Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama mbele yenu tena na kutoa mchango wangu katika hoja hii iliyopo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukushukuru wewe mwenyewe binafsi, Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Spika, Wenyeviti wote wa Bunge kwa uwezo na umahiri mkubwa mnaoonesha katika kuliendesha Bunge letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii pia kumpongeza kwa dhati Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa kwa umakini wake wa kusimamia shughuli za Serikali. Aidha, napenda kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliopata fursa ya kuchangia hoja yetu iliyowasilishwa hapa Bungeni. Kwa kweli michango ni mizuri na imejaa hekima kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, michango na changamoto nyingi zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge kuhusu Sekta ya Maji. Hii ni kwa sababu Sekta ya Maji kama tunavyofahamu maji ni uhai, maji ni afya, maji ni kilimo, maji ni uchumi, maji ni viwanda, maji ni ustaarabu na maji ni kila kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba yangu imechangiwa na wachangiaji 173 ambapo wachangiaji 59 wamechangia kwa maandishi na wachangiaji 88 wamechangia kwa kuzungumza. Kama nilivyosema hapo mwanzoni, michango ya Waheshimiwa Wabunge wote ilikuwa ni mizuri sana na ilivyosheheni mapendekezo, ushauri, busara na namna bora ya kuendeleza Sekta ya Maji. Aidha, siyo rahisi kujibu hoja zote za Waheshimiwa Wabunge kwa kina na kutosheleza kwa muda huu mfupi nilionao. Naahidi kwamba hoja zote tutazichukua, tutazifanyia na tutazijibu kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite kwenye maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza ambalo nitaanza kujikita ni usimamizi wa miradi. Naamini kwamba changamoto namba moja sasa hivi ya Wizara ya Maji ni usimamizi wa miradi. Tumekuwa na changamoto kubwa ya usimamizi wa miradi ya maji na changamoto hii imeanzia Halmashauri kwa Engineer wa maji, ikaja kwa Engineer wa Mkoa mpaka ikafika Wizarani, ni changamoto kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hii kuna maeneo mawili; eneo la mwanzo la usimamizi linahusiana na viwango na ubora wa miradi. Changamoto hii ni kihistoria, ilianzia toka mwaka 2010; miradi mingi iliyojengwa kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji ilijengwa kwa viwango vya chini. Miradi hiyo ilitekelezwa kati ya mwaka 2010 – 2015, tume nyingi zimeenda kuchunguza miradi hii na imethibitisha kwamba miradi hiyo ilijengwa chini ya viwango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi mingi ya kipindi hicho ndiyo yenye changamoto ambazo sasa tunapambana nazo na ni lazima tuna jukumu na tumepewa jukumu la Tanzania lazima tutatue tatizo hili na tuwapelekee Watanzania maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi iliyoanza kujengwa mwaka 2017 kwa kiasi kikubwa changamoto hizi zimepungua. Hii imetokana na ufuatiliaji wa karibu sana wa viongozi wa Wizara ya Maji, ninyi nyote mmekuwa mashahidi, kila leo mnaona viongozi wa Wizara ya Maji wanatembelea maeneo mbalimbali ya nchi yetu kuangalia miradi ya maji. Nawashukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na viongozi wote kwa kufanya kazi hii ya kuhakikisha kwamba miradi ya maji tunayojenga inaenda kwa viwango vinavyokubaliwa ili Watanzania waweze kupata maji safi na salama, hilo eneo la mwanzo ambalo kwa kiasi kikubwa sasa hivi wakandarasi wameanza kuogopa na tumeweza kwenda nao vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo ni tatizo na bado