Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Wizara ya Afya kwa juhudi kubwa zinazoonekana za kuongeza na kuboresha huduma za afya na usafi wa mazingira nchini. Hivyo kwa dhati kabisa naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja na kuwatakia utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru sana Serikali kwa fedha za ujenzi wa hospitali shilingi bilioni 1.05 na ukarabati wa kituo cha afya cha Mgori shilingi milioni 400 na Msange shilingi milioni 700. Sambamba na mafanikio haya, tulipata pia usajili wa Hospitali ya St. Carolos Mtinko kuwa Hospitali Teule ya Wilaya. Sambamba na upatikanaji wa dawa kwa kiwango cha kuridhisha, hongera sana kwa Mheshimiwa Ummy na timu yake kwa mafanikio haya katika Jimbo la Singida Kaskazini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mafanikio hakukosi kuwa na changamoto, Jimbo la Singida Kaskazini lina wananchi zaidi ya 250,000 ambapo kwa wastani wa watu 5,000 kwa kituo cha afya tuna uhitaji wa zaidi ya vituo vitatu vya afya ili kuboresha utoaji wa huduma za afya. Hivyo niombe Wizara kwa moyo wa dhati kutusaidia fedha za ukarabati kwa kituo cha afya cha Ilongero na angalau ukamilishaji wa majengo yaliyoanzishwa na wananchi kwa Kata za Ngimu na Makuro ambayo yana zaidi ya miaka nane kusubiri kupauliwa. Ningeshauri kwa hatua ya sasa tuombe shilingi milioni 300 kukamilisha hatua ya awali tukisubiri upanuzi katika awamu zinazokuja.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua pia juhudi za Serikali katika kuongeza Watumishi wa Sekta ya Afya, hivyo niombe sana Serikali kutusaidia watumishi katika Hospitali Teule ya Wilaya (St. Carolos Mtinko) na zahanati na kituo cha afya. Vilevile uboreshaji na usimamizi wa Maendeleo ya Jamii unahitajika maana kuna huduma zisizoridhisha kabisa kwa wananchi hasa vijijini. Hii inatokana na usimamizi usioridhisha na ukosefu wa vitendea kazi ambavyo vimekuwa ndiyo visingizio vya kutokutekeleza wajibu wao. Mheshimiwa Waziri tumefanya kazi kubwa ila tusipoangalia watendaji hawa watatuangusha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa wananchi tutaendelea kushiriki katika miradi ya maendeleo inayopata fedha kutoka Serikalini na kuendelea na ujenzi wa zahanati katika vijiji vyetu ili kuunga mkono juhudi za Serikali kuboresha hali ya huduma nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.