Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, leo naomba nianze mchango wangu kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kutoa mchango wangu kwa njia hii ya maandishi. Pia nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa dhamira yake ya kupeleka Tanzania kuwa na uchumi wa kati na nchi ya viwanda na dhamira hii tunaiona kwenye matendo yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza pia Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kufanya kazi kwa bidii katika kusimamia Wizara hii, pamoja na watendaji wote katika Wizara hii. Hata hivyo, ninayo mambo ya kushauri katika kutimiza kauli mbiu hii ya Tanzania ya Viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachowavutia wawekezaji kuja kuwekeza ni utulivu, amani na usalama uliopo lakini mara wanapoonesha nia ya kuwekeza wanakumbana na vikwazo vingi sana ikiwa ni pamoja na utitiri wa taasisi za usimamizi kama vile TBS, OSHA, NEMC, TFDA, FIRE na nyingine kama hizi ambazo kwa uhalisia zote zinafanya kazi zinazofanana. Vilevile urasimu wa njoo kesho, njoo kesho imekuwa ni kikwazo kingine. Kazi ya wiki moja inachukua miezi mitatu hata mwaka mzima. Pia taasisi hizi bado zimegubikwa na rushwa kubwa kubwa na ndogo ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado bidhaa zinazozalishwa nchini zina bei kubwa kuliko zinazozalishwa nje. Hii inachangiwa kwa kiasi kikubwa na gharama za uzalishaji nchini kuwa kubwa, kunakochangiwa na wingi wa kodi, nishati ya umeme na mafuta lakini hili la urasimu linagharimu sana nchi yetu. Watu wanaogopa kufanya maamuzi pale wanapohitajika kufanya hivyo, aidha ni kwa kutaka rushwa au kwa kushindwa kuwajibika. Kazi ya kwanza ya Wizara hii ingekuwa ya kulea wafanyabiashara na wawekezaji wa viwanda lakini kinyume chake sasa imekuwa ni maadui wakubwa kwani mfanyabiashara anapokuja Wizarani anaonekana kama msumbufu, badala ya mdau wa maendeleo mwenye kiwanda ni adui wa taasisi zilizo chini ya Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ufungaji wa maduka ya wafanyabiashara na ufungaji wa viwanda haulingani na ufunguaji wa maduka na viwanda vipya. Hii maana yake ni kuwa mazingira ya kufanya biashara nchini ni magumu sana. Ipo haja ya Serikali kukaa pamoja na wafanyabiashara wenye viwanda kuangalia namna nzuri ya kufanya biashara nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kufungamanisha kilimo na viwanda ni jambo muhimu sana lakini utekelezaji wa jambo hilo siyo mzuri sana. Uchakataji wa mazao yetu ya kilimo bado ni wa kiwango cha chini sana. Bado wakulima wengi wakubwa na wadogo hawana masoko ya uhakika wa mazao yao. Hii ni kutokana na ukosefu wa viwanda vya kutosha vya kuchakata mazao hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa naishauri Serikali kama kweli ina nia ya kutekeleza sera hii ni lazima kupunguza masharti na urasimu kwa watu wanaoonesha nia ya kuanzisha viwanda vya kuchakata mazao yetu ya kilimo, uvuvi na ufugaji. Huwezi kufungamanisha kilimo na viwanda kama hakuna viwanda vya kutosha vya kuongeza thamani ya mazao yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, idadi ya wafanyakazi wa kigeni kwa mwekezaji wa nje bado halijakaa sawa, kuna malalamiko mengi sana kwenye sekta hii. Wako wawekezaji walio waajiri wageni bila ya kuwa na sababu maalum tena bila kufuata sheria. Viko viwanda hata madereva, vibarua, fundi saidia na wengine kama hao ni wageni.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia vipo viwanda au wawekezaji wanakataliwa kuajiri watu hao (wageni) hata wale walioko ndani ya sheria. Jambo hili limekuwa likihamasisha rushwa makazini. Serikali ifanye ukaguzi wa mara kwa mara viwandani ili kusimamia sheria hii kwani ajira nyingi zinakwenda kwa wageni, hivi sasa jambo hili limekuwa ni la kwaida sana Watanzania wazawa viwandani wamebaki kuwa vibarua wasiokuwa bali ajira ya mikataba.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Waziri wa Viwanda na Biashara awe mlezi wa wafanyabiashara na wenye viwanda na kusikiliza changamoto wanazopata. Si kweli kwamba wafanyabiashara wote ni wakwepa kodi na ni wezi, je kwa nini watu hawa wanakwepa kodi? Lazima Serikali ije na utafiti kwa nini wafanyabiashara wanakwepa kodi. Kulipa kodi kabla ya kuanza biashara si jambo jema, TRA waangalie vyema jambo hili. Kama ni sheria basi sheria hii iko kinyume na maelekezo wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa naishauri Serikali lazima tufanye mabadiliko makubwa ya kisera juu ya namna ya kufanya biashara na uwekezaji nchini kwani kuzilaumu taasisi zinazosimamia sheria hatuzitendei haki. Kama zinaonekana ni kikwazo basi ni bora sheria za kuanzishwa taasisi hizi zikaletwa hapa Bungeni tuzifanyie marekebisho ili kuondoa utitiri wa taasisi hizo maana wote tunakubaliana kuwa taasisi hizi ni kikwazo kikubwa kwa wawekezaji na wafanyabiashara.