Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kunipa fursa ya kuchangia leo lakini pia nipongeze kwa jitihada mbalimbali zinazoendelea kufanywa na Serikali kuboresha sekta nzima hii ya ufanyaji biashara lakini pia kuleta maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku zote hapa huwa nasema pasipokuwa na coordination, namna ya kuhakikisha kwamba Wizara mbalimbali zinafanya kazi kwa pamoja, suala la viwanda na biashara itakuwa ni ndoto. Kwa hiyo, ni muhimu sana Serikali ikae kama timu mojo, Wizara na Wizara ziwasiliane na kama kuna jambo lolote washirikiane kuhakikisha jambo hilo wanalitatua kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi hapa tutakuwa tunalaumu labda Wizara ya Fedha kwamba kodi ni kubwa, lakini kodi zao ni tatu tu, ukiangalia tatizo kubwa ni regulatory authorities kuhusiana na tozo, ada na ushuru mbalimbali zinazoenda kwenye Wizara zote. Ukiona mmoja sasa hivi anasemwa kwenye Wizara yake atanyamaza lakini wengine wote wanabaki kusubiri yale mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kumekuwa na mtindo ili Wizara fulani ionekane imekusanya mahuhuli makubwa na mengi wanapiga fine za ajabuajabu. Mimi nashauri zile za fine mngeziweka pembeni, isiisabiwe, ikipigwa fine iende kwenye Mfuko Mkuu isiingie kwenye hesabu ya Wizara hiyo, kwenye Wizara ibaki ile ambayo ni jukumu lake, ndiyo tutaona Wizara na hizo taasisi zinafanya vizuri siyo kwenye fine, kwa sababu fine ndiyo inawabeba kwa sehemu kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nimeshauri kwamba hizi regulatory authorities tuziunganishe pawe na upper stream na lower stream, zifanye kazi under umbrella ya Tanzania Regulatory Authority kwa sababu ndiyo zote zimebeba hizo tozo, ada, ushuru mbalimbali. Pia nashauri kwamba pawe na ukomo wa kukusanya tozo za miaka ya nyuma. Leo anakuja mtu wa NEMC anakudai ya miaka kumi nyuma, anakuja mtu wa TFDA anakudai ya miaka kumi nyuma, hivi siku zote walikuwa wapi? Kama hii ya TRA miaka mitatu mwisho, siku za nyuma wasiwe na mamlaka ya kudai kwa sababu kama walilala ni makosa yao siyo makosa ya huyo mfanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nilikuwa nimeshauri kwamba tuwe na One Stop Center, Afisa Biashara iwe ya Mkoa, Wilaya au Wizarani, mimi siwezi kujua sheria zote za regulatory authority, leseni na tozo mbalimbali ambazo zinafika mpaka 40. Ni vizuri tukienda Afisa Biashara anielekeze kwamba nikikata leseni natakiwa niwe na vibali vyote hivi na mlipa huyo mtu mmoja One Stop Center kama mwingine amesahaulika hajajulikana, Serikali ndiyo itajua namna ya kufidia huko siyo mimi mfanyabiashara. Ease of Doing Business, tukiweza urahisi wa kufanya biashara ndiyo njia pekee tutaweza kuwa na mafanikio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini namna ya kulinda viwanda vya ndani, ni lazima tuwe na mifumo ya kulinda viwanda vya ndani dhidi ya bidhaa zinazotoka nje au zinazozalisha nje. Mkumbuke hawa ndiyo wanaozalisha ajira, ndiyo wanalipa kodi isije ikafika mahali sisi ikawa ni sehemu ya kuleta bidhaa kutoka nje kama Dubai, wanachukua bidhaa kutoka dunia nzima wanachukua tozo ndogo wanafanya biashara, je, sisi tunataka tuwe hivyo? Sisi tunataka tuwe na viwanda na vifanye kazi na lazima tuwe na mifumo ya kulinda viwanda vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata wenye viwanda na wenye biashara wanalalamika wanalipa SDL lakini fedha hizo hazirudi kwenda kuwasaidia kuboresha kwa mfano SIDO, TIRDO, CAMARTEC. Mimi nasema ile asilimia 4.5 yote ingeenda huko zikaboresha VETA zetu na hizi taasisi zote ili wawe na fedha za kufanya utafiti na kuandaa wataalam ambao wataweza kuja kukusaidia katika masuala ya viwanda vyetu na biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lazima tuunganishe uzalishaji, sehemu kubwa ya nchi yetu ni kilimo, mifugo na uvuvi. Tusipoangalia namna ya kuunganisha bidhaa zao hatutafanikiwa. Leo hii Serikali ifanye tathmini yake, miaka mitano nyuma na leo, sekta rasmi na sekta isiyokuwa rasmi ipi inakua, asilimia kubwa ya watu wameondoka kwenye sekta rasmi wanarudi kwenye