Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi name nichangie hoja iliyoko mezani. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai, lakini bado naendelea kuwashukuru wananchi wa Urambo kwa kunipa ushirikiano. Nami niungane na wenzangu kuipa pole familia iliyoondokewa na Mzee wetu, Marehemu Reginald Mengi, naomba Mwenyezi Mungu aiweke roho yake mahali pema Peponi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawajibika kuishukuru sana Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee na kadhalika kwa jinsi ambavyo wanachapa kazi katika Awamu hii ya Tano. Namwomba Mwenyezi Mungu awabariki sana Mheshimiwa Ummy mwenyewe ambaye anathibisha wanawake wanaweza. Pia nampongeza Mheshimiwa Dkt. Ndungulile kwa namna anavyochapa kazi na Mwenzie. Nampongeza pia Katibu Mkuu, Dkt. Chaula, kwa kweli hawa watu wanafanya kazi wakisaidiwa na wafanyakazi. Mwenyezi Mungu awapeni nguvu, endeleeni kuchapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni shukrani kwa niaba ya wananchi wa Urambo kwa kumaliziwa Kituo cha Afya cha Usoke. Naishukuru sana Serikali kwa kutupa shilingi milioni 400 kwa kumalizia Kituo cha Afya cha Usoke na sasa hivi wametuongezea kimoja ambacho kinaendelea kujengwa katika Kata ya Uyumbu Usoke Mlimani.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya shukurani hiyo, naomba niielezee Serikali kwamba sisi kama Urambo tuna kata 18. Maana yake ni kwamba kituo hiki cha pili kikimalizika tutakuwa na vituo viwili vya afya. Ni ombi kwa niaba ya wananchi wa Urambo kwamba tuongezewe kituo cha afya angalau katika Kata ya Songambele; na ikiwezekena hata viwili katika kata pia ya Vumilia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni jambo la uwazi kwamba sisi kama Urambo bado tunahudumia Wilaya ya Kaliua ambao bado; ukienda kwenye wodi ukitembelea wagonjwa waliolazwa utashangaa, wengi wanatoka Kaliua, wengine wanatoka kwa jirani zangu Uyui hasa maeneo ya Ndono na mpaka Uvinza sisi tunapata. Kwa hiyo, tunapoomba huduma ya afya kuongezewa ni kwa sababu pia tunahudumia wananchi wanaotoka katika maeneo ya jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe shukrani za pekee kwa Mheshimiwa Waziri Ummy. Alikuja kufanya ziara na ziara yake ilizaa matunda. Tulipoenda Usoke alifurahishwa sana na kazi iliyofanywa pale Usoke ya kumalizia kituo cha afya ambapo ulikuwa ni mradi uliokuwa wa ADB tangu 2010. Mheshimiwa Ummy alifurahi kwa jinsi ambavyo kituo kilimalizwa vizuri na akaahidi kwamba majengo mengine ambayo yapo yanaharibu sura ya kituo kile kwamba atatoa shilingi milioni 50. Mheshimiwa Waziri tunashukuru sana kwa ahadi yako, naamini itatimizwa tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Kituo cha Afya cha Usoke kilikuwa ni mabaki ya mradi wa ADB, ADB iliacha mradi mwingine ambao bado haujakamika. Inasikitisha kwamba tangu mwaka 2010 theater ambayo ipo karibu na wodi ya akina mama ilianza kujengwa pale, sasa hivi iko kwenye ngazi ya lenta, kwa kujua kwamba wakitoka pale theater wanaingizwa kwenye wodi ya akina mama. Mpaka leo haijaisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali imalize ilie theater nasi tunaamini kwamba tukipewa shilingi milioni 200 itamaliza hiyo theater ili akina mama ambao wapo karibu, ambao walikuwa walengwa, wakitoka theater pale wanaingia wodini na vice versa, wakitoka wodini wanapelekwa theater. Tunaomba theater ikamilishwe ambayo iko kwenye ngazi ya lenta. Inasikitisha, jengo zuri lakini tangu 2010 halijaisha ambayo itausaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi theater kwa kuwa tunahudumia na watu kutoka maeneo mengine, wengine inabidi wasubiri lakini theater ikiisha wagonjwa, wakiwepo akina mama na watoto watanufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika tuna mradi mwingine ambao uliachwa, ni mradi wa LGDB ambapo ni ICU. Huwezi kuamini Urambo hatuna ICU na ni Hospitali ya Wilaya. Tunaomba kwa heshima na taadhima kabisa Awamu ya Tano itusaidie tuwe na ICU na sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hali kadhalika na X-Ray, nimeshukuru Wabunge wengine wamesimama hapa wanafurahi kwamba tuna X-Ray ya kisasa ya kidijitali, sisi bado tupo kwenye analogy.

Mheshimiwa Naibu Spika, nisaidie nawe kuiomba Serikali itusaidie X-Ray ya kisasa. Kwa sababu hata haya majibu tunayopata sasa hivi tuna wasiwasi nayo, kwa sababu bado tupo kwenye enzi ya Ujima, tunatumia X-Ray ya analogy. Tunaomba tusaidiwe hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hali kadhalika, suala la wafanyakazi ni la muhimu sana. Bado tuna uhaba wa wafanyakazi kwa asilimia 48. Tunaomba nasi mtakapokuwa mkipanga wafanyakazi mtukumbuke nasi Urambo tuongezewe wafanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilifurahi sana ziara ya Mheshimiwa Waziri Ummy. Namwomba Mwenyenzi Mungu ampe afya ili arudi tena aone mabadiliko gani tumeyafanya tangu alipotoka. Kuna maneno mazuri uliyaacha Urambo bado watu wanakukumbuka nayo na hasa pale ulipokumbuka kile Kituo cha Afya cha Uyogo kinachojengwa kwa kushirikiana na Waingereza. Nawe ulitaka kuonyesha kuunga mkono nguvu ya wananchi na marafiki zao kutoka Uingireza ukaahidi shilingi milioni 20. Tushukuru sana kama utawapa shilingi milioni 20 Uyogo ili wamalizie kituo chao.

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya yote, bado wanamkumbuka Mheshimiwa Waziri alipotamka neno la maana sana kwamba atawapa ambulance. Kwa sababu wao wapo mbali na Hospitali ya Wilaya, akiwapa ambulance itawasaidia sana kuwawahisha akina mama hasa wanaokwenda kujifungua usiku, maana yake saa za kujifungua huwa hazijulikani; usiku na kadhalika, ambulance itasaidia sana. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, hali kadhalika Mheshimiwa Waziri alipokwenda zahanati ya Itebulanda, aliahidi nako shillingi milioni 20. Mheshimiwa Waziri tuna imani kabisa utatimiza kwa sababu uliipenda sana ile zahanati, inafanya kazi vizuri na imeanzisha wodi ya akina mama na kwamba utawaunga mkono kwa shilingi milioni 20.

NAIBU SPIKA: Muda wako umeisha Mheshimiwa. Ahsante sana.

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri, nashukuru Wizara nzima na ninaunga mkono hoja. Endeleeni kuchapa kazi. Ahsanteni sana. (Makofi)