajitosheleza. Hizo nondo, tumo katika mkakati huo na kwa kweli sasa hivi Tanzania inafanya vizuri sana katika viwanda vyake. Ni vile tu kwamba tulizoea kuviona baadhi ya viwanda vilivyokuwa vinajionesha vyenyewe ndiyo vyenye nguvu, tukavidharau vile vingine vidogo vidogo ambavyo vinaanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, wapo wawekezaji ambao wako tayari, akina Kilua Integrated Group wako hapo, ni Watanzania. Sio hao tu, tunao wengi ambao wanakuja. Vile vile tumefanikisha kuvutia viwanda vingi ambavyo sasa vimeanzishwa nchini, mfano kiwanda cha Cassava (starch), yaani wanga wa unga wa mihogo ambacho kiko kule Lindi. Juzi juzi hapa Mheshimiwa Rais amezindua tena Kiwanda cha Unga pale Mlale, Kiwanda cha Maparachichi pale Rungwe, Tukuyu na vile vile tumeona hata Unilever pale Njombe; na viwanda vingi vinaendelea kufunguliwa. Tatito labda hatujapata fursa ya kutembelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba sana Watanzania tupende bidhaa zetu za Tanzania, tupende kutumia bidhaa zetu na tujivunie, vile vile kwa wafanyabiashara na wajasiriamali wote kwa ujumla. Sasa hivi kitambulisho cha ujasiliamali kimeshushwa ni shilingi 20,000/= tu, huhitaji hata sasa utengeneze mahesabu, sijui ufanye nini; kwa mtu mwenye mtaji wa chini ya shilingi milioni nne, huyu akishakuwa na kitambulisho chake cha shilingi 20,000/= tu cha ujasiliamali, habughudhiwi, anaendelea na shughuli zake popote pale. Hayo ndiyo mambo ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli katika kuwasaidia wanyonge.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba katika masuala haya ya undelezaji wa biashara, hayawezi kufanyika na mtu mmoja. Hata sisi wenyewe tuwe na positive thinking, tuwe na hali ya kusemea vizuri nchi yetu. Ukishaulizwa swali tu, eh mazingira ya biashara nchini kwako yakoje? Unaanza; unajua tuna taabu nyingi sana, unajua kuna OSHA, kuna nini. Sasa unajiuza hasi wewe mwenyewe, ukishajiuza hasi na yule anayeandika atasema mazingira yako ni magumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani changamoto iliyopo siyo tozo tu, ni kuweka mazingira ambayo yatawafanya wafanyabiashara watengeneze faida ili waweze kumudu kulipa hizo tozo, kwa sababu baadhi ya tozo ndiyo chanzo cha uchumi, chanzo cha kuwezesha kuendeleza miundombinu mbalimbali ikiwemo ya afya, maji na mengine. Hata juzi ilikuwa bahati nzuri Mheshimiwa Dkt. Mpango alipokataa, ilikuwa tuongeze tozo nyingine kwenye mafuta, tulishasahau kwamba tunawadunga tena hao hao wafanyabiashara. Kwa bahati nzuri suala hilo tuliliona kwa mapana, halikuweza kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme kwamba Wizara yetu imejipanga na tutaendelea kutumia ushauri wenu Waheshimiwa Wabunge na wadau wengine na kuhakikisha kwamba taasisi zetu zote zinafanya kazi kiujasiriamali, siyo bora uko kazini. Mimi nimefika kazini, nimewaudumia akina nani na kwa namna gani? Hilo ndilo tunalitaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee niwashukuru wadau ambao huwa wanaturudishia mrejesho wa kupongeza jitihada ambazo tunazifanya. Mfano tu kiwanda cha karatasi Mgololo, walikuwa na changamoto tulipowatembelea, lakini tukamwona Waziri wa Maliasili changamoto zikaondolewa, wakatushukuru. Halikadhalika kulikuwa na wadau waliokuwa na shida ya kupata ardhi, kama hao wa cassava kule Lindi, tayari wanafanya shughuli zao vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia wapo wengi wenye shida kama hizo, tunasema kwamba ofisi yetu Wizara ya Viwanda na Biashara iko wazi na sisi wenyewe tuko ndani, siyo kwamba tu ipo wazi halafu hatuko ndani, tuko tayari kuwasikiliza msihangaike peke yenu, hakuna mkubwa kwenye ofisi yetu, sisi wote ni sawa mfalme ni wewe mteja, mfalme ni wewe mwenye kiwanda, mfalme ni wewe mfanyabiashara ambaye mwisho wa yote unachakata uchumi wetu na kulifanya Taifa letu liwe na uchumi imara na tuweze kulipia mahitaji yetu ya kila siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno haya, nashukuru sana na niwaombe Waheshimiwa Wabunge kutuunga mkono katika hoja yetu hii na naunga mkono mimi mwenyewe hoja yetu ya Bajeti ya Viwanda na Biashara. Ahsante sana. (Makofi)