Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. nianze moja kwa moja katika hotuba hii kwenye suala zima la mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya mwaka jana Wizara ilitenga bajeti na ilieleza kwamba, ingejenga minara ya mawasiliano katika vijiji vya Kinjumbi, Mwengei, Nandete, Chapita, Mtende na Mterambuko, hivi vingejengwa kwa kampuni ya TTCL, lakini Vijiji vya Kandawale pamoja na Mtumbempopera vingenjengwa na wenzetu wa Kampuni ya Vietell; mpaka hivi ninavyozungumza bado hakuna chochote kimeanza kufanyika. Niiombe Wizara hizi kampuni zianze kufanya kazi kwa sababu, tayari tumeshawaambia Wananchi na Wananchi wanasubiri kwa hamu kubwa, lakini nishauri pia katika bajeti hii ya mwaka huu niombe vijiji vya Mkarango, Ngarambi, Miteja, Namakolo, Mtepela, Kibata na Ingirito vipate mawasiliano kwa sababu, vijiji hivi havina mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jingine niende kwenye suala zima la barabara, awali ya yote katika suala la barabara nichukue nafasi hii kukupongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwani katika ile Barabara ya Nangurukuru – Liwale kilometa mia mbili kama na 30 hivi kwenye Kitabu cha Bajeti yako ukurasa wa 226 nimeona umetenga pesa kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu pamoja na engineering design. Nikupongeze sana kwa hilo, sasa angalao tuna matumaini kwamba, barabara itaenda kujengwa kwa kiwango cha lami, basi tunachosubiri ni utekelezaji. Sambamba na hilo naomba Serikali iiangalie pia, Barabara ya kutoka Tingi – Kipatimu na Ndeti. Nayo basi iingie kwenye kuwekwa bwasi kwenye upembuzi yakinifu, ili basi hatimaye ije kujengwa katika kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo naomba niendelee kukumbusha ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, katika Sherehe ya Kumbukumbu ya Vita ya Majimaji pale Nandete alisema kwamba, yeye angejenga barabara ya kutoka Nandete – Nyamwage. Naomba niwakumbushe barabara hii ni muhimu na ni ahadi ya Mheshimiwa Rais; na nishauri, kijiografia ukitoka Nyamwage kwenda Kipatimu ni kilometa 50 sawasawa na kutoka Njia Nne kwenda Kipatimu, lakini leo hii tukitaka kwenda Kipatimu unalazimika ufike mpaka Nyamwage ambako utaenda kilometa 75 mpaka Njianne ndipo uende Kipatimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa barabara hii ya kutoka Nyamwage kwenda Kipatimu ya kilometa 50 kama ingekamilishwa na ingejengwa kwa changarawe tu, basi ungeturahisishia sana mawasiliano kutoka Nyamwage kwenda Kipatimu. Kwa kupitia barabara hii ukitoka Dar-es- Salaam kwenda Kipatimu ni kilometa 230 tu, lakini kwa kuzunguka tunakwenda kwa kilometa 280. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba barabara hii ambayo inapita kwa Ndugu yangu Mheshimiwa Mchengerwa halafu inakwenda kwangu ijengwe basi, iwe chini ya TANROADS, iimarishwe ili basi tuweze tukapata tukaweza kusafiri kwa mwaka wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo niombe sasa TANROADS waangalie uwezekano wa kuweka vipande vya lami katika milima ya barabara ile ya Tingi – Kipatimu, kuna Mlima Ndundu na Mlima Ngoge, mlima sumbusfu sana. Basi tuwekewe angalao vipande vya lami, ili basi tuweze kusafiri kwa wakati wote, wakati wote tunaweza tukapita kama hivyo vipande vitawekewa vipande vya lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo naomba TANROADS waangalie barabara ya kutoka Ndundu kwenda Somanga imewekwa lami katika kipindi ambacho hakizidi miaka mitatu minne, lakini leo ukienda ile barabara yote imefumuka. Niiombe Wizara makampuni wakati wanatekeleza miradi hii muwe makini sana vinginevyo ni upotevu wa pesa za Serikali kwasababu, barabara ya lami tunategemea ikijengwa angalao ikae miaka 20 na kuendelea, sasa ile barabara imekaa miaka mitatu tu sasa hivi mnarudia tena kufanya ukarabati mkubwa kana kwamba ilijengwa katika kiwango cha changarawe, naomba Wizara hilo waliangalie sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jingine ambalo ningependa nilikumbushe ni suala zima la upanuzi wa Bandari ya Kilwa Masoko. Kilwa pale tuna bandari, lakini ile bandari imekuwa kama haitumiki ni useless, ipo tu. Sasa Wizara naona kama mmetusahausahau, mfanye upanuzi na ikiwezekana muifanye iwe inatumika sasa. Sambamba na hilo naomba muangalie upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Kilwa Masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kilwa ni Mji wa Kitalii, Mji wa Kilwa ni Mji wa Kitalii, lakini tuna uwanja wa ndege ambao katika bajeti ilisema ingefanya maboresho uwanja ule, lakini hakuna chochote kimefanyika. Naomba tuboreshe ule uwanja, ili basi tuweze kutengeneza fursa ya kupata watalii, Mji wa Kilwa ni Mji wa Kitalii, tuna Mji wa Kale wa Kilwa, tuna Mapango kama ya Nang’oma, tuna Fukwe kwa Mtoni Fumang’ombe na tuna vivutio vingi tu vya utalii, lakini kama uwanja huu ukiboreshwa basi utaweza kuvutia zaidi watalii na hivyo kuifanya Kilwa ipate ustawi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa barabara ya kutoka Nangurukuru kwenda Liwale kwa sasa kuna maeneo bado yanasumbua. Niiombe TANROADS iyashughulikie hayo maeneo, ili basi hiyo barabara iweze kupitika wakati wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ahsante. (Makofi)