Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. MUSSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya Maji, Wizara Muhimu sana katika maisha ya wananchi wenzetu na sisi wenyewe hapa tulipo. Nianze kwa kupongeza kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Waziri kaka yangu Mheshimiwa Profesa. Mbarawa, mdogo wangu Mheshimiwa Aweso na Katibu Mkuu na timu nzima ya Wizara pamoja na changamoto nyingi zilizopo za upatikanaji wa maji nchini, ikiwemo pia na changamoto ya kibajeti.

Mheshimiwa Spika, nami nianze kwa kushukuru kwa mradi wa maji wa Kijiji cha Igalula, nimeona imetengwa shilingi milioni 76 hapa za kwenda kumalizia kumlipa mkandarasi aliyefanya kazi katika Kijiji cha Igalula. Kwa kweli nashukuru sana Wizara kwa kazi kubwa iliyofanyika pale.

Mheshimiwa Spika, nina masikitiko, lakini mwishoni nitachangia. La kwanza, mradi wa Ziwa Victoria unakuja katika Mkoa wa Tabora, unakwenda katika Majimbo yote ya Mkoa wa Tabora kasoro Jimbo la Igalula. Hili nimekuwa nalisema sana na nimekuwa nikiahidiwa kwamba kuna miradi mingine mbadala itakuja lakini pia nimeahidiwa kwamba Jimbo la Igalula itaingizwa katika awamu ya pili ya mradi wa maji wa Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Spika, tumekuwa na subira hiyo, lakini pia Mheshimiwa Rais amekuja Igalula katika Kata ya Kigwa akaahidi kwamba maji ya Ziwa Victoria yatakuja. Nasikitika kwamba nimeona pia kuna mradi tena wa miji 29 na bado Jimbo la Igalula halijaangaliwa. Miji ambayo tayari inapelekewa maji ya Ziwa Victoria tena karibu na Jimbo langu imewekwa tena katika miji 29 kwenda kuwekewa miradi mingine ya maji.

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo la Igalula nimejaribu kupitia sijaona mradi hata mmoja ambao unakuja kusaidia kutatua kero ya maji katika Jimbo la Igalula. Bado katika mgao wa fedha za Halmashauri kwenda kusaidia utekelezaji wa miradi ya maji katika maeneo yetu, ukiangalia Wilaya yetu ya Uyui, tuna Majimbo mawili; Tabora Kaskazini kwa Mheshimiwa Almasi Maige na Jimboni kwangu; tumepata fedha takribani shilingi milioni 500 tu, lakini kuna Majimbo ambayo yanapita maji ya Ziwa Victoria, yana Jimbo moja, wanapata zaidi ya shilingi milioni 800. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisemi kwamba yamefanyika makosa, lakini tuangalie, Jimbo la Igalula maji hayaendi, fedha tunazotengewa ni ndogo, miradi hii itatekelezwa namna gani? Mheshimiwa Naibu Waziri alikuja Tabora, Igalula tukamweleza, kuna vyanzo vya maji viwili vimepatikana katika Kata ya Loya na Tura. Usanifu umefanyika, namshukuru Katibu Mkuu alinisaidia; katika Kata ya Loya usanifu ulishafanyika, documents ziko Wizarani kwenu, lakini hakuna chochote kilichoandikwa katika kitabu cha bajeti kuhusiana na mradi wa maji wa Loya na kuhususiana na mradi wa maji wa Tura.

Mheshimiwa Spika, nataka nikwambie, tanki kubwa la maji linalopeleka maji Manispaa, linalopeleka maji Sikonge na Urambo linajengwa kilomita 15 toka Jimboni kwangu Igalula. Wananchi wanaona tenki linatengenezwa pale, maji Igalula hayaji, this is not fair at all. Wananchi wanasikitika lakini kabisa hatutendewi haki. Kilomita chini ya 15 tenki kubwa linajengwa lakini wananchi hawapati maji. Mheshimiwa Waziri, naomba hili tuliangalie sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka pia nizungumzie mgawanyo wa fedha hizi ndogo ambazo nimejaribu kusema hapa; ukiangalia ukurasa wa 129, ukurasa wa 148, tazama na ukurasa wa 147, kuna maeneo wanafaidika na maji ya Ziwa Victoria yanakwenda. Miradi zaidi ya mitatu inazungumzwa katika kitabu hiki inakwenda Jimbo jirani na kwangu, wananchi wangu wanapata taarifa hizi. Inaonekana sisi hatufanyi kazi. Inaonekana wananchi wangu wamesahaulika kwenye suala la maji. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, tuangalie maeneo ambayo yana matatizo ya maji tuweze kupeleka hizo fedha.

