Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu ya Afya. Kama inavyojulikana ni ngumu sana nchi yoyote kupata maendeleo kama wananchi wake hawana afya bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, Watumishi wa Afya; pamoja na jitihada za kujenga mahospitali na vituo vya afya, lakini tumekuwa na upungufu mkubwa sana wa watumishi wa afya nchini. Mfano mpaka mwezi Machi, taarifa za Wizara zinaonesha zina upungufu wa watumishi kwa asilimia 48 na hii inaonesha kuwa kasi utoaji wa vibali vya kuajiri uko chini sana ukilinganisha na ongezeko la wagonjwa. Pia, ongezeko hili la ujenzi wa hospitali na vituo vya afya ni vema sana ungekwenda sambamba na ajira mpya za watumishi wa afya sambamba na kuwalipa watumishi wa afya waliopo wanaodai stahiki zao ili kuweza kuongeza tija ya utendaji kazi wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi la magari ya wagonjwa Jimboni Mikumi; Jimbo la Mikumi lina jiografia mbaya sana na katika kata 15 za Jimbo la Mikumi tuna vituo vya afya vinne tu navyo ni kuwa viwili, yaani Kituo cha Afya cha Kidodi na Kituo cha Afya cha Ulaya na vituo vipya vya afya vya Mikumi na Kituo cha Afya cha Malolo. Kwa hali hiyo inasababisha wananchi wengi kufia njiani wakati wanasafirishwa umbali mrefu sana ambapo ni kutokana na ukosefu wa magari ya wagonjwa. Jimbo zima halina gari hata moja la wagonjwa kwenye zahanati zote pamoja na vituo vya afya vyote. Tunaiomba sana Serikali itusaidie magari ya wagonjwa mawili au zaidi ili tuweze kuwaokoa wananchi hawa wa Jimbo la Mikumi, hasa mama na watoto. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, Dada Ummy Mwalimu, atusaidie na kuokoa maisha ya wanawake na watoto wa Mikumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, NHIF; uandikishaji wa Bima ya Afya ya NHIF umekuwa mdogo sana. Mfano, mwaka 2016/ 2017, walisajili 27% tu; mwaka 2017/2018, walisajili 32% tu; mwaka 2018/2019, walisajili 33%; na kusuasua huku kunatokana na ufinyu wa bajeti. Tunaomba sana Serikali izingatie sana bajeti ya afya kwa ujumla. Pia, Serikali iharakishe kuleta Muswada wa Bima ya Afya kwa Wote yaani Universal Health Coverage ili tuweze kuupitisha na kuleta tija zaidi ya kuwasaidia na kuwaokoa Watanzania wengi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuajiri Maafisa Maendeleo ya Jamii; ni vema sasa tukajikita zaidi kwenye kinga kuliko tiba na watu wanaoweza kutusaidia zaidi kwenye jambo hili la kinga ni Maafisa Maendeleo ya Jamii ili waweze kusaidia jamii zetu huko chini ili wapate elimu zaidi ya afya kwani ni kweli tupu kwamba, kinga ni bora kuliko tiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.