Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi nitoe mchango wangu kwenye Wizara hii muhimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuwapongeza Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, ndugu yangu, Mheshimiwa Kakunda; Naibu Waziri; Katibu Mkuu; Naibu Makatibu Wakuu, kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya, ndani ya muda mfupi wa miaka mitatu matokeo tumeyaona.

Mheshimiwa Naibu Spika, siwezi kumsifia tu bila kutaja hata viwanda vichache ambavyo vinaonekana kwa kila mmoja. Niseme kwenye mambo ambayo ni ya msingi, tukianza kwenye viwanda vya matunda, Wizara hii imefanikisha kufungua viwanda vikubwa viwili, kuna Alvin kule Bagamoyo lakini kingine kiko pale Chalinze Mboga. Ni viwanda vikubwa saizi moja na Bakhresa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukienda kwenye viwanda vya mpunga, kuna viwanda vingi vinajengwa lakini kikubwa kuliko vyote Afrika Mashariki na kati kinajengwa pale Morogoro Mjini, Kihonda. Wengi mkipita pale Njiapanda ya Viwandani mkono wa kulia mtakiuona, ambacho kitakuwa kiwanda kikubwa kuliko vyote Afrika Mashariki na Kati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kahawa viwanda vitatu; kipo cha AMIMZA kule Bukoba Mjini, KADERES pale Karagwe na OLAM pale Misenyi. Vyote hivi ni matunda ambayo yamekuja ndani ya muda mfupi katika kipindi cha Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, twende kwenye chai pale Unilever. Juzi tu Mheshimiwa Rais alienda kukizindia kiwanda kikubwa ambacho kinatoa ajira na uhakika wa masoko ya mazao yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mpaka sasa tuna maombi chungu nzima ya walioonesha nia ya kuja kuwekeza kwenye viwanda vya korosho. Tuna matarajio makubwa mwaka huu tutaanza kubangua korosho kwa kiasi kikubwa ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nawapongeza kwa kazi hiyo. Nimetaja vichache, viko vingi, naamini nikianza kuvitaja muda wangu utakwisha hata mchango wangu nisitoe sehemu zingine, kwa hiyo, nawapongeza sana kwa hayo makubwa mnayoyafanya kuibea Serikali hii na kuwatumika wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja nyingi hapa zimetolewa za Wabunge, hatuwezi kuzijibu zote kutokana na muda lakini naamini kabisa Wizara au Serikali italeta kwa maandishi majibu ya Wabunge wote mliochangia na michango yenu tunaithamini sana, mtapata majibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja ya kulinda viwanda vyetu vya ndani, hoja ni ya msingi kwa sababu viwanda hivi tunagombeana na wenzetu, vinakuja, lazima tuweke mazingira mazuri ya kuvilinda. Waheshimiwa Wabunge, tumewasikia, tunavifahamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitolee mfano tu kwamba kuna viwanda hivyo kama vya alizeti, sio vyote vinafungwa kwa sababu ya mipango mibovu ya Serikali, hapana. Nitolee mfano viwanda viwili vya alizeti vilivyofungwa pale Singida, vimefungwa kwa sababu ya upungufu wa malighafi nchini. Kwa hiyo, tusichukulie hiyo kama ni changamoto, tuichukue kama ni fursa ya kwenda kuongeza uzalishaji wa alizeti ili viwanda vyetu vipate raw material ya kutosha. Ndiyo maana hata viwanda vingine vya alizeti vinachakata mbegu za alizeti kwa muda mfupi sana, miezi mitatu baada ya hapo mbegu nchini hakuna.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, siyo kila kiwanda kinachofungwa ni kwa sababu kuna mazingira mabaya, hapana, vingine vinafungwa kutokana na kwamba kama Watanzania hatujatumia vizuri fursa ya kuongeza uzalishaji kwa ajili ya ku-feed hivyo viwanda vyote kwa raw material. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, tuchukue hii kama ni fursa tukawaambie wapigakura wetu tuongeze uzalishaji kwa sababu soko la uhakika lipo kwa viwanda vya ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujasiriamali umezungumzwa sana hapa katika suala la kangomba, mimi sipendi sana kuita kangomba, mimi nataka niwaite wajasiriamali. Mtoto wako usimfatafutie majina mabaya, hawa wajasiriamali ni Watanzania, ni watoto wetu na ndugu zetu na Serikali tumewasikia. Kinachogomba ni sheria ambayo Bunge hili ndiyo tulipitisha, kwa mfano, Sheria ile ya Korosho Na. 12 na Na. 15, ukikutwa na korosho kama huna kibali cha Bodi ya Korosho unatakiwa ukamatwe, yaani hata haya tunayoyafanya ni huruma na ubinadamu kwa Watanzania. Tukifuata sheria inavyosema basi hata wale wakulima wote ilipaswa tuwaweke ndani. Sasa hivi tuko kwenye mchakato kama Serikali kuipitia Sera ya Kilimo ya mwaka 2013 ili tuangalie mapungufu yote hayo na tuje na sera na sheria ambayo inakidhi mahitaji ya sasa na hali ya sasa ya masoko yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wakati mwingine haya tunayoyafanya ni kwa mujibu wa sheria ambazo zimetungwa na Bunge hili. Niwaombe ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, tukileta sheria hiyo kuondoa hao mnaoita kangomba (wajasiriamali) wafahamike basi muweze kuipitisha ili sisi kwa wajibu wetu wa Serikali kwenye kusimamia sheria uwe sawasawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hilo pia wanasema kwamba labda hatujalipa, tumewatesa wakulima, hapana. Ni kweli tunakiri kuna wakulima mpaka sasa bado hawajalipwa, tunadaiwa zaidi ya shilingi bilioni 102 kati ya shilingi bilioni 724. Mpaka sasa tumeshalipa zaidi ya shilingi bilioni 622. Sasa hivi Serikali tunaweka mazingira mazuri ili kuwezesha Benki hii ya Maendeleo ya Kilimo kupata hizi shilingi bilioni 102 haraka iwezekanavyo ili kwenda kuwamalizia wakulima wachache hawa waliobaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye soko la mbaazi, kwanza ni kweli miaka mitatu iliyopita soko la mbaazi lilikuwa siyo zuri. Sababu kubwa ni kwamba hatukuwa tumeingia mkataba maalum na walaji na soko kubwa la mbaazi katika nchi ya India. Baada ya kuona mapungufu hayo, Serikali tuko kwenye mchakato wa kuingia makubaliano maalum na watumiaji au wanunuzi wakubwa wa mbaazi duniani; India na nchi nyingine, ili tuwe na uhakika wa mbaazi zetu tukizalisha tunakwenda kuuza wapi, kwa bei gani na kwa nani ili haya mabalaa yote yaliyotukuta yasitokee.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha mwisho, bado tumeimarisha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Omary Mgumba, muda wako umekwisha, ahsante sana.

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA): Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)