Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kipekee kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu, kila tunaposimama hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, natangua tu kutoa pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki kwa kifo cha mpendwa wetu Dkt. Reginald Mengi. Natambua mchango wake hasa kwa sisi watu wenye ulemavu, alitupenda, alituthamini na alitusaidia. Kwa kweli tutamkumbuka kwa mengi. Kipekee kabisa Dkt. Reginald Mengi ataendelea kuishi ndani ya mioyo yetu. Ninamfananisha Dkt. Reginald Mengi na Mama Theresa wa Calcutta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, inshallah Mwenyezi Mungu hapo kesho tutakwenda nasi kujumuika nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze tu kwa kusema kwamba kwa wanafunzi wenzetu wanaosoma Vyuo Vikuu, niombe kwa Wizara kwa sababu kuna utaratibu wa Bima ya Afya ambayo wanakatiwa au wanakata wanafunzi wale na huu ni utaratibu mzuri ambao umeandaliwa na Serikali. Kipekee kabisa nampongeza mwanamke jasiri, shupavu Mheshimiwa Ummy Mwalimu, pamoja na Naibu wako, Katibu Mkuu, pamoja na Watendaji wote kwa kazi nzuri wanayoifanya. Hakika matunda tunayaona na Mwenyezi Mungu aendelee kuwapa Afya ili mwendelee kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Mheshimiwa Waziri kufuatilia Bima za Afya kwa sababu vyuo vingi hapa nchini, pamoja na kwamba wanafunzi wanatoa pesa, lakini hawapati hizo Bima za Afya kwa wakati. Pia wengine wanatoa zaidi ya kile kiwango kinachohitajika, wanatoa shilingi 100,000/=. Hawa wanafunzi wakati mwingine wasipotoa hawaruhusiwi hata kufanya mitihani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamwomba sana dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu alifuatilie hili na hata ikibidi, basi uwe utaratibu wanafunzi wanapoanza mwaka wa kwanza kuwepo na watu wa Bima ya Afya ili waweze kuwakatia vitambulisho kutokana na mikopo wanayopata ili kuondoa usumbufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hili lipo kwa shule za sekondari na hata hizi English Medium, tuwasaidie wazazi. Kama kweli zinatolewa hizo pesa, basi ziweze kukatiwa bima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine pia nizungumzie kuhusiana na Vyuo vya Maendeleo ya Jamii, vingi vimechoka, vimechakaa na vinahitaji ukarabati. Namuomba Mheshimiwa Ummy Mwalimu kuhakikisha kwamba Vyuo hivi vya Maendeleo ya Jamii vinafanyiwa ukarabati. Pia ikiwa ni pamoja na Maafisa Maendeleo ya Jamii kuweza kuwasaidia vitendea kazi ili waweze kufanya kazi ambayo wamepatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakemea pia baadhi ya Wahadhiri wa Vyuo Vikuu na hili hata Mheshimiwa Rais pia amelizungumza, baadhi ya Wahadhiri wa Vyuo Vikuu wanaowanyanyasa watoto wa kike kingono na wamediriki wakati mwingine hata kuwafelisha kwa sababu tu wamekataliwa kingono, tumefika mahali pabaya sana. Namwomba Mheshimiwa Waziri yeye ni Waziri pamoja na afya lakini jinsia, alisimamie hili kuwanusuru watoto wetu wanaokwenda shule ili waweze kusoma kwa amani na utulivu kama nchi yetu ilivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitalizungumzia kwa mapana zaidi suala la mapambano dhidi ya UKIMWI. Hali ya mapambano dhidi ya UKIMWI ni mbaya. Takwimu zinazoooneshwa na zimesomwa hapa, hivi sasa kila mwaka watu 72,000 wanaambukizwa virusi vya UKIMWI na ni kati ya miaka 15 mpaka 64. Miaka kuanzia 15 mpaka 24 hao ni vijana ambao maambukizi yako kwa asilimia 49 na kati ya hao ni watoto wa kike ndio wameathirika, tunalipeleka wapi Taifa letu? Nchi yetu tunasema nchi ya viwanda na viwanda tunategemea pia hata hawa ambao wako vyuoni waje kwenda kule, je, vijana hawa ambao hivi sasa wapo katika janga la maambukizi ya virusi vya UKIMWI tunawasaidiaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha atuambie ni mkakati upi unaandaliwa ili kuona kwamba tunanusuru maisha ya watoto wetu na hasa watoto wa kike, ndio ambao