Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kutoa mchango wangu kwenye sekta hii muhimu. Pia naomba niungane na wewe kuipa pole familia na watoto wa Mzee Mengi kwa kuondokewa na baba yao. Nilivyokuwa Waziri wa Uwekezaji, Uwezeshaji na Sekta Binafsi ndiye alikuwa Mwenyekiti wa Baraza la Sekta Binafsi.

Mheshimiwa Spika, baada ya pole hiyo, sasa naomba nichangie kwenye sekta hii muhimu na nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa sababu kila anapoongea na anapokuwa kwenye mikutano ya hadhara, jambo kuu analoliongelea ni kumtua mama ndoo kichwani, jambo ambalo kila mmoja wetu hapa nina hakika analipenda kwa sababu bila maji hakuna uhai, uchumi na maendeleo. Kwa hivyo, analolifanya Rais ni jambo muhimu na nawapongeza sana Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote ili waweze kuona kwamba azma hii ya Mheshimiwa Rais na wananchi wa Tanzania inafikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hivyo; Wilaya yetu ya Hanang ni Wilaya ambayo ni kavu, kwanza ipo kwenye lift valley na kwenye lift valley kule chini maji yanapatikana kwa shida sana. Ningependa kuanza na kuwapongeza sana Serikali kwa sababu walitoa shilingi bilioni
2.5 ili kuiletea Makao Makuu ya Wilaya maji na tulitegemea mwaka jana mwezi wa Tisa maji ya Katesh yawe yamefika lakini mpaka hivi nasimama hapa, mradi umetekelezwa kwa asilimia 66 tu. Naomba sana yafuatayo yafanywe; kwamba kuna wakandarasi ambao wanadai hela zao na certificates zimefika, naomba jamani tuweze kulipia certificate hizo ili maji ya Katesh yapatikane, siyo jambo zuri kwa Makao Makuu ya Wilaya kutokuwa na maji ya uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika,vilevile, nafurahi sana na kuipongeza Serikali kuchimba visima ambavyo vinatumia solar katika Kijiji cha Gehandu, Kijiji Garbapi, Kijiji cha Gidika, Kijiji cha Hirbadaw, Kijiji cha Gawlolo, Kijiji Murumba, Kijiji cha Dawar, Kijiji cha Ginirish na Kijiji cha Laghanga. Naishukuru Serikali kwa nini si rahisi kuwa na visima vingi kwa wakati mmoja, lakini naomba mradi huu uwe wa maana kwa wananchi kwa sababu kutokana na kuwa kwenye Kamati hii ya Maji nimetembelea sehemu nyingi, visima vingi vina solar ambazo zina betri lakini visima visima vyote nilivyovitaja na najiuliza kwa nini. Naomba Mheshimiwa Waziri ajue kwa nini visima vile vinaendeshwa na solar ambazo hazina betri na wanajua Hanang ni eneo moja ambalo lina baridi kwa hiyo maji hayatapatikana kwa ufanisi kama tunavyotaka.

Mheshimiwa Spika, lingine ni lile aliloongelea Mheshimiwa Musukuma kwamba tunatoa mradi na hela zinatolewa, tuna mradi wa Kijiji cha Gehandu ambao tayari ulishapokea shilingi milioni 183 lakini mpaka leo kisima hakijatoa maji na ni muda mrefu sio mwaka mmoja ni miaka zaidi ya miwili. Naomba Waziri aweze kuona ni kwa nini jamani inachukua muda mrefu kupita kiasi kwa miradi kuwa tayari na wananchi waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba vilevile niongelee suala la Mfuko wa Maji; Mfuko huu ndiyo utakuwa ni namna ya kuondokana na tatizo hili kubwa la huduma nyeti ya maji. Naomba Waheshimiwa Wabunge tuheshimu azimio letu, nami nasema kwamba Mfuko huu wa Maji ndiyo uliofanya tutekeleze miradi mingi jamani. Kwa hiyo, sasa tukirudi nyuma tutarudisha bidii iliyokuwepo nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba ile Sh.50 ya kutokana na mafuta iongezwe lakini na vyanzo vingine navyo viongezeke kwa sababu hata hiyo Sh.50 haitaondoa tatizo linalotukabili kutokana na ukosefu wa maji. Naomba sana ndugu zangu vyanzo vingine kama simu Vodacom, Airtel na vyanzo vingine vingi vije tu kwenye maji, tukiondokana na tatizo la maji, matatizo mengine kwenye sekta zingine yataondoka vilevile. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Musukuma asikubali kwamba wale wenye petroli wamtumetume humu ndani waseme kwamba hii isitokane na petroli. (Makofi)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Kwa hiyo naomba sana kama ata…

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, taarifa..

MHE. DKT. MARY M. NAGU: ataona kwamba hilo…

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mama nakuheshimu sana, eeeeh aisee.

SPIKA: Mheshimiwa Musukuma hujaruhusiwa kusema tafadhali, Mheshimiwa Mary Nagu endelea.

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Anisamehe kwa jambo lolote kwa sababu na yeye namheshimu, lakini naomba kwa kweli suala la Mfuko wa Maji kama alivyosema Mheshimiwa Chenge na walivyosema wengine, wote tulisimamie kidete. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba jambo moja ninamshukuru Mwenyezi Mungu na nawashukuru na Marais walioniteua kuwa Waziri, Waziri wetu naye akajenge hoja kule Serikalini ili Serikali ione umuhimu wa kuongezea Mfuko huu ambao tayari kama si Wizara hii kujenga hoja, haitoshi kuongea hapa Bungeni peke yake bali kwenye Cabinet na Waziri na wenzake wengine wasaidiane kuona na Serikali inaona umuhimu huo, nina hakika ukosefu wa maji… (Makofi)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Kuhusu utaratibu

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Inaongeza…

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Kuhusu utaratibu

KUHUSU UTARATIBU

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Spika, mahitaji ya maji ya wanawake na wananchi wa Tanzania ni makubwa. Kutokana na kuona umuhimu huo, kama nilisema jambo ambalo halimpendezi yeye basi avumilie na anisamehe. Naomba sana ndugu zangu suala la maji ni muhimu, ni kweli kwamba kuna watu ambao siyo waaminifu kwenye sekta hii, lakini kuna watu ambao wanafanya kazi kwa nguvu. Naomba Mheshimiwa Waziri kama Wabunge walivyosema, aunde hata tume kuona ma-engineer ambao siyo waaminifu waondolewe ili suala la maji lionekane kama linapewa nguvu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na sitaki hata kupitisha muda wangu, kama umebaki wengine waongee kuona kwamba hoja ya kuongezea fedha Mfuko wa Maji inaendelezwa vizuri na Mheshimiwa Musukuma akiondoka ananiheshimu, namheshimu, tutaongea naye hapo nje. Ahsante sana. (Makofi)