ilikuwa ni changamoto ni gharama halisi ya miradi ya maji. Gharama ya miradi ya maji iko juu sana, huku ndiko wakandarasi wengi wanakojificha na kupiga pesa za Serikali. Hii inafanywa kwa ushirikiano mkubwa kati ya wakandarasi wetu, Halmashauri, Wakurugenzi, Wahandisi wa Maji Mikoani, Wahandisi wa Maji wa Wizara ya Maji yenyewe, Idara ya Manunuzi, Wizara ya Maji pamoja na Mfuko wa Maji. Kumekuwa na mtandao mkubwa sana ambao unaanzia kule kwenye Halmashauri, Mkoani hadi Wizarani, hili jambo halikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mtandao huu, Wahandisi wetu wa Maji wa Wilaya wanatengeneza engineering estimation au makisio ya kihandisi ambayo si sahihi, wanaweka gharama za juu. Ubaya zaidi wanajaribu kuwapa wakandarasi wazijue kabla ya tenda. Hili ni jambo baya, siyo uadilifu na halikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mifano miwili ambayo ipo ambayo inaonesha jinsi gani pesa za Serikali zinaliwa kwa mtindo huu. Sitataja jina la mradi lakini kuna Project A (Mradi A), mradi huu ulitangazwa, mkandarasi akaomba na akatoa bei yake ni shilingi bilioni 4.5. Sisi baada ya kupitia mradi huu vizuri tukaona unaweza kujengwa kwa bilioni shilingi 2.4.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuchambua vizuri, nikiwaonyesha hapa, hii ndiyo bei ya mkandarasi nah ii ndiyo bei tuliyofanya uchambuzi wetu, baada ya kupitia tuliona kwanza kwenye mabomba alisema bei ya mabomba ni shilingi bilioni 2.77, sisi baada ya kufanya utafiti tukaona bei ya bomba ni shilingi bilioni 1.13, karibuni mara mbili. La pili, tumeenda tena tukaangalia baadhi ya maeneo kwa mfano ujenzi wa tenki yeye ame-quote milioni 488, sisi tuka-quote milioni 771. Sasa huku ndiko wakandarasi wengi wanakopiga pesa na mtandao huu unaanzia Halmashauri mpaka Wizarani. Watu wengi wanapiga hela kwa kutumia utaratibu huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumaliza hapo mkandarasi huyu tukasema hatufai. Tulilofanya tukasema sasa pesa ile ambayo tulikuwa tumpe mkandarasi huyu tutumie utaratibu wetu sisi tukajenge kazi hiyohiyo kwa shilingi bilioni 2.5 ama 2.6 lakini pesa nyingine tupeleke kwenye miradi mingine, kwa mfano tujenge mradi wa Kamwanda kule kwa Mheshimiwa Serukamba ambao ni shilingi milioni 811. Pesa iliyobaki tunaweza pia kujenga mradi wa Horohoro ambao ni takribani shilingi milioni 350. Pesa ambayo tume-save kwenye mradi huu kwa kutokumpa kazi mkandarasi yule tunaweza kujenga mradi wa Tunduma kwa shilingi milioni 500. Kwa kweli watu wengi wanapiga pesa kwenye miradi ya maji kwa njia hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatukusimama hapo, tulikwenda kuchukua mradi wa pili, mkandarasi huyu aliomba kazi hii kwa shilingi bilioni 1.6, baada ya kufanya mahesabu vizuri tukaona kazi ile inaweza kujengwa kwa shilingi takribani milioni 800 mpaka bilioni 1, hapa kuna takribani shilingi milioni 600 zingeliwa na mkandarasi. Pesa hizo tukizitumia tunaweza kuchimba takribani visima virefu 30 ambapo Wabunge wengi hapa wana shida ya visima hivyo. Kwa kweli kuna changamoto kubwa Wizara ya Maji na tumejipanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuona tatizo hilo, tukaenda tena mbali tukaangalia miradi kama mitatu, minne tukaona tatizo ndiyo hilohilo. Sasa tulifanya nini kama Wizara. Kuna mambo ya msingi tulifanya, hatua ya mwanzo tuliyochukua, tulifuta vibali vya miradi yote husika na tukaja na utaratibu mpya wa kutafuta mkandarasi na mkandarasi huyu tutatumia Mamlaka yetu ya Maji ambayo itafanya kazi nzuri na kwa bei nafuu na kwa muda mfupi kuliko