sekta isiyokuwa rasmi kutokana na tozo, ada, kodi na ushuru mbalimbali ambapo Serikali itafika mahali haitakuwa inapata ushuru wala kodi ambayo inastahili kupata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia vyuo vyetu vya elimu viangalie namna ya kutoa elimu ambayo inalingana na uhitaji wetu ndani ya nchi. Pia bidhaa nyingi zinazokuja nchini ni substandard lakini tunalipa kwa bei ileile ya standard. Kwa hiyo, ni vizuri taasisi hizo ziweze kufanya kazi vizuri na tuangalie namna ya kuondoa huu rasimu uliopo ili tuweze kufanya kazi vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri tuweze kuangalia namna ya kuwekeza kwenye sekta ambazo zinazalisha kama kilimo, mifugo na uvuvi ili ziweze kuzalisha bidhaa za kutosha na kwa viwango ili tuweze kuwa na viwanda. Serikali ingefanya tathmini kwamba bidhaa tunazoagiza kutoka nje ya nchi nini ambacho tunaweza kuzalisha hapa nchini, moja ikiwa ni mchele, mafuta ya kula, sukari, mbegu bidhaa hizo zote tunaweza kuzalisha humu nchini kwa nini tusiwekeze huko ili watu wetu wapate ajira?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ijue kwamba siyo kila mahali lazima upate direct tax kwamba lazima upate kodi au ushuru. Inawezekana katika kiwanda kimoja Serikali haipati chochote pale lakini kinaajiri watu zaidi ya 10,000 au 20,000, tayari watu wakiwa na spending power yaani uwezo wa kununua bidhaa Serikali itakusanya kodi kubwa kupitia indirect taxes.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wangeangalia kwenye tozo, kodi na ada wazipunguze ziweze kulipika na compliance itakuwa kubwa. Badala ya watu kuwa na tamaa ya kukwepa wakizipunguza gharama hizo watu wengi zaidi wataweza kulipa na Serikali itakusanya mapato makubwa lakini uzalishaji ndani ya nchi utakuwa mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunajitahidi kuondoa baadhi ya kodi kwa kupitia Sheria ya Finance lakini baadaye inarudishwa kupitia Kanuni. Mimi naomba suala hili la Kanuni kama Bunge hili litaridhia badala ya Waziri kuwa na mamlaka kupeleka moja kwa moja kutangaza kwenye Gazeti la Serikali haswa popote panapohusiana na kuongeza au kupunguza tozo mbalimbali iwe ni lazima iletwe Bungeni ama kwa kupitia Kamati husika ili zisiruhusiwe kwenda kupandishwa kiholela kwa sababu tunaweza kuondoa kodi fulani hapa baada ya muda mfupi unakuta Waziri kule kwenye Kanuni anapandisha tozo hizo na kufanya wafanyabiashara kuendelea kupata tatizo na urahisi wa kufanya biashara unakuwa mgumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri tungekuwa na mfumo wa kuangalia namna ya kufanya uratibu. Mimi nashukuru sasa tuna Waziri wa Uwekezaji na yeye kazi yake kubwa ni kuangalia urahisi wa uwekezaji wa ndani, wa nje, mkubwa au mdogo, yeye ndiye atakuwa sasa ndiyo mratibu wa shughuli zote kwenye biashara akisaidiana na Waziri wa Viwanda na Biashara lakini na Mawaziri wengine wote ili kuangalia wapi kuna changamoto na waweze kuleta mara moja kama ni sheria ibadilishwe lakini kama kwenye Kanuni wawaagize wale Mawaziri waziondoe ili urahisi wa kufanya uweze kupatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ingewezekana kwa miaka yote michango ya Wabunge ingeangaliwa kwenye Hansard walichangia nini na tukaletewa hapa, naamini kila mwaka tutaendelea kusema lakini yanayotekeleza ni machache. Lengo ni kuhakikisha kwamba tunapata mafanikio, nchi yetu iende mbele na fursa zote tunazo isipokuwa utaratibu wa kuhakikisha hizo fursa zinatumika vizuri ndiyo haufanyiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ndiyo kubwa kuliko zote ambapo ndiyo inasimamia biashara na masoko yote lakini pia kuendelea kukuza viwanda vikubwa na vidogo, ni jukumu lenu kushauriana na Wizara zingine zote kuweka mazingira wezeshi ili Watanzania waweze kuwekeza. Siyo kwamba Watanzania wanashindwa kuwekeza, mitaji na uwezo wanao, jukumu lenu kukaa na kuhakikisha tunaweza kufanya shughuli hizo kwa unafuu zaidi. Badala ya kuangalia maslahi ya watu wachache tuangalie maslahi ya wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo machache, nashukuru na naunga mkono hojo. (Makofi)