Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi. Niungane na wenzangu kwa kuwapongeza sana Waziri wa Viwanda na Biashara, Naibu Waziri pamoja na Makatibu Wakuu na wengine wote katika Wizara hii, kwanza kwa namna ambavyo wanachochea uwekezaji katika viwanda lakini pia kwa namna ambavyo wanasimamia kuhakikisha kwamba biashara zinashamiri tukitambua kwamba biashara na sekta binafsi ndiyo injini ya ukuaji wa uchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, zimejitokeza hoja mbalimbali, ntajitahidi kwa ufinyu wa muda kujibu baadhi, hususani nipende kuingia katika hoja ya wingi wa taasisi za udhibiti nikiunganisha pamoja na mazingira bora ya uwekezaji na biashara. Kama ambavyo tumekuwa tukisema, lakini pia hata katika hotuba ya Waziri wa Viwanda na Biashara imejitokeza, Serikali katika nyakati mbalimbali kuanzia wakati wa Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara wakati wa BEST Programme mwaka 2003 lakini pia mwaka 2010 ulipoundwa Mpango Kazi au Mwelekeo wa Roadmap, pia mwaka 2017/2018 ambapo Serikali ilikuja na mpango wa kuangalia mifumo mbalimbali ya taasisi za kiudhibiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, tayari kama Serikali, Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara imekuwa ikiliangalia suala hili kwa kina na hasa kuangalia changamoto ambazo zimekuwa ndiyo vikwazo katika kuhakikisha kwamba kunakuwa na uwekezaji mkubwa lakini pia biashara kuweza kukua. Napenda tu kusema kwamba tayari Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Viwanda na Biashara na Wizara nyingine katika sekta mbalimbali, tumeshachukua hatua kupitia mapendekezo yote ambayo yametolewa katika roadmap pamoja na blueprint, tumeendelea kuandaa mpangokazi wa blueprint pamoja na ile comprehensive action plan.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini si hilo tu, Mheshimiwa Waziri Mkuu mwenyewe kwa kutambua kwamba yeye ndiye mratibu na msimamizi wa shughuli mbalimbali za Serikali, tayari alishaitisha kikao tarehe 17 Aprili, lakini pia tarehe 18 Jumamosi hii tena tutakua na kikao na Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Wizara mbalimbali ili kuweza kupitia kwa kina changamoto na vikwazo vyote ambavyo vimekuwa vikichangia kutokua kwa biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, napenda tu kuwatoa hofu Waheshimiwa Wabunge na wananchi kwamba tayari Serikali inaendelea kuyafanyia kazi. Kwa kutambua hili, tayari ziko tozo ambazo zimependekezwa kuondolewa. Naamini kwa kuwa tumeshaziwasilisha Wizara ya Fedha kupitia ile Task Force ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha ya kuangalia maboresho ya kodi, katika Muswada wa Fedha ambao utaletwa mwezi Juni nyingi mtaweza kujionea mabadiliko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo tozo ambazo Mheshimiwa Waziri wa Afya amezipendekeza kupitia TFDA, zipo ambazo zitafutwa kabisa, lakini tunaamini zipo ambazo zitapunguzwa. Pia katika Bodi yetu ya Maziwa, Bodi yetu ya Nyama pamoja na taasisi nyingine za Kiserikali, TBS na nyinginezo, yapo mapendekezo mengi tu ambayo Wizara mbalimbali zimeweza kuyawasilisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niendelee tu kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba suala zima la mifumo ya udhibiti tunaliangalia ili kuhakikisha kwamba wafanyabiashara wetu pamoja na wawekezaji wanafanya biashara zao na wanakuwa na uwekezaji ambao unashamiri bila kuwa na vikwazo vya aina yoyote. Naamini tutaweza kujionea mabadiliko makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja ya Mheshimiwa Lucy Mayenga ya kuleta mabadiliko ya Sheria ya Uwekezaji. Kwanza, nimshukuru kwa kuleta hoja hii, ni hoja ambayo pia kama Serikali tumeiona tukitambua kwamba Sheria yetu ya Uwekezaji ni ya muda mrefu, ni takribani miaka 22 na ukiangalia mambo ambayo yaliasisiwa na kuakisiwa wakati huo, mwaka 1997, inawezekana kabisa hayaendani na mazingira ya sasa ya mwaka 2019 na baadaye. Pia kuangalia suala zima la ushindani baina yetu na nchi nyingine Afrika pamoja na nchi nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijahitimisha endapo muda utaniruhusu, wapo wengi sana ambao wamezungumzia masuala ya kuomba viwanda Muheza, wengine wamezungumzia masuala ya kuwa na viwanda mbalimbali katika uchakataji wa mifugo, kilimo, uvuvi na mengineyo. Napenda tu kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba katika azma yetu ya uwekezaji suala zima la kilimo, mifugo na uvuvi ni eneo ambalo limepewa kipaumbele kikubwa na ni moja ya vipaumbele namba moja katika kuvutia uwekezaji. Tunafanya hivi kwa kutambua kwamba zaidi ya asilimia 65.5 ya Watanzania wameajiriwa katika kilimo na tunafanya hivi kwa kutambua kwamba unapowekeza katika kilimo, mifugo na uvuvi kwa kiasi kikubwa, tija yake ni kubwa na wananchi wanapata athari kubwa katika uwekezaji wa aina hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu ambacho tumekifanya hivi sasa kwa kushirikiana na Mheshimiwa Jenista na Mawaziri wengine ambao wanasimamia kilimo, mifugo na uvuvi; tunaandaa programu maalum ya uwekezaji mahsusi katika sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi kuangalia vikwazo zaidi ni nini kupitia Mradi wetu wa ASDP II.

Mheshimiwa Naibu Spika, tayari tumeshaanza mashauriano na Taasisi Isiyokuwa ya Kiserikali au Mdau wa Maendeleo AGRA ili kuja na programu jumuishi kabisa ambayo itasaidia kuangalia sekta binafsi katika kilimo, mifugo na uvuvi ni nini hasa imekuwa ni kikwazo, tunafanyaje kuwekeza katika mbegu, tunafanyaje katika masuala mazima ya trekta, teknolojia, pembejeo, mitaji na mambo mengine kwa ujumla wake ili tuangalie mnyororo mzima wa uzalishaji na uchumi katika sekta nzima ya kilimo, mifugo na uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaamini kwa kufanya hivi tutaweza kupiga hatua kubwa na na Watanzania na Waheshimiwa Wabunge wataweza kujionea mabadiliko makubwa. Hatufanyi tu katika kilimo, mifugo na uvuvi, tutaendelea pia kuangalia sekta zingine ambazo tunaamini zitaweza kuwa na tija na athari kubwa katika uchumi na uwekezaji wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)