mkandarasi yule aliyekuwa amependekezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya pili tuliyochukua ni kuondoa watumishi 14 ndani ya Wizara ya Maji kwa muda wa wiki mbili. Watumishi watano (5) tumewaondoa Idara ya Maji Vijijini; watumishi watatu (3) Idara ya Manunuzi au Sekta ya Manunuzi; tumemuondoa Mkurugenzi wa Manunuzi, Msaidizi wake na mtumishi mmoja; tumeondoa watumishi watatu kwenye Mfuko wa Maji na Bodi yote ya Mfuko wa Maji tumeiondoa kwa sababu hivi ndivyo vilikuwa vichochoro vya kupigia pesa za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kuwa tumejipanga kusafisha. Ni lazima wafanyakazi wote wa Wizara ya Maji wabadilike, lazima wafanye kazi kwa uadilifu na weledi mkubwa. Wakati wa kupiga Serikali sasa imetosha, haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo tumefanya ni kuimarisha idara mbalimbali za Wizara ya Maji. Tumeimarisha Idara ya Maji yenyewe kwa kuunganisha maji vijijini na mjini; tumeboresha Kitengo cha Manunuzi, tunaboresha Mfuko wa Maji na tunaboresha Kitengo cha Usanifu ambapo penyewe pana matatizo makubwa. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwa ujumla kuwa Wizara ya Maji itabadilika, lazima ibadilike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kila siku watu wanakaa ofisini wanapiga pesa lakini Watanzania wetu wanapata taabu ya maji safi na salama, hii haiwezekani. Imetosha, lazima tujipange, aliyekuwa hawezi kufanya kazi hii anaondoka. Kama ni Mkurugenzi, kama ni nani, wote wanaondoka, lazima Wizara ya Maji inyooke. (Makofi/ Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuboresha hilo, tumesema sasa Wizara ya Maji lazima tuje na mpango wa kujua gharama za miradi ya maji. Kwa mfano, tunalofanya sasa hivi tunataka kujua unit cost kwa kila mradi, ukijenga tenki pengine la lita milioni mia moja itatumia shilingi ngapi, tunataka kuleta kitabu ambacho kitaonesha bei halisi za mradi wa maji ambapo Wahandisi wetu wa RUWASA na wengine wote watatumia kitabu hicho kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunapata thamani ya pesa tunayoingiza kwenye miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo tunafanya maboresho makubwa ni uanzishwaji wa RUWASA (Wakala wa Maji Vijijini. Kama Mheshimiwa Naibu Waziri alivyosema, kama Waheshimiwa Wabunge walivyosema kwamba Wahandisi wa Halmashauri ni tatizo, sasa tunakuja na RUWASA, wafanye kazi pale, tuhakikishe kwamba tunapata thamani ya miradi tunayotekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo kila Mhandisi anayetoka Halmashauri tutampeleka RUWASA. Kazi tutakayoifanya tutahakikisha tunafanya upekuzi wa kina kwa Wahandisi wote wanaotoka Halmashauri, hatutaki kupeleka watu wapigaji kwenye RUWASA hii mpya tunayoianzisha. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, tatizo la maji litamalizika na tumejipanga kuhakikisha kwamba tatizo la maji linakwisha na wananchi wetu wanapata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine nalotaka kuchangia ni kuhusu upatikanaji wa fedha. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, Fungu Na.49 - Wizara ya Maji, iliidhinishiwa bajeti ya maendeleo shilingi bilioni 673.214. Hadi kufikia mwezi Aprili, 2019, jumla ya shilingi bilioni 343.486 zilipokelewa. Tarehe 30 Aprili, 2019, Wizara ilipokea tena shilingi bilioni 56.26 ambapo shilingi bilioni 12 ni za Mfuko wa Maji na shilingi bilioni 44 ni pesa kutoka Serikali Kuu ama Hazina. Mpaka kufikia tarehe 30 Aprili, 2019, Wizara ilipokea shilingi takribani bilioni 400.