wanaangamia kwa kiasi kikubwa. Naomba sana tuone ni kwa jinsi gani tunawasaidia, leo hii tunasema kwamba mpaka tunapomaliza siku watu 197 wanaambukizwa virusi vya UKIMWI. Hili sio jambo la mzaha ni jambo kwa kweli pamoja na jitihada nzuri za Serikali na hasa kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu na mimi nikiwa kama Mjumbe wa Kamati ya UKIMWI na Dawa za Kulevya na bahati nzuri na Kifua Kikuu hali ni mbaya huko tunakokwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo utaratibu ambao tunafanya kampeni kwenye shule zetu, lakini maeneo mengi wale wahusika wamejisahau, tunaomba wawakumbushe ili tuone ni kwa jinsi gani basi kama ni kampeni au ni jinsi gani ya kuweza kukinusuru kizazi hiki ili kiepukane na hili janga la UKIMWI. Mimi naumia sana kama mwanamke, watoto ambao tunawategemea kwamba ndio viongozi tukiondoka hapa, wanakwenda chuo wanakwenda shule, wakirudi badala yak u-graduate na A wanarudi na virusi vya UKIMWI. Hili linaumiza sana, namwomba Mheshimiwa Waziri pia na Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na hizo jitihada na nipongeze sana pia Serikali yetu kwa jinsi ambavyo inalichukilia suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa kondomu hazipatikani, Mheshimiwa Waziri atakapokuja naomba atuambie ni kwa nini kumekuwa na uhaba mkubwa wa kondomu na pengine hili ndilo linalosaidia au linalochangia kuendelea kuenea kwa maambukizi ya virusi vya UKIMWI, tujue ni idadi ngapi pia wanapokea kwa mwaka hizo kondomu, kwa sababu najua siku za nyuma walikuwa wanapokea zaidi 18,000, lakini ni taarifa zilizopo ambazo Mheshimiwa Waziri atakuja kutuambia walipata kondomu 9000. Je, tatizo liko wapi, atueleze Mheshimiwa Waziri ili tuweze kunusu kizazi hiki ambacho kinaangamia na ugonjwa huu wa UKIMWI?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia malengo haya ya 90, 90 kwa kweli Serikali inafanya kazi kubwa, lakini watendaji kule chini bado ni tatizo. Tulipokwenda kwenye kampeni baadhi hawajui unapomwambia 90, 90 anakwambia ni kitu gani na wakati mwingine ni mtu mwenye dhamana ya kuweza kusaidia katika hili. Kwa hiyo, naomba sana kwa kweli, mimi nalia sana na UKIMWI na hasa watoto wa kike tuone ni kwa jinsi gani tutawasaidia watoto wetu ili kuwaepusha na huu ugonjwa wa UKIMWI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, nimalizie tu kwa kusema kwamba, unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake bado pia hili ni tatizo katika maeneo mengi. Mwisho kabisa niseme kwamba, kazi nzuri inayofanywa na Wizara hii tunaiona na Mheshimiwa Ummy anaacha alama katika Wizara hii pamoja na Naibu wake. Kikubwa tunachokifurahia na tunaona kabisa kwamba kazi nzuri ya Mheshimiwa Rais kwamba yupo hapo lakini Dkt. Ndugulile, ni Daktari, kwa hiyo hakuna mtu atakayeweza kuwadanganya katika Wizara. Tunawaomba sana waendelee kusaidia na kuhakikisha kwamba vituo vya afya ambavyo Serikali hii ya Awamu ya Tano imeviboresha, basi tuone vifaa vinapelekwa ili tuweze kupunguza tatizo la vifo vya wanawake na watoto kwa sababu hawa wanawake ndiyo nguvu kazi ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, kwa mara nyingine tena, tuendelee kumwombea Dkt. Reginald Mengi. Pia tujiulize kwa sababu tunao matajiri wengi, sisi wenyewe binafsi je, tunasaidiaje watu wenye uhitaji? Katika maeneo mengi tunao tunawaona na wana shida ambayo kweli wanahitaji kusaidiwa na hata matajiri waliojaliwa tunawasaidiaje, tunaacha alama gani, Dkt. Reginald Mengi, kilio cha Watanzania na huko anakokwenda basi Mungu anaona. Kwa hiyo na sisi iwe ni somo kwetu ni jinsi gani tunakwenda kuwasaidia Watanzania wenye uhitaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana, nampongeza sana Mheshimiwa Ummy pamoja na Mheshimiwa Dkt. Ndugulile, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote Wizarani, waendelee kuchapa kazi, tuko pamoja na wao, a luta continua, mapambano bado yanaendelea. Ahsante sana. (Makofi)