Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi hii kuweza kuchangia hotuba ya Wizara ya Afya. Awali ya yote, niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa ambayo anayoifanya akisaidiana na wasidizi wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara hii ni muhimu imefanya kazi karibu maeneo yote ya nchi yetu. Mkoa wa Katavi hatuna Hospitali ya Mkoa. Mheshimiwa Waziri anafahamu na fedha ambazo zimetengwa na Wizara ni kidogo sana. Tulikuwa tunaomba Mheshimiwa Waziri aangalie mazingira ya Mkoa wa Katavi aongeze fedha ili tuweze kujenga Hospitali ya Mkoa ambayo itasaidia kutoa huduma ya afya kwenye maeneo ya mkoa na kutoa huduma za afya kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kutoa fedha za ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Tanganyika, imepata shilingi bilioni moja na nusu kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali Tanganyika. Hilo tunawapongeza sana Wizara kwa kazi kubwa na Mheshimiwa Waziri na timu ya wataalam ambao wametoa hizo fedha kwa ajili ya kutoa huduma. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri aendelee kutusaidia kwenye Vituo vya Afya ambavyo viko kwenye maeneo husika. Nilishamwomba Kituo cha Afya cha Nyagala, naamini anakikumbuka, naomba sana hiki Kituo akiwekee kipaumbele kwa ajili ya kuwapa wananchi wa eneo hilo. Walishaanza hatua za awali, wamejitolea, wamejenga baadhi ya majengo, kwa hiyo tunategemea Mheshimiwa Waziri kwenye fedha atakazozipata, atusaidie kituo hicho ili tuweze kuwasaidia wananchi wa eneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambasamba na hilo, tunaipongeza Serikali kwa kujenga Vituo vya Afya vya Mwese na Mishamo. Kwenye hivyo vituo viwili ambavyo vilitolewa fedha na Serikali upo upungufu ambao tunahitaji Wizara isaidie. Tunaomba vifaa tiba, kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Mwese, tunaomba vifaa tiba kwa ajili ya Kituo cha Mishamo. Naamini tukipata hivyo vifaa tiba vitawasaidia kutoa huduma iliyo nzuri na wananchi wakanufaika na kile kilichoelekezwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri kwenye maeneo ambayo alifika Mheshimiwa Waziri, alifika eneo la Kituo cha Afya cha Karema, eneo lile tunahitaji watusaidie watupatie ambulance, yeye aliahidi na alifika akaona mazingira yalivyo, kwa hiyo tunaomba kumkumbusha Mheshimiwa Waziri ahadi ambayo aliwapa Wanatanganyika, eneo lile la Karema aweze kukamilisha ili aweze kuwasaidia wananchi kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, tunaomba Madaktari na vituo vya afya, zahanati na hospitali inayojengwa sasa inahitaji wahudumu wa afya, Wilaya ya Tanganyika ina Daktari mmoja tu. Naomba kwenye bajeti hii, aangalie uwezekano wa kupeleka wataalam watakaotoa huduma kwenye vituo vya afya. Vituo vya afya hivyo vilivyojengwa ni vizuri, lakini vina tatizo la wahudumu ambao wanaweza wakatoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na naendelea kumpongeza kwa kazi nzuri ambazo anazifanya. Ahsante. (Makofi)