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwenendo wa madeni ya wakandarasi. Kama alivyoongea Naibu Waziri, hadi kufikia mwezi Aprili, Wizara ilikuwa na certificates za miradi mbalimbali yenye thamani ya shilingi bilioni 78.67. Baada ya kupokea fedha hizo, shilingi bilioni 56.256 ambazo kwa sasa tunaendelea kuwalipa wakandarasi hao, deni la certificates limepungua kwa asilimia kubwa sana na certificates tunazozipata sasa hivi tunazifanyia uhakiki ili tuhakikishe nazo zimeenda sawa baadaye tuanze kuzilipa mwezi Juni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kukuhakikishia wewe na Bunge lako Tukufu itakapofika mwezi Juni wakandarasi wote watakuwa hawatudai. Hata hivyo, naomba muelewe kwamba kila siku wakandarasi wanazalisha certificates kwa sababu kazi zinaendelea site, lakini tumejipanga tuhakikishe kwamba kila certificate inayokuja tunailipa lakini baada ya kuhakiki kwa sababu Wizara ya Maji kuna historia ya upigaji, lazima tujipange tuhakikishe kwamba tunakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine nalotaka kulizungumza, Mheshimiwa Naibu Waziri ameligusia kidogo, ni tozo kwa watumiaji maji chini ya ardhi (tozo ya uchimbaji visima). Kupitia Sheria ya Usimamizi wa Rasilimali za Maji, Na. 11 ya mwaka 2003, kifungu cha 96 na Kanuni zake kinanipa mamlaka ya kusimamia tozo za uchimbaji visima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi Mheshimiwa Spika alizungumza hili kwa masikitiko makubwa na sisi kama Serikali tulilisikia. Waheshimiwa Wabunge mlilizungumza jambo hili la tozo ya uchimbaji wa visima kwa masikitiko makubwa, tulilisikia. Watanzania wanyonge wamelalamikia jambo hili tumelisikia. Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, imesikia kilio cha wanyonge, cha Watanzania kuhusu tozo ya watumiaji wa visima vya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuanzia leo Serikali imefuta tozo ya visima vya maji kwa watumiaji binafsi kwa matumizi ya nyumbani. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia tena; kuanzia leo Serikali imefuta tozo ya visima vya maji kwa watumiaji binafsi kwa matumizi ya nyumbani. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania hawa lazima wapate maji safi na salama. Hhatuwezi kuona Watanzania wetu wanalalamika na wanapata shida, Serikali tunafanya kila tunaloweza kuhakikisha kwamba matatizo haya tunayaondoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni huduma za usambazaji wa maji vijijini. Sera ya Taifa ya 2002 inasema waziwazi Watanzania wapate huduma ya maji si zaidi ya mita 500 kutoka maeneo wanayoishi. Vilevile Ilani ya Chama cha Mapinduzi inasema kwamba itakapofika mwaka 2020, Watanzania waishio vijijini wapate maji asilimia 85.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tumejipanga, tunaendelea kutekeleza miradi mbalimbali. Hadi hivi sasa jumla ya miradi 1,659 yenye vituo vya kuchotea maji 131,370 imejengwa. Kati ya vituo hivyo, vituo 86,780 vinafanya kazi na vina uwezo wa kuwahudumia wananchi milioni 25.359. Aidha, miradi 653 yenye gharama ya takribani shilingi bilioni 501 inatekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kujipanga hivyo, Serikali inatekeleza miradi mingine kwa mfano tuna mradi wa maji vijijini ambao unagharimu takribani shilingi bilioni 46.47 ambapo mradi huu tunaita payment by result. Tuna mradi mwingine ambao unafadhiliwa na Benki ya Dunia ambapo gharama yake ni takribani shiligi bilioni 806 na kazi yake kubwa ni kupeleka huduma ya maji vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa ya miradi ya vijijini ni kama ifuatavyo. Kama nilivyosema mwanzo, miradi mingi iliyojengwa kati ya 2010 - 2015 imejengwa chini ya viwango. Kazi yetu sisi kama Serikali na kama Wizara ni kuendelea kuhakikisha kwamba miradi hii tunaisawazisha ili wananchi wapate huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo lina changamoto ni uharibifu wa mazingira. Hali ya tabianchi inabadilika kila siku na baadhi ya maeneo yana changamoto sana. Tunachimba kisima leo baada ya miaka kumi kisima hicho kimekauka. Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kuwaomba Watanzania wenzangu tupambane na hali hii ili kuhakikisha kwamba miundombinu tunayojenga hii inakuwa endelevu ili tuweze kutumia sisi wenyewe pamoja na vizazi vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine iko kwenye usimamizi wa Jumuiya za Maji. Utakumbuka Bunge lako Tukufu hapa lilipitisha Sheria ya Huduma ya Maji na Usafi wa Mazingira, Na. 5 ya mwaka 2019, ambayo yenyewe imeeleza kwa kina uboreshaji wa jumuiya hizi za watumia maji. Tunaamini tukiweka mambo haya vizuri, miradi ya maji kwa kiasi kikubwa itafanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite kwenye eneo la huduma ya maji mijini. Kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi imeeleza waziwazi ifikapo mwaka 2020 wananchi watakaopata maji kwenye miji mikuu ya mikoa lazima iwe asilimia 95. Hali ikoje leo hii? Hivi tunavyozungumza kuna baadhi ya maeneo watu wanapata maji asilimia 97, 90, 86, lakini kwa wastani watu wanaopata maji kwenye miji mikuu ya mikoa ni asilimia 87. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumejipanga kuhakikisha kwamba tutafikia asilimia 95 ifikapo mwaka 2020. Katika kujipanga huko kazi ya mwanzo tuliyoifanya ni kuhakikisha tunaboresha utendaji kazi wa Mamlaka zetu za Maji, hilo la kwanza, kwa sababu kama mamlaka za maji zitalegalega hatutaweza kufikia malengo tuliyojiwekea. Kwa hiyo, kazi ya kwanza tuliyojiwekea ni uboreshaji wa utendaji kazi wa Mamlaka zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hilo jambo la kwanza tulilofanya ni kuweka performance contract (mikataba ya kazi) baina ya Waziri na Mwenyekiti wa Bodi, baina ya Katibu Mkuu na Mtendaji wa Mamlaka, lazima tuwapime kutokana na utendaji wao wa kazi. Hatuwezi kuendelea biashara kama kawaida, watu wanafanya wanavyotaka, watu wanakaa hawafanyi kazi, hili tutalisimamia na mimi ntalisimamia kwa nguvu zangu zote. Mtendaji Mkuu yeyote ambaye hatafanya kazi kama tulivyokubaliana, tutamuondoa. Lazima Mamlaka za Maji zibadilike, lazima Wizara ya Maji ibadilike, lazima Watanzania sasa waone matokeo makubwa ya Serikali yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumefanya maboresho kwenye ulipaji wa bili za maji. Kuna changamoto kubwa kwa baadhi ya maeneo ya watu kutokulipa bili za maji. Tumeamua sasa tulete prepaid meters, mita za kielektroniki ambazo tumezifunga watu waweze kupata huduma nzuri na walipe maji kutokana na matumizi wanayotumia. Kwa sababu kulikuwa na mchezo kwa baadhi ya Mamlaka kuibia wananchi lakini ukitumia prepaid meter sasa utalipa kutokana na matumizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili tutalisimamia na tutahakikisha kwamba tunafunga prepaid meters maeneo mengi. Bado prepaid meter bei yake iko juu lakini tutajitahidi kama tunavyoweza tuhakikishe kwamba tunawafungia wananchi wengi ili waweze kupata huduma nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tumeamua kwenye Mamlaka hizi kuboresha miundombinu ili kupunguza kwa kiasi kikubwa upotevu wa maji. Kuna upotevu wa maji kwenye maeneo mengi sana na tumeamua kujipanga kuhakikisha kwamba upotevu