Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake, wanafanya kazi nzuri, lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitumie nafasi hii kuzungumza mambo machache; kule Korogwe tuna barabara inaitwa Korogwe – Dindira – Bumbuli – Soni, ni barabara ya kilometa 77. Kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2010 ambayo ninayo mkononi hapa, kwenye ukurasa wa 48 kulikuwa na ahadi ya kufanya usanifu kwenye barabara hii. Kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015, kwenye ukurasa wa 58 kuna ahadi ya chama chetu kwenda kutengeneza barabara hii kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipoingia kwenye Bunge lililopita, kwa maana ya Mkutano wa Kumi na Nne, niliuliza swali, Mheshimiwa Waziri akaniambia wametenga shilingi milioni 130 kwa mwaka huu wa fedha unaoisha Juni kwa ajili ya usanifu, lakini mpaka sasa hivi hela zile hazijafika, na usanifu umeshafanyika kwenye kilometa 20 za kutoka Soni kwenda Bumbuli, bado kipande cha kutoka Bumbuli – Dindira – Korogwe na ahadi hii imekuwa ni ya muda mrefu kwa watu wa Korogwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepitia kitabu cha Mheshimiwa Waziri, nimeona kwenye ukurasa wa 181 kuna hela, bilioni sita, wametenga kwa ajili ya barabara pale, wamesema kuanza matengenezo ya lami. Hata hivyo, nilipokwenda ndani zaidi kwenye kitabu, kwenye ukurasa wa 275 wametenga shilingi milioni 770 kwa ajili ya ukarabati, lakini wameweka kwenye ukurasa wa 317 wametenga shilingi milioni 140 kwa ajili ya usanifu. Kwa ukubwa wa kilometa zilizobakia, shilingi milioni 140 haiwezi kutosha kukamilisha shughuli ya usanifu kwenye barabara ile, hata ile 130 ambayo bado haijafika ikija haiwezi kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kwamba matengenezo ya barabara hii ni muhimu, lakini kwa kuwa watu wa Korogwe wamekuwa na kiu ya barabara hii kwa muda mrefu na ni ahadi ya chama chetu; ni ahadi ya viongozi wa Serikali akiwemo Mheshimiwa Rais, akiwemo Mheshimiwa Waziri Mkuu, nimwombe Mheshimiwa Waziri, kama hatuna mahali pengine pa kupata fedha ya kukamilisha usanifu ili tuanze kujiandaa kwenda kujenga, basi hizi 770 tupeleke kwenye usanifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka huu tumefanya matengeneo na nimpongeze Meneja wa TANROADS, Mkoa wa Tanga, Enineer Ndumbaro, anafanya kazi nzuri sana, sisi Wabunge wa Mkoa wa Tanga tunaisifia kazi yake, anafanya kazi nzuri sana. Mwaka huu tumefanya matengenezo, sehemu iliyobakia ni maeneo machache yaliyobaki, nina hakika hizi milioni 140 na zile milioni 60 nyingine wametenga zinaweza kutosha kumaliza hii kazi. Hebu hizi milioni 770 tupeleke kwenye usanifu ili kazi ya usanifu ikamilike, halafu tuendelee na kutafuta hela kwa ajili ya kutengeneza barabara kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara ya Old Korogwe kwenda mpaka Magoma ambayo inakwenda kuunganisha mpaka na wenzetu wa Mkinga, ni barabara muhimu, lakini haijawahi kufikiriwa kuwekwa kwenye kiwango cha lami. Tunaomba sana Serikali iikumbuke hii barabara. Pia nawakumbusha watu TANROADS wameweka alama za X kwenye nyumba za watu na kuna wengine wamekaa miaka mingi kama watu wa pale maeneo ya Kerenge Kibaoni waende wakapewe elimu juu ya hatma ya makazi yao pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipongeze sana Shirika la Reli kwa kazi kubwa ya kufufua hii reli, reli ya kutoka Tanga kwenda mpaka Moshi na sehemu ya Tanga- Same imeshakamilika. Ninachoomba tu, SGR wakati ukifika watukumbuke, lakini kwa sasa hivi yale maeneo ambayo kuna makazi ya muda mrefu, watuwekee vivuko ili wananchi waweze kuvuka kutoka upande mmoja wa reli kwenda upande mwingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Nditiye na kaka yangu Engineer Ulanga wamefanya kazi kubwa kule Kizara tulikuwa na shida ya mawasiliano, lakini bado yako maeneo nimeyapeleka kwao maeno ya Lewa, Lutindi, Makumba na Kata ya Mkalamo, tunaomba watupelekee huduma ya mawasiliano kwa ajili ya watu wetu pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, muda sio rafiki sana. Kuna jambo limezungumzwa hapa na kiti chako kimeshalisemea. Tunazungumza yapo malalamiko kwamba kwa nini Wakala wa Ndege amehamishwa kwenda kwenye Ofisi ya Mheshimiwa Rais? Lazima tukumbuke nchi yetu inaongozwa kwa mujibu wa sheria za nchi yetu aliyepewa dhamana ya kuongoza Taifa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hawa walio chini yake wanamsaidia na hata ukiosoma Presidential Affairs inaeleza, hakuna dhambi kwa Rais kuamua kazi ipi ya Serikali isimamiwe chini ya Wizara ipi au ofisi ipi siyo dhambi. Ni vibaya kusema kwamba Rais amefanya makosa au ana nia ovu, sheria inamruhusu, hakuna sheria inayovunjwa ni utaratibu wa kawaida. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)