Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakushukuru kwa kunipa nafasi, lakini nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na kuweza kuchangia katika Wizara hii. Mimi nianze kidogo kuweka sawa baadhi ya mambo ambayo yapo kwenye Wizara hii ya Viwanda na Biashara. Nitaendelea kuunganisha pale alipochangia ndugu yangu Mheshimiwa Antony Komu suala la wasaidizi wa Mheshimiwa Rais kumpotosha kwa mambo mengi sana. Kwenye korosho, hili limetokea, watu wamempotosha sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani Mheshimiwa Rais akiwa Arusha alizungumzia suala la kangomba ambalo nataka nikwambie, kwa sisi Waislam hiyo biashara inayoitwa kangomba siyo dhambi, kwa sisi Waislam. Kwa sababu ipo hadithi sahihi kabisa inatoka kwa Ibn Abbas Radhiya Allahu- Anhu, Ibn Abbas anasimulia, alikuta Mtume amefika Madina na alipofika Madina akakuta watu wanafanya biashara ya matunda kwa makubaliano, kwa uwiano wanaokubaliana wenyewe. Mtume alipokuta biashara ile inakwenda, akasema hii biashara siyo haramu. Hadithi hii imepokelewa vizuri kabisa na wapokeaji wazuri kwa sisi Waislam ambao ni Bohari pamoja na Muslim. Kwa hiyo, kangomba siyo haramu kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo Waziri wa Biashara ambaye upo hapa, kwenye korosho tunajua watu hawajapata fedha mpaka leo; wapo waliopata fedha na upo utaratibu ambao umetumika labda huujui, nikukumbushe tu kwamba mwezi wa Nne zimetoka fedha, mtu anadai shilingi milioni 59 ili ku-rescue situation ionekane wakulima wamelipwa fedha, anaingiziwa shilingi milioni tisa anadai shilingi milioni 41. Hicho ndicho kichokuwepo kwenye korosho. Ukitaka ushahidi, mimi ninayo simu hapa, nimeingiziwa fedha mwenyewe. Nadai shilingi milioni 48, nimeingiziwa shilingi milioni nane, nyingine naendelea kudai na hili unalijua vizuri, unalifahamu vizuri kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo wakulima wa korosho wameanza kufanya palizi, hawana fedha. Kama hawana fedha, wanatafuta watu wanaingia makubaliano, mtu anampa shilingi 100,000/= wanakubaliana wenyewe kwamba atampa gunia moja la korosho. Mnakaa mnamshauri Mheshimiwa Rais kwamba aliyefanya vile ni kangomba. Hii ni biashara halali kwa sisi Waislam. Kwa hiyo, kangomba siyo haramu kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sababu ya msingi ya biashara hii ni kwamba Serikali hamjajipanga. Leo Serikali imezungumza kwamba inachukua fedha kuwalipa wakulima, lakini mpaka wakulima wanadai fedha za korosho. Je, mkulima asilime korosho? Anapatikana mtu ambaye amekubaliana naye mwenyewe kwa hiari yake anampa fedha, mwingine anachukua trekta anaenda kulima shamba la mikorosho. Akishalima ekari moja kwa makubaliano kwamba atampa korosho kilo 50, lakini mkikaa mnamwambia Mheshimiwa Rais kwamba wale watu ni kangomba. Wale siyo kangomba. Kwa hiyo, jambo hili lazima Mheshimiwa Waziri alijue vizuri sana ili akitokea, isije mwakani tena watu mkakurupuka mkamshauri Mheshimiwa Rais ndivyo sivyo kwenye korosho.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Katani, ongea nami ujumbe wako uwafikie. Kwa sababu ukiongea nao moja kwa moja sasa, hakuna namna wao wataupata. Wewe ongea na kiti ili wao waupate.

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Kwa hiyo, naomba sana suala hili wakati wanamshauri Mheshimiwa Rais waende kufanya research kwanza, wajue matatizo ya wakulima yakoje? Mwaka huu tutakuwa na tatizo la dawa. Kuna tatizo la wakulima, kulima korosho yenyewe. Leo ukienda Mtwara, mikorosho watu wanawekeza. Shamba lenye ekari 10 mtu anawekeza kwa shilingi 500,000/= tu. Yule aliyewekezwa shamba, akivuna gunia 50 kwa sababu amewekeza na hana shamba, kesho kutwa anataka akuoneshe hati ya shamba, maana yamefanyika mwaka huu. Mtu alikuwa hatakiwi kulipwa fedha, mpaka alipokwenda Mheshimiwa Rais juzi, akasema watu wote walipwe. Huu ni ushauri ambao wasaidizi wa Mheshimiwa Rais wanamshauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwenye hili, naomba sana Bunge lifahamu vizuri, kwamba kwenye biashara hizo za mazao na siyo kwenye korosho tu, hata kwenye mpunga. Mimi nina trekta Ifakara pale, nalimisha mashamba, mwisho wa siku wananilipa magunia ya mpunga. Ukija kutafuta shamba langu, mimi sina shamba Ifakara.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nataka niombe sasa Mheshimiwa Waziri ajaribu kutueleza kama alivyokuwa anazungumza ndugu yangu Mheshimiwa Komu; ile kampuni, baada ya kampuni kushindwa sasa kuilipa Serikali zile tani 100,000 za korosho walizokuwa wameingia makubaliano ya kisheria, watuambie hao INDO Power wanatufidiaje kwa kutudanganya? Maana wamelidanyanga Taifa. Ni lazima tuone INDO Power moja wanashtakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili watulipe fidia kwa sababu Watanzania walikuwa na matumaini kwamba korosho tani 100,000 zimepata mnunuzi, kumbe ni matapeli, Wakenya wamekuja kututapeli na wametudhalilisha wakulima wa korosho ambao mpaka leo hatujapata fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye suala la viwanda. Kule Kusini tulikuwa na viwanda vya kubangua korosho takribani 12. Vile viwanda vimeuzwa. Waliouziwa vile viwanda, maelezo yalikuwa waendeleze vile viwanda kwa ajili ya kubangua korosho.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri anajua, vipo viwanda leo ni maghala ya kutunzia korosho, siyo viwanda vya kubangua korosho. Wakati ana windup atuambie Serikali ina mpango gani kwa wale walionunua viwanda kwa dhamira ya kubangua korosho kwa kubinafsishwa wana mpango gani kuhakikisha wale walioshindwa wana mpango gani kuhakikisha wale walioshindwa kupangua korosho viwanda vinataifishwa, virudi kwa watu ambao wanaweza kupangua korosho ili tuweze kuendelea na tasnia ya viwanda Tanzania? Atusaidie na bahati nzuri alikuwepo kwenye ziara ya Mheshimiwa Rais na haya ameyasikia mwenyewe na mengine amejionea mwenyewe kwa macho, ajaribu kutusaidia kujua viwanda vile vya korosho mambo yake yanakuaje?(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)