wa maji unapungua kwa asilimia kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo tumekubaliana na Mamlaka za Maji, kwenye mapato yao lazima kila mwezi watenge asilimia 35 ili waende kujenga miundombinu ya maji. Utaratibu uliokuwepo zamani Mamlaka zote za Maji zikitaka kujenga mradi zinakuja Wizarani kuomba pesa kwenye Mfuko wa Maji. Baada ya kuingia Wizarani nikawaambia hii haiwezekani, ninyi mnafanya biashara, mnauza maji, lazima muanze kujenga miundombinu ya maji na tumejipanga na hii tunaisimamia kwelikweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoa mfano, DAWASA (Mamlaka ya Maji ya Dar es Salaam) tayari wanajenga miradi mbalimbali kwa kutumia pesa zao za ndani. Mradi wa kwanza ni ule wa Chalinze – Mboga – Bagamoyo ambao unatumia takribani shilingi bilioni 10.7. Mradi wa pili ni Kibamba – Kisarawe ambao vilevile unajengwa kwa pesa za ndani za Mamlaka ya Maji DAWASA na tunatumia takribani shilingi bilioni 10.67. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna miradi mingine kwa mfano usambazaji wa maji maeneo ya Kiwalani, Madale, Usukumani na mengine mengi, kote huko tunapeleka huduma ya maji kwa kutumia pesa za Mamlaka zenyewe. Pia tuna mradi ule wa visima Kimbiji, tayari tumeshatangaza tenda ambapo tutatoa maji kutoka visima vyetu vya Kimbiji kuleta pale Kigamboni na tunajenga matenki na kazi hii itafanywa kwa kutumia pesa za ndani za DAWASA. Hatuwezi kuendelea tena kuanza kuzibeba Mamlaka hizi za maji wakati zinafanya biashara, zinafanya kazi, lazima tubadilike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine ambalo nataka kulizungumzia ni miradi ambayo tunaitekeleza ili kufikia malengo tuliyopewa na ilani ya Chama cha Mapinduzi. Hivi ninavyozungumza, tunatekeleza mradi wa maji kutoka ziwa Victoria kwenda Nzega Igunga, Tabora, Uyuwi, ambao unagharimu takribani shilingi bilioni 605. Tunatekeleza vile vile, mradi wa maji wa Arusha ambao unagharimu takribani shilingi bilioni 525.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatekeleza mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria kwenda kwako wewe Mheshimiwa Mwenyekiti Bariadi, Busega, Itilima, ambao utagharimu takribani shilingi bilioni 300 na mkataba ulisainiwa hivi juzi. Tuna changamoto kwenye miji mingi hapa Tanzania Serikali kwa kulitambua hilo, Serikali kwa mapenzi makubwa yaliyonayo kwa wananchi wake inatekeleza mradi wa miji 29 ambao unafadhiliwa kwa mkopo wa masharti nafuu kutoka Indi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu utagharimu takribani shilingi tirion moja nukta mbili, miji ambayo itanufaika na mradi huu kwanza ni muheza, Wanging’ombe, Makambako, Kianga, Songea, HTM, Korongwe na handeni, Njombe Mugumu Kilwa Masoko, Geita, Chunya, Makonde, Manyoni, Sikonge, Kasulu, Lujewa, Chato, Singida Mjini, Kiamboi, Mpanda, Chemba, Mafinga, Urambo, Kaliuwa, Pangani, Ifakara Rorya, Tarime, Chamwino na Nanyumbu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi inaendelea vizuri na tunategemea wiki inayokuja tutasaini na mkandarasi ambaye atapitia usanifu na kutayarisha makabrasha ya zabuni nitawaalika Wabunge wote ambao wanapitiwa na mradi huu waje washuhudie sherehe hii kwa sababu ni jambo muhimu katika maisha ya watanzania wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kulifuatilia hili, tutampa mkandarasi huyu au mtaalam mshauri huyu miezi miwili aweze kumaliza usanifu na kutupatia makabrasha ya zabuni na tunategemea mambo yote yatakwenda vizuri mkandarasi atakuwa kwenye site bayana ya mwezi Septemba na mwezi Oktoba ili aanze kazi ya