Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia katika hoja hii ya Mheshimiwa Waziri Viwanda na Biashara. Nichukue fursa hii kumpongeza sana yeye Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Watumishi wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri ambayo wanaendelea kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa pongezi sana kwa Serikali kwa mkakati huu wa ujenzi wa viwanda; ni mkakati mzuri, mkakati wenye tija sana na ni mkakati ambao utapelekea nchi yetu kuweza kufika katika hadhi ya nchi ya uchumi wa kati. Mkakati huu wa ujenzi wa viwanda nchini naomba nimpe pongezi sana Mheshimiwa Rais kwa kuusimamia mkakati huu kwa nguvu zake zote. Ni mkakati ambao una tija sana na ni mkakati ambao ni ukombozi kwa vijana wa kike na wakiume Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukombozi mkubwa kwa sababu katika mambo ambayo yanawaathiri vijana sana hivi sasa na tatizo hili linaendelea, ni ajira. Vijana hawana ajira; waliosoma wasiosoma, wenye vyeti vya Chuo Kikuu, nakadhalika, ajira imekuwa mtihani mkubwa. Viwanda vitatuletea ajira. Kwa hiyo, Mheshimiwa suala hili la viwanda lisimamie kwa dhamira nzuri ili ilete ukombozi kwa wananchi wetu na hususan vijana wa kiume na wa kike katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishauri Serikali kwamba katika ujenzi wa viwanda hivi, basi msisitizo uwe katika viwanda ambavyo vinatumia malighafi ya hapa ndani nchini kwetu. Malighafi ya hapa nchini kwetu ndiyo maana miradi kama Mchuchuma, Liganga ni miradi migumu sana kwa sababu inatumia moja kwa moja malighafi ya nchi yetu, lakini viwanda vya saruji, viwanda vya vigae, viwanda vya kuchakata minofu ya samaki, viwanda vya kuchaka muhogo na kadhalika, hivi ni viwanda muhimu sana, kwa sababu kule tunapata faida mara dufu; tunapata ajira viwandani, tunapata pia kazi katika uzalishaji wa zile malighafi ambazo zinaenda kwenye viwanda hivi. Kwa maana hiyo, tunakuza zaidi wigo ule wa ajira kwa vijana wetu wa Kitanzania ambao tunahitaji sana waweze kupata kazi hizo.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda hivi vinajengwa ardhini. Kwa hiyo, ni muhimu sana Serikali ikafanya juhudi kubwa kuhakikisha kwamba inatoa maeneo ya kujengea viwanda mapema; na kwa maana hiyo pia kuyalipia fidia kwa wale wananchi ambao wana maeneo hayo. Nalisema hili kwa uchungu sana kwa sababu katika juhudi hii ya kutwaa maeneo, katika Jimbo la Bagamoyo kuna wananchi sasa ni miaka 11. Huu ni mwaka wa 11 wametwaliwa maeneo yao chini ya EPZ I na EPZ II na mpaka leo mwaka wa 11 hawajalipwa fidia hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 1971 Mheshimiwa Marehemu Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere mwaka aliwaita Waingereza kuja kuwaonesha maendeleo makubwa ambayo tumepiga ndani ya kipindi cha miaka kumi. Miaka kumi ni muda mrefu. Sasa huu ni mwaka wa 11, wengine wamefariki, wengine wamepata vilema, wengine yaani wamekata tamaa. Wananchi hawa ni wananchi masikini kabisa, hawana uwezo mkubwa. Kimfaacho mtu chake, wamekaa mwaka wa kwanza, wa pili, wa tatu, wa 10 na wa 11 hawajapata fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Bagamoyo EPZ imechukua maeneo mara mbili; EPZ I imechukua eneo jumla ya hekta 5,742, halafu tena EPZ II hekta 3,338 kwa maana ya jumla ya hekta 9,080 katika hao wafidiwa ni 2,180, mpaka leo kuna wafidiwa 1,025 ambao bado hawajalipwa, miaka 11 baadaye wafidiwa 25,000. Jumla ya fedha ni shilingi bilioni 51 tu ndizo wanazodaiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, shilingi bilioni 51 zimesubiriwa kwa miaka 11. katika bajeti ya shilingi trilioni 32, shilingi bilioni 51 ni tone tu katika bahari; na wananchi hawa ndiyo kila kitu, maana yake wanategemea kila kitu. Wengine akina mama wajane wameachiwa watoto, wajukuu na kadhalika, kupata hela hii ndiyo ukombozi wa kila jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali yangu adhimu, Tukufu iweze kuwalipa fidia wananchi hawa mapema iwezekanavyo, wamesubiri sana. Katika kusubiri kwao maana yake watakapokuwa wamelipwa tu, ardhi hii iko free sasa kuweza kutumika kwa ajili ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo mwaka 2018 katika bajeti nililiongelea, naiomba tena Serikali yangu Tukufu mwaka huu, EPZ II imehusisha maeneo yenye makazi makubwa ya wananchi jumla ya hekta 3,338; Ziha kwa Awadhi, Ziha kwa Mtoro, Mlingotini, Kondo na Kiromo, vijiji vyote hivi vina wakazi wengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa heshima na tahadhima, naiomba Serikali yangu Tukufu iondoe maeneo haya ya makazi makubwa ya wananchi katika mradi wa EPZ ili wananchi hawa waendelee kuishi kwa amani na utulivu. Wameshatoa zaidi ya hekta 5,700 kwa ajili ya hii EPZ na nadhani inatosha kabisa na hawajalipwa kwa miaka 11, wala hawana mahali pa kwenda na hawana nguvu za kuhamia mahali pengine. Naiomba Serikai yangu adhimu iwaache wananchi waendelee kuishi katika maeneo yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda umeshaisha Mheshimiwa. Kengele ya pili imeshagonga.

MHE.DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Naibu Spika, muda umekuwa mfupi. Nakushukuru sana kwa kunipa fursa. Naunga mkono hoja. (Makofi)