Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii niweze kuchangia Wizara hii ya Miundombinu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kunipa afya na nguvu ya kuweza kuchangia katika Wizara hii. Niwapongeze Waziri, Mheshimiwa Eng. Kamwelwe, Naibu Waziri Mheshimiwa Nditiye na Naibu Waziri Mheshimiwa Kwandikwa kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuishukuru Wizara hii kwa kunitengea fedha za kujenga kilometa 1 kila mwaka ambapo zinajengwa katika barabara ya kutoka Magamba – Mlalo na Magamba - Mlola. Nashukuru Serikali kwa kilometa 1 waliyotutengea lakini ni chache sana ambapo sasa hatuendi na ile kasi ya kujenga viwanda na kwenda kwenye uchumi wa kati. Nimuombe Waziri aweze kututengea hata kilometa 4 ili pande zote mbili ziende kilometa 2, Mlalo kilometa 2 na Mlola kilometa 2. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hayo pia kuna barabara ambayo kila siku nilikuwa naionglea, inaanza Mlalo - Ngwelo - Mlola – Makanya – Milingano - Mashewa. Barabara hii inaenda mpaka kwa Mheshimiwa Kitandula Mkinga kule, inaenda mpaka Chongoleani, kwa hiyo, barabara hii ni ya kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini barabara hii nimeiongelea sana na hii ni bajeti ya nne. Nikuombe Mheshimiwa Waziri kwamba, itoshe sasa, mimi siyo mtoto wa kufikia, mimi ni mtoto wako kabisa, sijawahi kushika shilingi, sijawahi hata kukataa bajeti, ifikie hatua sasa Mheshimiwa Waziri hebu barabara hii uichukue ili tuweze kunusuru watu wa Makanya na maeneo mengine niliyoyataja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo Mheshimiwa Waziri anafahamu fika kwamba barabara ile ni ya kiuchumi. Barabara ile kuanzia Makanya au Mlola kwenda maeneo niliyoyataja hakika tutakuwa tumekuza uchumi. Kwa hiyo, nikuombe sana itoshe, kwa kweli sijui niingie kwa style gani au nije kwa style gani ili uweze kunielewa barabara ile iweze kupandishwa hadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kuna barabara nyingine ya kutoka Dochi – Ngulwi - Mombo ambayo ni kilometa 16. Barabara ile Mheshimiwa Waziri niliripoti kwako 2017 wakati barabara ile inapata mafuriko. Kwa hiyo, nikuombe nayo barabara hii Mheshimiwa Waziri hebu iingize sasa iweze kutengenezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii walisema kwamba TARURA inaweza lakini TARURA haina fedha za kutosha kila mwaka inatengewa kilometa 1 au 2, kwa hiyo, ni kama vile barabara hii imetelekezwa. Mheshimiwa Kwandikwa ni shahidi amefika mpaka pale kwa wananchi wa Ngulwi ameongea nao akawaambia kwamba barabara hii sasa itatengenezwa lakini mpaka leo hii barabara ile haijatengenezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ile pia ni ya kiuchumi. Halafu ni barabara ya mchepuko, kama unavyofahamu Lushoto kuna barabara moja tu kubwa ambayo ni ya Mombo – Soni - Lushoto kilometa 32. Kwa hiyo, kukitokea matatizo kama yalivyotokea 2017 na kuziba barabara ile ya Soni – Mombo basi Wilaya ya Lushoto tunakosa huduma kabisa. Kwa hiyo, niombe sasa barabara hii iwe barabara mbadala na inawezekana hata barabara hii sasa ikawa ni barabara kwa ajili ya kushuka tu magari na hii ya Soni - Mombo kwa ajili ya kupandisha magari. Hiyo, naamini kwa kweli ukiipanga vizuri Mheshimiwa Waziri inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja sasa kwenye minara (mawasiliano). Mheshimiwa Nditiye wewe ni shahidi nimekuja mara kadhaa kwako kwa ajili ya kukuomba minara. Mfano maeneo yangu mengi ya Wilaya ya Lushoto hayana mawasiliano, mfano, Ubiri, Mazumbai, Magului, Makanya, Kireti, Kigumbe na maeneo ya Mlalo ya Makose, Longoi, Mavumo na Kikumbi. Nikuombe chondechonde kaka yangu hebu sasa peleka mawasiliano katika maeneo haya ili wananchi wetu waende na wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende sasa kwenye Uwanja wa Ndege Tanga, wenzangu wameongea sana kuhusu uwanja huu. Uwanja ule wa Ndege kweli tumeona tumetengewa mashine zile lakini ziende sambamba sasa na kuongeza uwanja ule. Mwaka jana Mheshimiwa Waziri ni shahidi wakati wa bajeti wakati ana-wind-up alisema kabisa kwamba uwanja ule utaletewa bombardier lakini mpaka leo hii bombardier hatuioni, Tanga kumekucha, Tanga kuchele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hebu sasa Tanga ionekane, safari hii tuweze kupata bombardier inayotoka Dar-es-Salaam kuja Tanga mpaka Pemba ikiwezekana hata iende mpaka Mombasa. Hili naomba sasa nalo ulichukue wakati wa ku- wind-up naamini kabisa utalisemea na ukizingatia Tanga tayari tunaongeza kina cha bahari, Serikali imetuona, tuna viwanda pia kama unavyojua.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, naona muda umeisha. Naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia 100, ahsante. (Makofi)