Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hotuba iliyo mbele yetu, hotuba ya Wizara ya Maji, hoja ambayo ni muhimu na ni nyeti kwa Watanzania wote.

Mheshimiwa Spika, nianze kuwapongeza viongozi wa Wizara hii; nianze kumpongeza Waziri wa Maji, Mheshimiwa Prof. Mbarawa; nimpongeze Naibu wake, Mheshimiwa Aweso; nimpongeze Katibu Mkuu, Prof. Kitila Mkumbo na Naibu Katibu Mkuu Eng. Kalobelo; wakurugenzi wa Wizara pamoja na watendaji wa maji katika ngazi mbalimbali, Mamlaka ya Serikali za Mitaa pamoja na mikoa. Kwa kweli wanafanya kazi kubwa na kazi wanazozifanya zinaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri ulikuja kukagua mradi wetu wa Chawi, ulifanya kazi kubwa ulizunguka mpaka Nanyamba, Mheshimiwa Aweso ulitatua changamoto kubwa ya mradi ambao ulikuwa unatekelezwa Nanyamba, unasimamiwa na Mtwara Vijijini, baada ya kikao chako kifupi ulitoa suluhisho la changamoto ile.

Mheshimiwa Spika, niwashukuru kwa miaka miwili mfululizo mlikuwa mnatenga fedha za kutosha kwa ajili ya miradi ya maji ya Halmashauri ya Mji wa Nanyamba, nawashukuru sana. Lakini kipekee niwashukuru hivi karibuni mmetoa kibali kwa ajili ya ujenzi wa visima kumi. Kwa hiyo. nichukue nafasi hii Mheshimiwa Waziri nikushukuru kwa jinsi unavyotoa jicho la kipekee kwa Halmashauri ya Mji wa Nanyamba.

Mheshimiwa Spika, nichangie sasa kuhusu Mradi wa Maji wa Makonde; mradi huu ni wa siku nyingi na upo katika ile miji 28, na mradi huu katika eneo letu utahudumia Mamlaka za Serikali za Mitaa zisizopungua nne na majimbo kama matano. Mradi huu ni wa siku nyingi na unahitaji kujengwa upya. Sasa Mheshimiwa Waziri nikukumbushe tu kwamba tulishawasilisha andiko Wizarani kwako na ulipofika pale Chawi uliahidi kwamba hakuna Mtanzania atakayekosa maji kwa sababu ya gharama.

Mheshimiwa Spika, mradi huu ni wa siku nyingi na unahitajika kujengwa upya. Sasa Mheshimiwa Waziri nikukumbushe tu kwamba tulishawasilisha andiko Wizarani kwako na ulipofika pale Chawi, uliahidi kwamba hakuna Mtanzania atakayekosa maji kwa sababu ya gharama. Nanyamba andiko letu ni kutoa maji Mitema na kupeleka Halmashauri ya Mji wa Nanyamba, mradi ambao unahusisha kata tisa, mitaa tisa na vijiji 34. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watendaji waliniahidi kwamba tutaingiza kwenye utekelezaji wa fedha za mkopo wa Serikali ya India hata kama hawajatoa maandishi kwa Mkurugenzi wetu, lakini kauli ya Waziri, kauli ya Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu tunaiamini. Rai yangu kwa Mheshimiwa Waziri ni kwamba Serikali inafanya kazi kwa maandishi. Naomba mtoe andiko mumpelekee Meneja wa Mradi wa Makonde ili wakati wa utekelezaji asione kwamba ni annex aone kwamba ni component muhimu katika mradi huo.

