Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nichangie kwenye hoja iliyoko Mezani ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote niungane na Taarifa ya Kambi ya Upinzani na ninaiunga mkono kwa asilimia zote, lakini pia ni Mjumbe wa caucus ya Bunge ya Mpango wa Maendeleo Endelevu (SDGS). Na nitapeleka mchango wangu katika sehemu tatu, nitaanza na masuala ya SGR, lakini nitaongelea Barabara ya Dumila – Kilosa – Morogoro – Mikumi, halafu nitaunganisha na masuala ya mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulifanya ziara pamoja na hi caucus yetu ya SDGS kutoka Dar-es-Salaam kwenda Morogoro mpaka Kilosa ambapo mradi huu wa SGR umefika. Tuliona jinsi ambavyo kumekuwa na changamoto mbalimbali katika mradi huu pamoja na sifa nyingi ambazo wenzetu wamekuwa wakizisema, lakini kuna changamoto kubwa sana. Na ninasema naunga mkono Taarifa ya Kambi kwa sababu imejaribu kutoa uchambuzi jinsi gani ambavyo tungeweza kuboresha reli hii ya SGR, ili kuleta manufaa yenye tija kwa Watanzania ambao ndio pesa zao zinatumika mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika SGR tumegundua kwamba, malighafi nyingi zinazotumika zinanunuliwa kutoka nje. Unaweza uka-imagine ukiangalia vitu kama cement pamoja na chuma ambacho kinatumika kwa wingi sana katika mradi huu vyote vinaagizwa kutoka nje. Na maana yake ni kwamba, kama tunaagiza hivyo vitu kutoka nje tunatumia pato letu la Taifa na pesa zote za kigeni zinakwenda kwenye mradi huu. Na ndio maana mara nyingi tumekuwa tukisema tumekuwa hatuna vipaumbele katika nchi yetu kwa sababu, mambo ambayo tunayafanya sasa hivi tungeweza kuyafanya na kuyatambua kwa wenzetu walipopita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunagundua kwamba, katika Awamu iliyopita ya Nne kipaumbele kilikuwa ni Liganga na Mchuchuma kabla sisi wengine hatujaingia kwenye Bunge hili Tukufu tulikuwa tukisikia Liganga na Mchuchuma, Liganga na Mchuchuma, lakini sasa hivi hicho kipaumbele hatukioni kabisa. Mradi wa Liganga na Mchuchuma ungeweza kutumika chuma chake katika Mradi huu wa SGR ungeweza kupunguza gharama za mradi huu na ungeweza kuwana tija zaidi kuliko sasa hivi tunapotumia pesa nyingi za Watanzania katika mradi wa SGR. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imefika kipindi sasa kila mtu anakuja na vipaumbele vyake, imekuwa kama ile hadithi ya zamani kwamba, kuku na yai nani ameanza kuzaliwa na vitu kama hivyo. Ndio maana tunasema ili tuweze kufanikiwa ni lazima tukae chini na tuendeleze yale wenzetu waliyoanza Awamu ya Tano ilipaswa kuendelea na jambo hili la Liganga na Mchuchuma, ili kuweza kufanya Mradi wa SGR uwe na tija zaidi kwa Watanzania wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na kutembelea huko huu Mradi wa SGR umepita katika Jimbo la Mikumi na SGR Makao yake Makuu pale Kilosa yapo katika Kijiji cha Muungano, Kata ya Mabwerebwere katika Jimbo la Mikumi. Kumekuwa na malalmiko makubwa sana ya wananchi wa pale kwamba, pamoja na kwamba, pale ndio imewekwa kambi, lakini pia wale watu hawajapata vile vipaumbele. Tunatambua kwamba, mradi wowote ambao tunakuwa tunasaini lazima vipaumbele viangalie wananchi waliokaa maeneo yale kwa ajili ya ajira na mambo madogomadogo yanayoenda katika ajira zile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye SGR Wananchi wa Kilosa wamekuwa wanalalamika sana kwamba, wanaachwa