Mheshimiwa Spika, nami nizungumzie suala la kuongeza fedha katika Mfuko wa Maji ili miradi hii iende. Nimeanza kuzungumzia changamoto za Igalula kwa kifupi tu; lakini miaka yote mitatu tuko hapa, nimekuwa nazungumzia uwezekano wa Serikali kuongeza shilingi 50/= ili ziende kwenye Mfuko wa Maji ziweze kutusaidia sisi wenye matatizo ya maji katika maeneo yetu. Utamu wa ngoma uingie ucheze. Kwa sisi tunaotoka vijijini, unapozungumzia suala la maji, ukamwambia mwananchi eti tukiongeza shilingi 50/= kutakuwa kuna inflation, hawezi kukuelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi effect za inflation kwa wananchi wetu wa Igalula na effect za kukosa maji, zipi tatizo ni kubwa sana kwa wananchi wetu? Kukosa maji ni tatizo kubwa sana. Ikiongezwa shilingi 50/= shida yake watakayopata wananchi wetu ni ndogo kuliko wananchi kuendelea kukosa maji kwa sababu eti ya shilingi 50/=. Kama alivyosema Mheshimiwa Chenge, nami nataka nimuunge mkono Mheshimiwa Chenge. Alichosema ndugu yetu Musukuma ni cha msingi, Mheshimiwa Waziri safisha Wizara yako, miradi inaonekana ina thamani kubwa haiishi, lakini haina manufaa kwa wananchi wetu. Kisima kimoja kinachimbwa kwa shilingi milioni 45, lakini utafiti tulioufanya kisima kinachimbwa kwa shilingi milioni 20 na wananchi wanaweza kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yapo matatizo katika Wizara, tunaomba Mheshimiwa Waziri asafishe Wizara yake ili hizi fedha tunazomwidhinishia hapa, ziende zikalete matokeo kwa wananchi wetu ambao wana matatizo makubwa sana. Pamoja na matatizo yaliyopo katika Wizara yake, sisi Wabunge kazi yetu ni kumpitishia fedha, kumpatia fedha ili miradi iende. Hatuwezi kuacha kumwongezea fedha eti kwa sababu kuna ubadhirifu katika Wizara yake. Wizara yake ikisafishwa, hizi fedha zikienda wananchi wetu watanufaika kwa njia moja au nyingine.

Mheshimiwa Spika, hili suala la kusafisha Wizara halihitaji kuchukua miezi miwili au mitatu. Tunajua Mheshimiwa Waziri amezianza juhudi, lakini zifanyike haraka sana ili mwisho wa siku hizi fedha tunazozipitisha hapa zikalete matokeo chanya kwa wananchi wetu na siyo kingine ni kupata maji kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unaweza kuona hapa Wabunge wote watakaosimama, wanachokihitaji wao ni maji. Suala la kwamba unapata wapi fedha, tuachie sisi. Tutasimamia Azimio letu la shilingi 50/= ili uweze kuongezewa fedha za Mfuko wa Maji. Nataka niwaombe Waheshimiwa Wabunge wote, shida ya maji inatukuta sisi sote, kwa hili tusimamie Azimio letu, ule upungufu tumwachie Mheshimiwa Waziri akayafanyie kazi.

Mheshimiwa Spika, hapa Jumatatu hakitaeleweka mpaka shilingi 50/= iongezwe. Wananchi wa Igalula wanataka maji, tunajua hatuwezi kuzungumza kupata maji bila kupata rasilimali fedha. Hii fedha tutasimamia aipate, lakini tukiipata maji yasipopatikana, sasa Mheshimiwa Waziri huo mzigo utakuwa ni wa kwake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nilitaka niseme hayo, lakini naomba Mheshimiwa Waziri aangalie mgao wa fedha unaokuja katika mikoa yetu, aangalie changamoto zilizopo. Kwa sababu Igalula tuna changamoto tofauti na Sikonge na maeneo mengine. Mgao wa fedha uje, miradi ambayo tumeshaifanyia usanifu iletewe fedha ili iweze kutusaidia kutekeleza miradi tuliyokuwa nayo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, lakini Jumatatu hakieleweki hapa mpaka shilingi 50/= iweze kupitishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)