Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Wizara ya Afya kwa juhudi inazofanya za kuboresha Sekta ya Afya nchini. Katika Jimbo la Korogwe lenye tarafa tatu na kila tarafa ikiwa na kituo cha afya, tuna gari moja tu la kubebea wagonjwa. Gari ambalo na lenyewe limechakaa sana maana ni la muda mrefu, naiomba sana Wizara kwa unyenyekevu mkubwa watusaidie tupate gari la wagonjwa maana vituo vya afya viko mbali na hospitali.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulipokea fedha za ujenzi wa Kituo cha Afya kipya katika Kata za Mkumbara, kituo kimekamilika. Tunaiomba Wizara kwa kushirikiana na TAMISEMI kutupatia vifaa ili kituo hiki kianze kufanya kazi ya kutoa huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu wa watumishi katika Wilaya ya Korogwe kwa zaidi ya 46%; tunaiomba Wizara kusaidia upatikanaji wa watumishi hawa ili kuboresha huduma za afya wilayani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuboresha na kuratibu vizuri huduma za wazee, ni vyema Serikali ikaandaa Sheria ya Wazee kama ilivyo kwa watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, viko vituo vya afya vya muda mrefu kama Kituo cha Afya cha Magoma na Bungu ambavyo vinahitaji ukarabati na upanuzi. Pamoja na uhitaji wa ukarabati na upanuzi, pia vifaa kama vitanda vimechakaa sana vinahitaji kubadilishwa kama siyo kuongezwa. Naiomba Wizara ianzishe utaratibu wa kuongeza vifaa kwenye vituo vya afya kwa awamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ustawi wa Jamii; viko vituo vya kulelea watoto/makao ya watoto ambavyo havina hadhi ya kuwa makao ya watoto na vingine vinatuhumiwa kwa kashfa mbalimbali kama unyanyasaji na ukatili wa kijinsia na Maafisa Ustawi walioko wilayani baadhi yao siyo waaminifu, ni vyema Wizara iimarishe utaratibu wa ukaguzi wa makao ya watoto.