katika mradi huu, kazi za udereva, kazi zile za kutumia nguvu na vitu kama hivyo, wamekuwa wanawekwa pembeni na kilio chao kimekuwa kikubwa. Lakini pia, tulitegemea kutakuwa na kipengele katika mkataba wowote tunajua kuna kipengele kile ambacho kinahusu social responsibilities na vitu kama hivyo, lakini tumeona CSR katika mradi huu katika maeneo ya Mikumi na Kilosa yamekuwa hayazingatiwi kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu, Wananchi wanaokaa pale Mabwerebwere wana changamoto nyingi mradi huu tunategemea kwamba, walivyokuwa pale wangeweza kuwasaidia kwenye masuala ya shule ambapo Wananchi sasahivi wanalalamika na wanachangishana mia mbili mia mbili kwa ajili ya kujenga shule, wana changamoto kubwa ya maji, wana changamoto kubwa ya zahanati. Tulitegemea mradi mkubwa kama huu ungeweza kurudisha kidogo kwa wananchi wa maeneo yale ambao waliacha mashamba yao na vitu vingine mradi huu uweze kupita, lakini wamekuwa na kilio kikubwa sana kwa kusahauliwa na mradi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, mradi huu umepita katika Kijiji kinaitwa Umunisagala. Hawa watu wa Umunisagala wamekuwa wakilia na malalamiko yao yamekuwa makubwa sana kwa sababu, nao wamesahaulika katika mradi kama huu na wamesahaulika kwa sababu, wametoa ardhi yao. Reli ya zamani ile meter gauge ilikuwa inapita pale, lakini sasahivi SGR imepita eneo lingine kwa sababu ya kukwepa mmomonyoko wa ardhi pamoja na mafuriko ambayo yanatokea maramara kwa hiyo, wamechukua eneo kubwa la Kijiji cha Umunisagala, lakini hawajawazingatia katika masuala mengine ya kijamii kama hayo ya shule, zahanati, maji na vitu vingine kama hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilitegemea hawa wakandarasi ambao wanahusika Yapi Merkezi wangeweza kutoa japo kidogo ili kuweza kuwapoza wananchi wa maeneo yale nao wajisikie kwamba, wana ownership ya mradi ule maana tunaamini kabisa, ili tufanikiwe tunahitaji kuwa na ujirani mwema kati ya wawekezaji pamoja na wananchi wanaoishi maeneo haya. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali izingatie sana kuwaangalia Wananchi wa Wilaya ya Kilosa ambao wengi wamebomolewa nyumba zao, mradi umepita huko; Polisi imebomolewa na ratiba inaonesha kwamba, hata viwanja vya michezo vitabomolewa, itapita reli hii. Sasa hawa watu lazima tuwafikirie na tuwe na jinsi ya kuwa-compensate ili waweze kukaa na kupenda mradi kama huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nizungumzie suala la reli. Wakati tumeenda kwenye ziara ya SGR pale Kilosa nilizungumza na Mkurugenzi wa Reli Tanzania kwa sababu kulikuwa na changamoto kubwa sana Wananchi wa Mikumi, Kidodi pamoja na Ruaha waliwekewa alama za X kwa muda mrefu. Na pia kulikuwa na reli ya zamani iliyokuwa inatoka kwenye kiwanda cha Sukari Kilombero pale Ruaha inaenda mpaka Kilosa na kubeba mizigo kupeleka sehemu nyingine, kwa kweli, ile reli imekwisha hata mataluma hayapo. Na tulipoongea na Mkurugenzi kwa nini watu wamewekewa reli kama wana nia ya kufufua, walituambia bado hawajapata mtu wa kuweza kuwawezesha kutengeneza hiyo reli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini leo ninavyoongea hapa leo watu wa reli wamekuja pale Mikumi kuna maeneo ya kikwaraza Mji Mdogo wa Mikumi ambao ni Mji wa Kitalii wameweka na wameweka barrier wamezuia wananchi wasipite na magari yao kwenda kwenye maeneo ya Kikwaraza, maeneo