kujenga miundombinu kwenye maeneo mbalimbali hapa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunao mradi wa kupeleka maji miji sita ambayo ni Mwanza, Musoma, Bukoba, Misungwi na Lamadi ambao unagharibu takribani shilingi bilioni 276. Tunao mradi wa kiistoria, mradi wa Mugango Kiabakari Butiama, ambao utagharibu takribani shilingi bilioni 30.69. Mradi huu umezungumzwa kwa muda mrefu, lakini sasa tulishafikia mahala pazuri tulishapata mkandarasi tumeshaandika BADEA kwa no objection BADEA imeshatoa un objection Kuwait fund imeshatoa un objection sasa tuna subiri no objection kutoka Saudi fund na tunategemea hivi karibuni watatuletea na mkandarasi ataanza kufanya mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwahakikishie ndugu zangu wa Mugango, Kiabakari, Butiama, na Musoma kwa ujumla kwamba itakapofika mwisho wa mwezi wa sita tunategemea mkandarasi awekwe site tutatuwe tatizo la maji ambalo linawakabili. Pia tunayo miradi mingi sana tuna mradi pale Dar es Salaam, mradi wa wasambaji maji ambao unagharimu takribani shilingi bilioni 197.8.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nijikite kidogo na eneo ambalo ya miradi ambayo imejengwa kutoka mwaka 2010 mpaka 2015 lakini hayatoi maji. Kuna miradi takribani 88 ambayo ilijengwa mwaka 2010 mpaka 2015 lakini haitoi maji miradi hiyo kwa mfano; kuanzia mradi wa masoko kule Rungwe Mbeya, mradi wa Mwanza Shirima kule Kwimba, mradi wa Tunduru kuna mradi wa Mbesa, kuna mradi wa maji kule Matimira, kuna mradi wa maji kule Singida ambayo ni Ikole Miginga, Kuna mradi wa maji kule maeneo Kigoma Kankoko, ambayo kuna miradi sita haifanyi kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuja na mpango wa kuhakikisha kwamba miradi hii yote inafanya kazi na wala hatutaleta mkandarasi tutatumia wataalam wetu wa Mamlaka za Maji, hivi tunavyozungumza mradi wa masoko wako watu tumenunua mabomba na wako vibarua takribani 80 wanachimba mtaro kuhakikisha kwamba kazi ya mradi huo inamalizika mara moja. Vilevile, kwa mradi wa Kakonko huko Kigoma tumepeleka wataalamu wetu kutoka Moshi, Mamlaka ya Maji Moshi ambayo wanauwezo mzuri wa kujenga vyazo vya maji kwenda kufanya kazi hiyo huko Kakonko Kigoma ili kutatua matatizo ya maji ya huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa miradi kwa mfano ya kule Kwimba tumepeleka Mamlaka ya Maji ya Mwanza kuhakikisha pia wanamaliza tatizo la mradi huu naomba niwahakikishie ndugu zangu watanzania, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na wengine wametuona kule Mbeya vijijini matatizo ya maji kwenye maeneo mengi tutayamaliza ili kuhakikisha watanzania watapata maji safi na salama. Kama mradi umejengwa 2010 mpaka 2015 lazima tuukarabati kwa sababu wataanzania wanalotaka wao ni kusikia habari ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na mazungumzo kuhusu wataalam wa maji ni kweli wataalam wa maji wengine wanachangamoto kubwa, wataalam wa maji wengine weledi wao ni mdogo, wataalam maji wengine hasa wa halmashauri uwezo wao ni mdogo, wataalamu wengine wa halmashauri siyo waadilifu, lakini pia nina amini wapo baadhi ya wataalamu ni wazuri sana na wataalam hawa wanategemea kuangalia kiongozi wao kama kiongozi wao anaonyesha njia kama kiongozi wao unasimamia vizuri na wao watajifunza kutoka kwako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba niwahakikishie kwamba tutafanya kila tutakaloweza tuchukuwe wataalam ambao ni waadilifu na tutasimamia kwa uwadilifu mkubwa. Kama nilivyosema mwanzo mtaalam yoyote kama yupo halmashauri, kama yupo kwenye