Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa nguvu kuendelea kuwatumia wananchi wa Jimbo la Kyerwa. Pia nichukue nafasi hii kuipongeza Wizara ya Maji kwa kazi nzuri inazozifanya. Pamoja na changamoto ambazo wameeleza, lakini tumeona Mheshimiwa Waziri na timu yake wakienda maeneo mbalimbali kutatua kero ya maji. Kwa hiyo, tunakupongeza sana Mheshimiwa Waziri na tunaamini juhudi hizo zitaendelea ili kuhakikisha tunapata maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, pamoja na changamoto ambazo zipo, napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru kwa miradi ambayo inaendelea kule Jimboni kwangu Kyerwa. Tunao mradi mkubwa ambao tumemaliza usanifu, mradi wa kimkakati wa Kata 18 kwenye vijiji 57. Mradi huu tunaamini mpaka hatua tuliyofikia ya usanifu, sasa kazi iliyobaki ni kazi ya kutangazwa tenda na kuutafutia pesa ili mradi huu uweze kuanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoomba sana Mheshimiwa Waziri, hali ni mbaya kwa Wanakyerwa, naomba sana mradi huu uangaliwe ili wananchi waweze kupata maji safi na salama. Tunajua maji ni uhai, maji ni kila kitu, maji ni uchumi. Bila kuwa na maji safi na salama mambo mengine hayawezi yakaenda hata tunaposema tunaingia kwenye uchumi wa kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili uchumi wetu uweze kustawi, uweze kusonga mbele ni pale ambapo tutakuwa na maji safi na salama kwa sababu tunategemea kule vijijini ndiko kuna uzalishaji mkubwa na hawa wananchi wakipata maji safi na salama ule usumbufu wa kuamka usiku kwenda kutafuta maji utaondoka na wataingia kwenye shughuli za uzalishaji na uchumi wa Taifa letu utaweza kukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri mradi huu nimeshakutana na wewe ofisini, nimeshakutana na Naibu Waziri, nimeshakutana na Katibu Mkuu lakini nimekutana pia na Waziri wa Fedha, ninaamini Mungu atasaidia mradi huu utapatiwa pesa ili uweze kuanza na wananchi wa Kyerwa waweze kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nilisemee kwa upande wa Kyerwa, tunao mradi wa Kata ya Mabira unaendelea vizuri lakini kuna mradi wa Kata ya Kaisho, Rutunguru na Isingiro, mradi huu Naibu Waziri ulipofika Kyerwa walikueleza Mkandarasi kwa kweli hana uwezo na uliamuru Mkandarasi yule asimamishwe lakini tangu umetoka kule hakuna kazi inayoendelea, mradi umesimama na huyu Mkandarasi kwa kweli mimi niombe asije Wizarani kuwadanganya, hana uwezo kabisa. Wakati mwingine unajiuliza, hivi hawa Wakandarasi wanapatikanaje? Mtu ambaye anaendesha kampuni yeye na mke wake ndio unakuta wako site, ndio wanaofanya kazi, yaani hakuna kitu kinachoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli naomba sana na Mheshimiwa Waziri ikiwezekana muunde Tume ya kwenda kukagua hii miradi na kuangalia uwezo wa hawa Wakandarasi kweli uwezo wao ni mdogo na wanakwamisha hii miradi isiweze kukamilika. Hili Wabunge wengi wameliongelea, maeneo mengi kwa kweli Wakandarasi hawana uwezo na wakati mwingine unaweza ukafikiri labda hizi kampuni wanapeana ni zile za urafiki au za kutafuta 10 percent ili waweze kupata chao waondoke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tuna nia ya dhati ya kuweza kuwapa maji safi na salama Watanzania, lazima tuhakikishe tuna wataalam wenye uwezo wa kuweza kusimamia miradi hii, lakini pia hata wale wanaotoa hizi tenda tuwafuatilie kwa karibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunamwamini Mheshimiwa Waziri, anafanyakazi zake vizuri pamoja na Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu yote lakini lazima waangalie wataalam walionao kule chini, wanaweza wakawakwamisha ili wasiweze kufanikisha zile juhudi zao. Kwa hiyo, naomba sana hili waliangalie na pia kwa mfano, kama kule kwangu Kyerwa kuna watalaam wawili, Mzee moja ambaye ni Injinia kwa kweli ni mzee ambaye afya yake haijakaa vizuri, anahitaji msaada. Kwa hiyo, Kyerwa ni kama tuna mtaalam mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri hili aliangalie. Tunaposema tunataka tuwe na chombo ambacho kinajisimamia kuhusiana na maji, lazima tuwe na wataalam wa uhakika. Hata tukisema tutaunda chombo, bila ya kuwa na wataalam, tutakuwa tunapoteza muda. Nawaomba sana hilo tuliangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano ni kwenye Wizara ya TAMISEMI, wameunda TARURA. Kwa muda mfupi TARURA wamefanya kazi nzuri sana, ni kwa sababu wamepeleka wataalam wenye uwezo. Nami nawaomba sana wapeleke wataalam ili waweze kuwapatia wananchi maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, Waheshimiwa Wabunge wameongea sana kwamba ili tuweze kutatua tatizo la maji, tumeomba sana huu mfuko wa maji uweze kuongezewa fedha. Bunge lilishaazimia shilingi 50/=, lakini nashindwa kuelewa, ni kwa nini hili jambo linapata shida sana? Tunaomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa aeleze kweli tuweze kuridhika. Hatuwezi tukaridhika kwa maneno tu, tunahitaji wananchi wetu waweze kupatiwa maji safi na salama ndiyo tunaweza kuelewa. Vinginevyo kwa kweli Jumatatu wakati unahitimisha, kama hutakuwa na majibu ya kuongeza shilingi 50/= kwa kweli hatutaelewana kama Wabunge wote walivyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, nilikuwa najiuliza, hivi tukiamua leo Watanzania, maana tumeamua kuwapatia huduma Watanzania; tukiamua kila vocha ya shilingi 1,000/= ikatwe shilingi mbili tu, hebu jaribu kupiga mahesabu ni vocha ngapi ambazo zinaweza kuingizia pesa nyingi kwenye mfuko wa maji na tukaweza kutatua tatizo la maji?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana, tunavyo vyanzo ambavyo vinaweza vikatupatia maji safi na salama. Watanzania tumeamua kupiga hatua, ni pamoja na kujifunga mkanda. Vinginevyo, tutakuja hapa tutaeleza mambo ya siasa, tutasema tunawapelekea maji lakini hakuna hatua yoyote ambayo tutachukua. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri hili uliangalie tuweze kuwafikishia wananchi wetu maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli baada ya kusema hayo, naishukuru Serikali, wanasema hata kwa kile kidogo uweze kushukuru. Kwa Kyerwa kwa kweli Awamu ya Tano angalau tunaweza tukasema kuna chochote tunachokiona, kama nilivyosema tunao mradi wa kimkakati wa vijiji 57 kwenye Kata 15.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kuomba sana, Mheshimiwa Waziri mradi huu ndiyo unaweza ukawa mkombozi kwa wananchi wa Kyerwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)