Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na team yake kwa ujumla kwa kazi kubwa wanayoifanya. Mwenyezi Mungu awabariki sana ADDS - Head Radiology.

Mheshimiwa Naibu Spika, Lushoto ni Wilaya isiyopungua takribani watu 800,000 na wote hawa wanategemea Hospitali ya Wilaya. Cha kusikitisha, hospitali hii haina huduma muhimu kama X-Ray mashine na hii imesababisha wananchi wengi kukosa huduma hiyo na ukizingatia wananchi wengi hawana uwezo wa kwenda mbali kupata matibabu. Kwa hiyo, naomba Serikali yangu Tukufu ipeleke X-Ray mashine ili wananchi wa Lushoto waweze kupata huduma hiyo kuliko iliyo sasa, kwani wananyanyasika mno.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuhusu maendeleo ya jamii. Suala la huduma kwa wazee imekuwa ni mtihani sana, kwani wazee hasa wa Lushoto wanapata adha kubwa kwa kukosa vitambulisho, hasa wale ambao wapo vijijini ambako hakuna hata zahanati.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hayo, kuna wananchi wengi wanaoishi vijijini, hata wale ambao wanauhitaji maalum pamoja na walemavu hawapati mahitaji yao kabisa. Kwa hiyo, naiomba Serikali yangu ipeleke dawa na vifaa tiba vyote vinavyohusika kwa watu hawa, ukizingatia vijijini hakuna zahanati wala kituo cha afya. Kwa mtaji huo, sasa Serikali itumie magari ya afya ili kufikisha huduma hii kwa walengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Lushoto ni Wilaya yenye milima, kwa hiyo, hata wananchi wakitaka kufuata huduma za afya, ni lazima wafunge safari ya siku mbili au tatu hasa ikitokea mgonjwa amezidiwa na anahitaji usafiri wa gari. Hii imepelekea wagonjwa wengi kupoteza maisha hasa kwa akina mama wajawazito. Kwa hiyo, naiomba Serikali yangu Tukufu tuangalie watu wa Jimbo la Lushoto hasa kwa Kituo cha Afya Mlola tuweze kupata gari la wagonjwa, kwani kwa sasa hali ni mbaya, wagonjwa wanapoteza maisha kila siku kwa ajili ya kukosa gari la wagonjwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, naishukuru Serikali yangu Tukufu kwa kutupatia shilingi milioni 700 kwa ajili ya kujenga majengo matano na vifaa tiba. Kwa sasa majengo yemekamilika, kwa hiyo, tunahitaji sasa vifaa tiba ili kituo chetu kianze kufanya kazi; na kwa kuwa mmeshatutengea fedha, shilingi milioni 300, naomba Serikali yangu ipeleke vifaa hivyo ili kuwahisha huduma kwa wananchi na kupunguza msongamano katika Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna upungufu mkubwa wa Watumishi wa Afya katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto pamoja na kwenye Vituo vya Afya na Zahanati zetu. Mfano, sasa hivi Jimbo la Lushoto nina zahanati zaidi ya sita, zote zimekamilika, zinahitaji vifaa tiba pamoja na watumishi. Hivyo basi, naiomba Serikali yangu ipeleke vifaa tiba pamoja na watumishi katika zahanati zilizopo katika Jimbo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, Lushoto kulikuwa na hospitali kwa watu wanaopatwa na vichaa ambayo ilikuwa inamilikiwa na Kanisa, lakini huduma ile kwa sasa haipo. Kwa hiyo basi, naiomba Serikali yangu ione ni jinsi gani ya kufufua huduma ile muhimu, maana sasa hivi watu wenye ugonjwa huo wana pata taabu kusafiri umbali mrefu; na kama inavyofahamika watu wenye kupatwa na ugonjwa wa kichaa kumsafirisha inakuwa ni shida sana. Nisisitize tana Serikali yangu irudishe ile huduma ya kituo cha watu wenye ugonjwa wa kichaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.