Mheshimiwa Spika, mradi huu kama nilivyosema unahusisha vijiji 34 na mitaa tisa; kwangu wananchi wanaopata maji ni asilimia 45, lakini mradi huu ukitekelezwa, tutafikia asilimia 85. Kwa hiyo, naomba component hii ya kutoa maji Mitema kupeleka Nanyamba isisahauliwe na aandikiwe barua Meneja wa Mradi ili wakati wa utekelezaji basi isiwe annex iwe ni sehemu ya mradi wa Makonde. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichangie mradi wa maji wa kutoa Mto Ruvuma na kupeleka Mtwara Manispaa. Wachangiaji waliopita wamezungumzia mradi huu lakini naamini kwa sababu chanzo cha maji kipo Jimboni kwangu Mahembe Chini, naomba sasa mradi huu utekelezwe, ni mradi wa muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, suala lingine, kuna kauli mbili Wizarani, kuna kauli ya kutekeleza mradi huu, lakini kuna maneno ya chini chini kwamba mradi huu siyo viable kwa hiyo, hautatekelezeka. Kwa hiyo, naomba wawe wazi tuambiwe kama mradi unatekelezwa au autekelezwi. Wananchi wa Mtwara wanataka maji whether wanatoa Ziwa Victoria kupeleka Mtwara au Mto Ruvuma, tunachotaka ni maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama mradi unatekelezwa tuambiwe kwamba mradi unatekelezwa; na kama kuna mabadiliko ambayo yameonekana kwamba kwa Wizara kutekeleza mradi huu kuna gharama ambazo siyo za lazima, basi mtuambie. Wanachohitaji wananchi wa Mtwara, Nanyamba na sehemu ya Mtwara Vijijini ambapo linapita bomba hili, wajulishwe ili na wao waweze kufahamu na pia ili miradi inayotayarishwa na Mamlaka ya Serikali ya za Mitaa iweze kujumuisha maeneo haya ambayo hapo awali tuliacha kwa sababu kuna mradi mkubwa wa kutoa maji Mahembe Chini, yaani Mto Ruvuma na kupeleka Manispaa ya Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa 106 wa kitabu cha Mheshimiwa Waziri unazungumzia changamoto za utekelezaji wa miradi ya maji. Hapa changamoto ya kwanza amesema upatikanaji mdogo wa fedha za kutekeleza miradi. Naungana na wale wanaosema tuongeze shilingi 50/= ili tupate fedha za kutosha za kutekeleza miradi yetu ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna haja ya kuwa na wasiwasi. Professor amesema kwenye kitabu chake kwamba kuna changamoto ya fedha na isije tukawalaumu baadaye kwamba Mheshimiwa Prof. Mbarawa alishindwa, kumbe siyo kwamba alishindwa, hakuwezeshwa, hakupewa fedha za kutosha. Kwa hiyo, tuwape fedha za kutosha ili Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji waweze kutekeleza miradi ya maji kama walivyojipangia. Tusipofanya hivyo, tutawalaumu kwa makosa ambayo siyo ya kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia hapa Mheshimiwa Waziri ameweka wazi kwamba fedha za maendeleo hadi Aprili amepata asilimia silimia 53, fedha za uhakika ni za Mfuko wa Maji, wenye kufanya maamuzi ni sisi. Mheshimiwa Chenge amesema vizuri kwamba kuna Azimio la Bunge. Kwa hiyo, tuliunge mkono Azimio la Bunge, Wizara hii ipate fedha ili itekeleze miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye Ilani ya Chama chetu cha Mapinduzi inasema tutatekeleza miradi ya maji kwa asilimia 85 ifikapo 2020. Bila kuwaongezea fedha tutakuwa na maswali magumu sana mwakani. Hii ni Mei sasa hivi, 2020 siyo mbali. Tuwape fedha ili wakatekeleze miradi ya maji ili 2020 tusipate kazi ya kuzungumza maneno marefu majukwaani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa mwisho unahusu mabadiliko ambayo tumeyafanya hivi karibuni kuhusu sheria Na. 5 ya 2019 kuhusu Huduma ya Maji na Usafi wa Mazingira. tunaazisha RUWASA, ushauri wangu kwa Wizara, hebu tufanye matayarisho ya kutosha ili chombo hiki kipya tunachokianzisha kianze kwa ufanisi.

Mheshimiwa Spika, Mamlaka za Serikali za Mitaa zina hadhi tofauti. Tumeona pale tulipoanzisha TARURA, tuliwaambia kwamba Mhandisi wa Maji aende kule na gari yake. Ukitamka hivyo, Meneja wa RUWASA wa Nanyamba hatakuwa na gari, kwa sababu so far Nanyamba haina gari ya maji. Kwa hiyo, ukisema atumie gari ambayo alikuwa anatumia Halmashauri, Meneja yule ameanza kazi kwa kufeli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba matayarisho ya kutosha yafanywe ili RUWASA atakapoanza, Meneja wa RUWASA wa Mamlaka ya Serikali za Mitaa awe na rasilimali za kutosha. Kwanza apate ofisi, awe na rasilimali za kutosha, awe na vitendea kazi na aanze kwa kujiamini na siyo kuwa omba omba wa Mamlaka ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, rai yangu kwa Wizara, tufanye maandalizi ya kutosha. Sheria tumeitunga vizuri, lakini tusipofanya maandalizi ya kutosha tutaanza kuilaumu RUWASA wakati hatujawapa rasilimali za kutosha.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)