mkoa, kama yupo wizarani, akifanya uzembe kama si mhadilifu nitamfukuza hapo hapo bila kupoteza hata muda. Nia yetu lazima tujenge Wizara ya maji mpya, Wizara ya maji ambayo itakwenda kujibu matatizo ya watanzania watanzania wamechoka wanahitaji maji Safi na Salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na issue nyingine wa uvunaji wa maji tumesikia maoni na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge ili tumelichukuwa na tulizielekeza halmashauri zitengeneze sheria ndogo ndogo kwa ajili ya kuvuna maji hasa kwenye majengo na taasisi za Serikali kwa vile hili naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge tutaendelea kulisimamia kuhakikisha kwamba tutafanya kazi hiyo vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utunzaji wa vyanzo vya maji, Mheshimiwa Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira amelizungumza sana hili kwa kweli utunzaji wa vyanzo vya maji ni muhimu sana kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri mwaka, tunazungumzia mwaka 1962 wakati watanzania wapo milioni 10 upatikanaji wa maji kwa mto mmoja ilikuwa mita za ujazo 7862, leo hii tuko watu karibuni milioni 54 upatikanaji wa maji takribani au upatikanaji kwa maji kwa mtu mmoja ni lita za ujazo 2300.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tujipange kwa sababu tulipoangalia vizuri tunaelekea chini ambako baadaye nchi yetu itakuwa na shida kubwa ya maji hili, jambo linaweza kutokea popote nyote Waheshimiwa Wabunge mlikuwa mashahidi South Africa Cap town siku zake zilizopita kulikuwa na changamoto kubwa ya maji, sisi tumejipanga kuhakikisha kwamba tunatunza vyanzo vya maji tunapanda miti na tunafanya kilimo ambacho kinaenda na vyanzo vya maji hasa kwenye maeneo ya vyanzo vya maji, hiyo ni muhimu sana kuhakikisha kwamba vyanzo vya maji hivi tulivyonavyo vinakuwa endelevu tuvitumie sisi pamoja na watoto wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunajaribu kuweka mipaka tunapima mipaka kwenye vyanzo vya maji ili visianze kuvamiwa vamiwa, tumejipanga vizuri tukishirikiana na wadau wote kuhakikisha kwamba vyanzo vya maji vyote tunavilinda na vinakuwa salama sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na Waheshimiwa Wabunge Wabunge wengi wamezungumza kwenye michango yao kwamba na mahitaji ya visima, na Waheshimiwa Wabunge tutatoa karatasi kila Mbunge aandike mahitaji yake ya visima ili tuanze kuhifanya kazi hiyo kwa uharaka sana kwa sababu wananchi wetu hatutaki wapate tabu hii ni muhimu sana tutatumia resources zetu zote, tutatumia nguvu zetu zote, tutatumia utaalam wetu tuhakikishe visima hivyo vimechimbwa haraka iwezekanavyo. Yule ambaye atashindwa kwenda na speed yetu tutamwambia imetosha kaa pembeni, tumejipanga kuhakikisha kwamba nchi yetu sasa kwenye sekta ya maji tunaenda mbele tumechoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Bwawa la Kidunda ni kweli imekuwa muda mrefu lakini tunajipanga sasa Serikali kuanza kufanya kazi ya ujenzi wa Bwawa hilo ili tuwe na maji ya uhakika kwa ajili ya Dar es Salaam, Bagamoyo na Kibaha, tutafanya kazi hiyo hiyo kwa bwawa la Farkwa, ambalo linategemiea sana na chemba na hapa Wilaya ya Chemba pamoja na jiji hili la Dodoma ambalo Serikali iko hapa makao Makuu yake, tumejipanga kwa ufupi kuhakikisha kwamba sekta ya maji matatizo yote tunamaliza ili watanzania wapate maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, kwa heshima na unyenyekevu mkubwa sasa ninaomba kutoa hoja.

WAZIRI WA ELIMU NA MAFUNZO YA UFUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.