Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kukushukuru kwa kunipatia nafasi hii, nikianza na kuunga mkono kwa asilimia mia moja hoja iliyoletwa mbele yetu na Wizara ya Maji. Nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Maji kwa kazi nzuri anazozifanya katika Wizara hii, Mheshimiwa Waziri nampongeza amekuwa akitembelea mazingira yetu na kuona hali halisi ya upatikanaji wa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kufanya masahihisho katika ukurasa wa 56 wa hotuba. Hotuba ya Mheshimiwa Waziri imesema kwamba, nishukuru kwanza kwa Serikali kutoa shilingi bilioni 1.7 ili kukamilisha Bwawa la Mwanjolo, lakini nataka kusema kwamba maelezo yalitolewa katika kitabu kwamba tayari wananchi wa Mwanjolo, Jinamo, Mbushi Wilayani Meatu wanapata huduma ya maji wananchi 13, 859 siyo sahihi. Kilichopo hapa ni mabirika ya maji kwa ajili ya mifugo, ndiyo wanaokunywa maji. Usambazaji wa maji katika vijiji vilivyotajwa hapa haujafanyika. Ninachoomba fedha kwa ajili ya kufanya usanifu kwa ili kusambaza maji kwa wananchi katika vijiji tajwa hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali na kuishukuru kwa kusaini mkataba wa shilingi bilioni 330 kwa kutoa maji Ziwa Victoria kwa ajili ya Mkoa wa Simiyu na kuyapeleka Nyashimo, Bariadi pamoja na Itilima ambao utekelezaji wake utakamilika mwaka 2022. Nataka nitoe maoni yangu machache; toka mwaka 2016, Wabunge wa Mkoa wa Simiyu tumekuwa tukiomba mradi huu yajengwe mabomba mawili, lakini fununu niliyoisikia kwamba linajengwa bomba moja. Kama litajengwa bomba moja dhana nzima ya kukabiliana na athari ya mabadiliko ya tabianchi haitakuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizi zilitafutwa na Ofisi ya Makamu wa Rais kwa lengo kuu la kukabiliana na athari ya mabadiliko ya tabianchi katika Mkoa wa Simiyu ambao umekumbwa na ukame wa muda mrefu, endapo kama litajengwa bomba moja wananchi hawataweza kumudu maji haya kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji. Lengo kuu lilikuwa ni kukabiliana kwa kilimo cha umwagiliaji, kama litajengwa bomba moja maji haya yakitibiwa gharama yake itakuwa juu wananchi hawataweza kuyanunua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nashauri mawazo ya Wabunge yasikilizwe kuwe na mabomba mawili ambayo litakuwa na maji ghafi ambayo hayajatibiwa ambayo hayatakuwa na gharama kubwa ili wananchi waweze kuyamudu kwa ajili ya kukabiliana na athari ya mabadiliko ya tabianchi. Kwa kuwa mradi huu unatekelezwa kwa awamu mbili na Wilaya ya Meatu na Maswa ni Wilaya zilizo na ukame mkubwa...

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)