Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza napenda nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya njema na kuniwezesha kushiriki katika Bunge lako Tukufu. Kwa namna ya kipekee nimshukuru sana na nimpongeze Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli, Makamu wa Rais, Makamu wa Rais Mama Samia Suluhu na Waziri Mkuu kwa ushirikiano mkubwa wanaotupa sisi Wizara ya Maji katika kuhakikisha tunatimiza majukumu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya kipekee nimshukuru mke wangu mpenzi Kauthar Francis na mama yangu kwa malezi na matunzo wanayonipa, Waswahili wanasema, usione vyaelea ujue vimetunzwa. Kwa hiyo, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wifi yenu yupo vizuri na ndiyo maana nami nipo vizuri katika utendaji wangu wa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wangu Profesa Makame Mbarawa, huyu ni jembe wembe. Ukiachana na Uwaziri wake lakini amekuwa mlezi katika kuhakikisha maagizo na maelekezo anayotupa katika Wizara yetu ili yawe na tija na kuleta mabadiliko makubwa katika Sekta ya Maji. Mheshimiwa Waziri ahsante sana, Mungu akubariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya kipekee, sisi hatuwezi kufanya kazi peke yetu, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Katibu Mkuu Profesa Kitila Mkumbo, Naibu Katibu Mkuu Eng. Kalebelo, Wakurugenzi wote na watendaji wa Wizara ya Maji; tumekuwa tukifanya kazi kwa ushirikiano mkubwa sana. Pamoja na changamoto tunazopitia lakini bahari kubwa ndiyo inayovukwa, tutaivuka katika kuhakikisha tunawaletea maendeleo makubwa sana Watanzania katika sekta ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii sana kumpongeza Mwenyekiti na Wajumbe wote wa Kamati ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa kazi nzuri, mapendekezo na ushauri wao lakini pia Waheshimiwa Wabunge wote na Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani kwa michango yao, tumeipokea na tutaifanyia kazi. Tumepata bahati ya kipekee kuona Wabunge kila aliyesimama ametoa mawazo, amezungumzia suala la maji na namna gani tunaweza kuboresha Wizara yetu katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Nataka niwahakikishie Wabunge sisi kama viongozi wa Wizara hatutokuwa kikwazo katika kuhakikisha Watanzania waishio mijini na vijijini wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kujibu hoja; moja ya michango ya Waheshimiwa Wabunge ilikuwa ni suala zima la ubadhirifu wa fedha za miradi na usimamizi wa miradi ya maji. Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli alivyoniteua nikiwa kama Naibu Waziri wa Maji tulipeana mikakati pamoja na watendaji wote, Katibu Mkuu na Waziri kwamba tupite maeneo yote ambayo tumepeleka fedha za miradi ya maji hususani maeneo ya vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kuwashukuru na kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge kwa ushirikiano mkubwa ambao wametupa sisi viongozi wa Wizara ya Maji kubaini changamoto kwenye eneo la maji vijijini. Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakijua miradi ya maji kuliko hata Wahandisi wetu wa Maji, lakini wamekuwa wakitoa solutions za kutosha. Niseme tu itoshe kwamba Waheshimiwa Wabunge wametusaidia kuokoa miradi mingi ya maji katika eneo la vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilifanya ziara Mbeya Vijijini kwa Mheshimiwa Oran Njeza, tulivyofika pale Mhandisi wa Maji alitupa taarifa ya miradi iliyotekelezwa katika miradi ya maji, lakini nami nikawa na taarifa yangu, baada ya kutupa taarifa nikamwambia nipeleke Mradi wa Galijembe ingawa hakutupa katika taarifa yake. Mhandisi yule wa Maji ananiambia Mheshimiwa Waziri kule eneo unapotaka twende kuna miinuko mikubwa utachoka, nikamwambia hapa sisi tumekuja kufanya kazi, tupeleke Mradi wa Galijembe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na mvutano mkubwa sana, tulivyofika katika eneo la Mradi ule wa Galijembe, mradi zaidi ya milioni 290 Mkandarasi amelipwa 260 hayupo site zaidi ya miaka mitatu. Unamuuliza Mhandisi wa Maji, mkandarasi yupo wapi, anasema Mheshimiwa huyu ni msumbufu huu mwaka wa tatu tukimwandika barua haji. Nikatoa agizo kwamba kesho lazima aje katika eneo la mradi. Kweli alivyokuja tukamuuliza mkandarasi nikiwa na Katibu Mkuu Profesa Kitila Mkumbo, unawezaje kulipwa fedha za miradi ya maji ilhali hujatekeleza? Mkandarasi ananiambia