ya Tambukareli ambayo kwa kweli ni sehemu ambayo ardhi yake sasa ndio wawekezaji wengi wa masuala ya Campsite wamenunua maeneo hayo. Kama mnaona kwenye Tv kuhusu Mji Mpya wa Mikumi ni maeneo hayo ambayo watu wa reli leo wameziba na kuzuwia Wananchi wasiende. Sasa unaona watu wa Campsite wanashindwa kuwekeza kwenye Mji wa Kitalii. Tutapata wapi pesa za utalii kama tunaanza kushindwa kuwekeza na kuweka vitu vizuri katika mpangilio kama huo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana watu wa reli waliangalie hilo. Huo Mji Mpya wa Mikumi unahitaji sana kuweza kuzingatiwa na kutoa nafasi kwa Wananchi, ili waweze kuwekeza zaidi kwenye jambo la utalii ambalo litaongeza uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hilo tangu nimeingia kwenye Bunge lako Tukufu nilikuwa nikizungumzia Barabara ya Dumila – Kilosa – Mikumi. Hii ni barabara ya kilometa 142 na ilikuwa ni ahadi ya tangu Rais Jakaya Mrisho Kikwete, Awamu ya Nne na alipokuja Rais Dkt. Magufuli pia kwenye kampeni zake aliahidi kuijenga kwa lami. Nashukuru nimeona kwamba, kuna bilioni mbili zimetengwa, lakini bado kuna nafasi kubwa sana ambayo bado haijazingatiwa maana katika kilometa 142 zilizojengwa kwa lami ni kilometa 45 tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwenye kitabu cha Waziri katika ukurasa wa katikati hapa 166 inaonesha kwamba, watatengeneza kwa kilometa 20 tu, lakini awamu hizi zilisema kwamba, itatoka Dumila mpaka Ludewa kwa kilometa 45 halafu itatoka Ludewa mpaka Ulaya halafu ikitoka Ulaya itamalizia Mikumi, lakini wamesema watatengeneza kilometa 24 tu ambazo zitatoka Ludewa mpaka Kilosa. Sasa ninataka Waziri akija atuambie ni lini wataanza kujenga awamu ya kilometa 78 kutoka pale Kilosa mpaka Mikumi ambapo kuna kata nyingi zipo katikati zinazotegemea barabara hii kwa ajili ya kujenga uchumi kwa Wananchi wa Wilaya ya Kilosa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kata ambazo ziko njiani katika barabara hii ya kilometa 78 ni Kata ya Magomeni, Kata ya Masanze, Kata y Zombo, Kata ya Ulaya, Kata ya Muenda na Kata ya Mikumi. Unaweza ukaona jinsi ambavyo kama barabara hii itatengenezwa itaweza kusaidia na ku-boost uchumi wa Wananchi wa Mikumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine nilitaka nizungumze kuhusu mawasiliano. Niliuliza swali wiki mbili zilizopita na Naibu Waziri alinijibu kwamba, hawawezi kupeleka mawasiliano kwenye vijiji ambavyo vina mtandao wa aina moja, lakini hivyo vijiji nilivyovitaja havina mtandao kabisa katika Jimbo la Mikumi na niko mbioni kuandika barua kukuletea Naibu Waziri, ili uweze kuona vijiji ambavyo namaanisha. Vijiji hivi vipo kwenye Kata za Vidunda maeneo ya Chonwe, Naudung’u, Itembe, lakini Kata ya Kisanga, kuna Kata ya Tindiga, Malangali kule kwa Lukwambe pamoja na Malui, lakini Uleling’ombe, maeneo ya Mlunga na Lengewaa, lakini pia kuna maeneo ya Masanze, Munisagala, Chabina na Dodoma Isanga, lakini pia kuna Kata ya Muenda ambapo bado mawasiliano hayajafika katika maeneo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimuombe sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kuwa ulisimama na kunijibu hapa na kusema bado unaendelea na tathmini na nia yenu ni kuleta mawasiliano kwa Wananchi wa Jimbo la Mikumi, mtusaidie kuzingatia maeneo haya ambayo yanahitaji sana mawasiliano kwa ajili ya uchumi wao. Asante sana. (Makofi)