Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi pia niweze kuchangia Wizara hii ya Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, kwa kuwa na ndoto kubwa ya Tanzania ya Viwanda ifikakapo 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia niwapongeze Mheshimiwa Makamu wa Rais pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kutafsiri ndoto hii vizuri kwa watendaji wa Serikali walioko chini yao. Kwa kweli, mambo yakienda hivi, tunaweza kufikia ndoto hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumze mambo machache tu ambayo Serikali lazima iyaangalie tunapotaka kufikia ndoto hii ya Tanzania ya Viwanda ifikapo mwaka 2025. Hatuwezi kuwa na viwanda imara ikiwa hatuwezi kuvilinda. Viwanda vinavyoanzishwa kwenye nchi yetu lazima vilindwe. Hakuna nchi ambayo imetamani kuwa nchi ya uchumi wa viwanda, halafu ikaviacha viwanda vyake bila kuvilinda kwa sababu vingeweza kufa. Hivyo hivyo, nasi kama nchi, lazima tuwe na juhudi za makusudi kulinda viwanda vyetu ili viweze kusimama, kukua na kuimarika. Vinginevyo tusipovilinda, itakuwa ngumu kufikia ndoto ya Mheshimiwa Rais ya Tanzania ya Viwanda mwaka 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba tunaweza kuvilinda viwanda vyetu kwa njia za kikodi na utawala. Tusipofanya hivyo, nimesema Tanzania ya Viwanda hatuwezi kuipata haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda vyetu vingi vimeanzishwa lakini havifanyi kazi kwa uwezo wake kamili. Tulikuwa na viwanda vya nguo 33 mwaka 1992 lakini leo tuna viwanda vitano vinavyofanya kazi lakini navyo kwa chini ya kiwango. Ni kwa sababu viwanda hivi vimeachwa wazi vishindane na mabwana wakubwa walioanzisha viwanda vya nguo muda mrefu kama India, China, Uturuki na nchi zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bila kulinda viwanda vyetu vya nguo itakuwa ni ngumu, lakini tukivilinda viwanda hivi, vinaweza vikatupatia ajira kwa wakulima wetu, ajira kwa watu wetu, kwa maana ya wafanyakazi viwandani lakini pia vinaweza vikaongeza kipato kwa ajili ya taifa letu kwa maana ya kulipa kodi. Tusipofanya hivyo hatutafanikiwa kabisa (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimejaribu kuona namna alivyotoa hotuba yake Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, sijaona kama kuna sera makusudi ya kulinda viwanda vyetu ili viweze kukua. Kwa namna vilivyo sasa hivi, viko kwenye kiwango cha chini sana, ni viwanda ambavyo tunaweza kuviita ni vichanga. Sasa tukivi-expose kwenye mashindano haya makubwa, havitaweza kukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hotuba ya Waziri, amesema viwanda vyetu vya chuma vina uwezo wa kuzalisha tano milioni moja, lakini vinazalisha tani laki mbili na arobaini, mwisho hapo. Sasa tatizo ni nini? Tatizo ni kwamba vinashindanishwa na viwanda vya chuma vilivyostawi na kuimarika muda mrefu vya Wachina.

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda hivi visipolindwa, haviwezi kukua na vikiendelea kufanya kazi kwa uwezo wa chini namna hii, gharama zake ni kubwa, matokeo yake wananchi wetu wanaendelea kununua nondo na vifaa vingine vya chuma kwa bei ya juu. Lazima tulinde viwanda vyetu, lazima tuvilinde viwanda vya nguo, chuma na viwanda vinavyoinukia sasa hivi. Tusipofanya hivyo, kuwa na Tanzania ya Viwanda, itakuwa ni ndoto 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia vivutio vya uwekezaji kwenye viwanda. Vivutio hivi vya uwekezaji kwa viwanda, lazima vile vinatabirika. Mwaka jana tulipitisha sheria kuvilinda viwanda vinavyozalisha madawa, ni jambo zuri sana, lakini tusiishie kulinda viwanda vinavyozalisha madawa tu lazima twende pia kwenye viwanda vingine. Lazima tuweke vivutio vinavyoeleweka, vinavyotabirika, vitakavyokuwa vya muda mrefu ili hawa wawekezaji watakapokuja hapa ndani, wawe na uhakika ya kwamba vivutio hivi vitakuwa ni vya kudumu na hivyo wanaweza wakafanya biashara hapa ndani vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye suala la Mradi wa Mchuchuma na Liganga. Mradi huu wa Mchuchuma na Liganga ni wa muda mrefu sana. Kwa kweli niungane na wengine wote waliosema kwamba imechukua muda mrefu na inabidi sasa juhudi za makusudi zifanyike ili tuwe na mradi huu mapema iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nataka kutoa tahadhari…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mbunge, kengele ya pili imeshagonga.

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, muda ni mdogo sana. (Makofi)