Mheshimiwa Naibu Waziri tusipoteze muda, mimi nataka kikao chako kiwe kifupi, fedha tumelipwa lakini hizi fedha tulizopewa tumegawana na Mhandisi wako wa Maji; kama nalipwa certificate ya milioni 20, milioni 10 yangu na 10 yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatukuishia hapo, nilikwenda Shinyanga Vijijini katika Mradi wa Mwakitolyo, zaidi ya 1.4 billion, fedha zote zimelipwa za mradi huu wa maji, lakini unafika pale katika eneo la mradi wa maji unakagua, unakuta maji hayajapanda hata katika tenki, unamuuliza Mhandisi wa Maji fedha zimekamilika zote mkandarasi amelipwa, kwa nini maji hayapandi? Ananiambia Mheshimiwa Naibu Waziri naomba nikunong’oneze; nikamwambia hapana toa taarifa kwa wananchi watuelewe. Ananiambia Mheshimiwa Naibu Waziri sijawahi kuona kijiji wachawi kama hawa, tumetandika mabomba usiku yanapaa kama bombardier; hatuwezi tukawa na Wahandisi wa Maji kama hawa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mambo ya ajabu, hii siyo stori, lakini kutokana na changamoto hizi tulizoziona, sisi kama Wizara ya Maji tukakumbuka maneno ambayo Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli pale Ikulu alituambia sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji, anatupa Wizara ya Maji wananchi wa Tanzania waishio mijini na vijijini wapate maji safi na salama, tukishindwa kuifanya hiyo kazi atatutumbua. Sisi kama Viongozi wa Wizara ya Maji hatupo tayari kutumbuliwa, hawa wahandisi wa namna hii hawana nafasi katika Wizara yetu ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtatusamehe hawa wahandisi baada ya maelezo haya, tuliwabeba wazima wazima, mpaka hivi sasa wanaendelea na kesi mahakamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo kubwa la utekelezaji wa miradi ya maji ukiachana na fedha, wataalam wetu baadhi yao walikuwa siyo wazalendo. Sisi tulikaa na viongozi wa Wizara tukaona haja ya kuunda Kamati Maalum ya watu 10 ambayo inaongozwa na Profesa Mbwete, kukagua miradi yote ya vijijini na kuona changamoto yake ili tuje na mapendekezo ambayo tutaweza kutatua changamoto hii. Profesa Mbwete alifanya kazi hii kubwa, lakini akabaini kuna changamoto 17 ambazo zinatukabili sisi katika Sekta ya Maji Vijijini. Alikuja na mapendekezo 50 katika kuhakikisha sisi tunayatatua ili mwisho wa siku sekta hii ya eneo la vijijini liwe linafanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya mapendekezo ambayo amekuja nayo Profesa Mbwete ilikuwa kuanzishwa kwa Wakala wa Maji Vijijini na ndiyo maana sisi kama Wizara ya Maji tukaja katika Bunge lako Tukufu na tukawaomba Waheshimiwa Wabunge ili waweze kutupitishia Muswada ule ili wale Wahandisi wa Maji waje katika Wizara yetu ya Maji. Nataka niwaambie Wahandisi wa Maji nchini popote walipo, kuna Mheshimiwa Mbunge hapa alichangia katupa stori ya movie Fulani, akasema kwamba we will meet again, nataka niwaambie Wahandisi wa Maji we will meet again. Sisi tutakutana nao, lakini kwa kuwa wametupa rungu, sisi kama viongozi wa maji hatuna kisingizio kingine tena, tutawashughulikia katika kuhakikisha tunaleta nidhamu katika Wizara yetu ya Maji na tuweze kuleta matokeo chanya kabisa katika sekta yetu ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine cha msingi, pamoja na changamoto hizo zote ambazo tumezibaini, tumefanya kazi kubwa na kazi nzuri ya baadhi ya wataalam wetu. Leo ukienda kwa Mheshimiwa Mwakajoka pale Tunduma tuna mradi mkubwa na ndiyo maana Mheshimiwa Mwakajoka anakubali kazi tunayoifanya. Ukienda kwa Mheshimiwa Haonga kwake pale Mlowo, tuna mradi mkubwa tumeutekeleza na wananchi wake wanapata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ukienda Chunya na maeneo mengine yote miradi ambayo tumeianza, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Rais na Waheshimiwa Wabunge, hakuna single cent itakayopotea, sisi kama viongozi kwa kushirikiana na Waheshimiwa Wabunge tutasimamia miradi hii ili iweze kuleta tija na maana kubwa kwa wananchi wetu. Maji hayana mbadala, maji siyo kama wali, ukikosa wali utakula ugali, ukikosa ugali utakula makande; ukikosa maji utapata maradhi. Sisi ni Wizara ya Maji siyo Wizara ya ukame, tutahakikisha Watanzania waishio mijini na vijini wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo ililetwa na Waheshimiwa Wabunge ilikuwa suala zima la madai ya wakandarasi. Tunajua kabisa kwamba kulikuwa na kusuasua kukubwa sana wa baadhi ya miradi, kwamba wakandarasi wamefanya kazi lakini hawajalipwa. Nikiri tulikuwa na madai zaidi ya bilioni 88 ambayo tunadaiwa na wakandarasi, nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais pamoja na Wizara ya Fedha, mpaka ninavyozungumza tumeshapata zote bilioni 88 na tumeshawalipa wakandarasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wote ambao tumewalipa wakandarasi wao, certificates zipo na tutawapa orodha ya wale watu tuliowalipa. Sisi jukumu letu ni kusimamia na miradi iendelee kufanya kazi na sisi kama Viongozi wa Wizara ya Maji tunaomba bajeti yetu watupitishie ili twende tukasimamie fedha zile na zilete miradi mikubwa kabisa katika kutatua changamoto hii ya suala zima la maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo imeletwa na Waheshimiwa Wabunge ilikuwa manung’uniko ya suala zima la ulipaji wa vibali, kwa maana ya umilikaji wa visima, kwamba mtu amechimba kisima kwa fedha zake mwenyewe na pale kulikuwa na changamoto ya maji, lakini anatakiwa alipe kibali lakini alipe ada kila mwaka. Hii ni changamoto, sisi kama viongozi wa Wizara tumeiona, tunakwenda kubadilisha kanuni zetu na tunaziwasilisha kwa Waheshimiwa Wabunge ili tuondokane na changamoto hii katika kuhakikisha Watanzania hawapati tabu katika suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina maneno mengi sana, Mheshimiwa Profesa yupo hapa, atazungumza kwa kina. Sisi tunachotaka kusema Mheshimiwa Profesa anafanya kazi nzuri, sisi tutakupa ushirikiano wa dhati kabisa katika kuhakikisha tutatatua tatizo hili la maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine iliyokuja, kuona kwamba kuna baadhi ya wananchi wanaishi katika vyanzo vya maji. Leo kuna Ziwa Victoria, Ziwa Tanganyika na Ziwa Nyasa, lakini wananchi wa maeneo yale hawapati maji. Sisi kama Wizara tumeliona na tumeagiza tufanye usanifu unaendelea katika kuhakikisha tunabuni miradi ili wananchi wale wa pembezoni waweze kupata maji na kutumia rasilimali muhimu iliyokuwepo. Nataka nimhakikishie Mbunge wa Sumve, Mheshimiwa Mzee Ndassa ukisoma Tenzi za Rohoni zinasema unapotembea na kuzuru wengine naomba usinipite Mwokozi, hatutokupita pale Sumve katika kuhakikisha unapata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza hayo, naomba nimalizie kwa kuzungumza na kaka yangu Mheshimiwa Mbunge wa Kibamba, Mheshimiwa Mnyika. Miaka ya nyuma kabla mimi sijaja Bungeni nilikuwa mwanafunzi, alikuwa unajenga hoja kuhusu suala zima la uboreshaji wa maji katika Jiji la Dar es Salaam, hali ilikuwa mbaya sana Dar es Salaam. Kulikuwa na mabomba ya Mchina yalikuwa hayatoi maji, nilimfahamu kwa kusimamia hoja yake, namheshimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilifanya kazi kubwa sana, Quran inasema waamma biniimati rabbikka fahaddith, zielezeeni neema za Mwenyezi Mungu kwa kushukuru. Serikali imefanya kazi kubwa sana, leo eneo la Kibamba zaidi ya kilometa 360 tumezitandika katika kuhakikisha wananchi wa Kibamba wanapata maji. Leo hii ninavyozungumza wananchi wa Kibamba walikuwa wanapata maji kwa saa nane, lakini sasa hivi kwa saa 24. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiachana na hayo, Mheshimiwa Mbunge ni shahidi kwa kuwa ana macho; tuna mradi tunautekeleza Matosa, Hondogo, King’azi A na Mbezi Makabe. Mheshimiwa Mnyika nini au tukupe donda ufukuze nzi? Tunatambua kabisa Mheshimiwa Mnyika maji yamekuwa na uhitaji mkubwa sana lakini sisi kama viongozi wa Wizara tunaendelea kuwaagiza DAWASA kutenga asilimia 35 kwa mapato ya ndani kuhakikisha tunayafikia maeneo ambayo hayajafikiwa na maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)